Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Happiness Daniel Ngwando

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha Sheria ya Ndoa pale wanandoa wanapotalikiana ili kumaliza kesi zao haraka?

Supplementary Question 1

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa makuzi ya mtoto bora mwenye ubongo uliokomaa yanaanzia miaka sifuri mpaka miaka nane, wakati huo mama ndiye mlezi mkuu wa mtoto huyu, wakati anatoka kwenye familia yake anakuwa ameongozana na watoto hawa, je, Serikali haioni haja ya huu muda kuwa mrefu kwa kuwa mgogoro huu hadi unafika Mahakamani umetokea kwa Wajumbe wa nyumba kumi na Mabalozi? Kwa hiyo, mgogoro huu ulishawaka moto muda mrefu. Je, Serikali haioni huu muda wa mwaka mmoja mpaka miaka miwili ni mrefu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa mwanamke ana mchango mkubwa kwenye familia na nyumba zetu, lakini mama huyu pale unapotokea mgogoro anatoka yeye na rambo na watoto, hata alivyochangia kwenye ile familia anakuwa habebi, je, Serikali haioni haja kuepusha migogoro isiyo na lazima, wanandoa hawa wanapogombana kila mmoja aende kwa baba yake na mama yake, mlango ufungwe, ili haki itendeke? Ahsante. (Makofi/Kicheko)

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Happiness, kwa kweli anafanya kazi kubwa sana ya kuwasemea wanawake na watoto siyo tu wa Mkoa wa Ruvuma, lakini wa Tanzania nzima kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la kwanza kwamba muda wa mpaka miaka miwili wa kesi za talaka ni muda mrefu na unaweza ukaleta athari ya mtoto na hasa mtoto wa chini ya miaka minane. Kama nilivyojibu kwenye majibu ya msingi, ni kwamba muda umewekwa mahususi kwa ajili ya kuhakikisha mashauri mbalimbali yanaisha katika Mahakama ikiwemo mashauri yanayohusiana na masuala ya talaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa muda wa kumaliza Shauri la Talaka katika ngazi ya Mahakama ya Mwanzo ni miezi sita. Ndani ya miezi sita lazima shauri hili liwe limekamilika na maamuzi yametoka, lakini katika ngazi za Mahakama za Wilaya na Mahakama ya Hakimu Mkazi, ni muda wa mwaka mmoja, na katika ngazi ya juu zaidi ambayo ni Mahakama Kuu, ni miaka miwili. Kwa hiyo, mara nyingi kesi za ndoa tunaona zinaisha katika ngazi ya Mahakama ya Mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, yapo mazingira mengine ambayo kesi hizi zinaenda katika ngazi ya juu, na ndiyo maana Mahakama imeweka Mwongozo wa kutaka kuharakisha kesi hizi zisikilizwe kwa wakati ili kuweza kutoa haki hizi kwa wakati na kulinda maslahi ya wanaohusika katika mashauri haya ikiwemo watoto wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake sasa la pili ambalo amegusia suala la mwananmke au mke kufukuzwa kwenye nyumba ya ndoa, pindi anapokuwa kwenye shauri linalohusiana na masuala ya talaka, Sheria za Tanzania zinatambua na hasa Sheria ya Ndoa Sura ya 29 hairuhusu mume kumfukuza mke kwenye nyumba ya ndoa. Nyumba ya ndoa imetambulika kabisa kisheria, ni ile nyumba ambayo mume na mke wanaishi. Nyumba hiyo ya ndoa inakuwa na umiliki wa pande zote kwa maana ya mume na mke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mume haruhusiwi kumfukuza mke kwenye nyumba ya ndoa pindi wanapoingia kwenye Shauri la Talaka. Huo ni msingi ambao umewekwa katika Kifungu cha 59 cha Sheria ya Ndoa, lakini tumeona maamuzi mbalimbali yanatolewa na Mahakama kufafanua na kusisitiza msingi huu uliowekwa kwenye Kifungu hiki cha 59. Mathalani kwenye Kesi ya Elizabeth Dikene dhidi ya John Dikene ambayo ni Shauri la Ndoa (Na. 5) la Mwaka 2004. Mahakama imesisitiza msingi wa kwamba mume haruhusiwi kumfukuza mke kwenye nyumba yao ya ndoa wakiwa wako kwenye Shauri la Talaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunafahamu kwenye jamii kunakuwa na changamoto mbalimbali ambazo zinahusisha wanawake kukutana na mazingira kama hayo. Kwa hiyo, wanawake wanapokutana na mazingira kama hayo, wanachoweza kufanya ni kuchukua taratibu za kisheria ambapo anaweza kuwasilisha maombi ya zuio, yaani mhusika, tuseme mke anaweza akaandaa maombi ya dharura Mahakamani (Chamber Summons) kwa ajili ya kuiomba Mahakama kuweka zuio la muda (Temporary Injunction) ili asifukuzwe. Azuie aidha, kufukuzwa kwenye ile nyumba yao ya ndoa au kuzuia pia nyumba kuuzwa, kwa sababu kuna wakati mwingine unaweza ukashaangaa mpo kwenye Shauri la Talaka, lakini nyumba mnayoishi, yaani nyumba ya ndoa ipo katika kuuzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utaratibu umewekwa, unaweza ukaomba zuio hilo la muda ili Mahakama iweze kuingilia kati na kuzuia hatua za namna hiyo. Maombi haya yanafanyika kwenye Mahakama, ambapo inasikilizwa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri, majibu yako nadhani ameyaelewa na umempa reference nzuri, aende afuatilie. Malizia.

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa hiyo, kwa wale wanaohitaji Huduma ya Msaada wa Kisheria, katika kila halmashauri kuna dawati la kutoa Huduma ya Msaada wa Kisheria wafike ili waweze kupatiwa suluhu ya changamoto na hususan kama hii ambayo ameitaja Mheshimiwa Happiness.