Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Twaha Said Mwakioja

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Primary Question

MHE. TWAHA S. MWAKIOJA aliuliza: - Je, lini Serikali itawapatia maji safi na salama wananchi wa Wilaya ya Mkinga kupitia Mradi wa Tanga – Horohoro?

Supplementary Question 1

MHE. TWAHA S. MWAKIOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuishukuru Serikali kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu hayo mazuri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mradi huu wa kihistoria ambao kwa Wilaya ya Mkinga haujawahi kutokea. Pamoja na hivyo mradi huu unatekelezwa kwa kusuasua sana. Wananchi wa Mkinga wameyasubiri maji haya kwa muda mrefu, tarehe za ukamilishwaji wa mradi huu zimekuwa zikibadilishwa kila mara. Pamoja na maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuwa mradi huu tangu mwaka jana ukamilike pamoja na maelekezo ya Mheshimiwa Waziri wa Maji kwamba mradi ukamilike, lakini mradi huu haujakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufuatilia ni kwamba mkandarasi anaidai Serikali na alishasimama akaondoka eneo la mradi; je, Serikali ina kauli gani kuhusu kumlipa mkandarasi huyu ili tarehe iliyotajwa ya kukamilisha mradi huu mwezi Julai iweze kutimia na wananchi wenzangu wa Mkinga waweze kupata maji safi na salama waliyoahidiwa na Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Mkinga inatarafa mbili, mradi huu wa kihistoria na mzuri unakwenda kuwapatia maji watu wa Tarafa moja ya Mkinga. Hali ya Tarafa ya pili ya Maramba katika upatikanaji wa maji ni mbaya mbaya kweli kweli. Wakati wa kiangazi walifikia hadi kununua dumu la maji kwa shilingi 3,000 mpaka shilingi 5,000.

Je, kaka yangu Waziri wa Maji yupo tayari kuambatana na mimi katika kipindi hiki cha bajeti ili tukaione hali ya Tarafa ya Maramba na ikiwezekana atafute vyanzo vipya vya maji na ikibidi basi atuunganishe na Gridi ya Maji ya Taifa?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Mheshimiwa Twaha Said Mwakioja, Mbunge wa Mkinga kwa kazi nzuri kwanza kabisa ya ufuatiliaji wa miradi. Kwa namna alivyoongea inaonekana anafuatilia hatua kwa hatua na kujiridhisha changamoto iko wapi. Sisi Serikali kupitia Wizara ya Maji tumejipanga kuhakikisha miradi mingi ya maji inakamilika ukiwemo mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ameongelea mradi huu ni wa kihistoria. Ni kweli kabisa Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza shilingi bilioni 35.4 kuhakikisha kwamba eneo la Mkinga linapata suluhisho la kudumu. Vilevile, Serikali imeshamlipa mkandarasi shilingi bilioni 1.5 lakini pia ndani ya mwezi huu mkandarasi tunaenda kumlipa shilingi bilioni 1.7 arejee na kuendelea na mradi ili uweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua kiu ya Mheshimiwa Mbunge na Wana-Mkinga ni kuhakikisha kwamba maeneo mengi yanatatuliwa kuhakikisha kwamba wanapata huduma ya maji safi na salama, lakini tuangalie upatikanaji wa maji mpaka sasa kwa Wilaya ya Mkinga ni 72.9% na kuna vijiji 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vijiji 85, vijiji 52 vyote vina maji isipokuwa vijiji 23. Katika vijiji 23 Serikali tumejipanga kuendelea kutafuta fedha ili vijiji 23 vya Mheshimiwa Mbunge ikiwemo Maramba ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja tutaingiza kwenye mpango wa bajeti ili twende kuhakikisha kwamba Wana-Maramba kwa sauti ya Mbunge wao wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)