Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 24 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 275 2026-05-07

Name

Happiness Daniel Ngwando

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha Sheria ya Ndoa pale wanandoa wanapotalikiana ili kumaliza kesi zao haraka?

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha Tisa cha Sheria ya Ndoa, Sura 29 kinatafsiri ndoa kuwa ni muunganiko wa mwanamke na mwanume kwa lengo la kuishi pamoja maisha yao yote. Kwa msingi huo, Sheria ya Ndoa imeweka utaratibu wa kuanza kusikilizwa kwa mashauri ya ndoa katika Bodi za Usuluhishi wa Ndoa kabla ya kufikishwa Mahakamani kwa ajili ya maombi ya talaka, lengo likiwa kutafuta suluhu zaidi kuliko kuachana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika juhudi za kuhakikisha usikilizaji na umalizaji wa mashauri, Mahakama ya Tanzania imetoa Mwongozo wa muda wa usikilizaji kesi kulingana na Mahakama ilipofunguliwa. Kwa mujibu wa Mwongozo huo, kesi zinazosikilizwa na Mahakama ya Mwanzo, ukomo wake ni miezi sita; Mahakama ya Wilaya na Hakimu Mkazi ukomo wake ni mwaka mmoja; na Mahakama Kuu ukomo wake ni miaka miwili. Aidha, Mashauri ya Talaka, kwa mujibu wa taratibu yanaweza kusikilizwa na kuamuliwa na Mahakama za Mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuimarisha taasisi ya ndoa na kuhakikisha migogoro ya ndoa inatatuliwa kwa njia ya usuluhishi, Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imeanzisha programu ya kuwajengea uwezo Wajumbe wa Bodi za Usuluhishi wa Ndoa Nchini kote. Utekelezaji wa Programu hiyo ulianza rasmi tarehe 8 Aprili, 2026 katika Mkoa wa Kagera. Lengo ni kuhakikisha wanandoa wenye migogoro wanapata suluhu stahiki kabla ya kuwasilisha mashauri yao Mahakamani kwa ajili ya maombi ya talaka.