Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Onesmo Merdson Mnkondya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. ONESMO M. MNKONDYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha mbolea inapatikana kwa haraka wakati wa msimu wa kilimo?

Supplementary Question 1

MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Spika, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza. Pamoja na kufunguliwa kwa maghala nane na kampuni nane, lakini pia kuwepo kwa vituo 85 na mawakala 174 Wilayani Mbozi, kwa nini msimu huu mbolea aina ya DAP imechelewa kufika kwenye jimbo langu na imefika wakati wa msimu wa kilimo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Jimboni kwangu mpaka hivi ninavyozungumza, wananchi wanalia sana, wanalalamika sana, video zao ninazo na nimewatumia Mawaziri. Wanalalamika aina ya mbolea ambayo wametumia mwaka huu, pengine kutokana na baadhi ya wafanyabiashara kukosa uaminifu ama kutokana na kuchelewa kwa mbolea aina ya DAP ambayo wameizoea, wametumia mbolea mbadala na badala yake haijakidhi vigezo tulivyovizoea. Imepelekea mazao kudumaa, wananchi wameingia hasara, wananchi wanalia.

Mheshimiwa Spika, ipi kauli ya Serikali kwa wananchi hawa; na Serikali itafanya nini kuhakikisha msimu ujao wananchi hawa hawapati hasara ya aina hii na mnadhibitije hali hii isitokee kwa wakulima wangu? (Makofi)

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mnkondya kwa maswali madogo mawili mazuri na yenye kufuatilia maslahi ya wananchi wa Jimbo lake la Mbozi na Mkoa mzima wa Songwe.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza amezungumzia kwa nini mbolea ya DAP imechelewa mwaka huu. Niseme tu kwamba mbolea ya DAP sisi kama nchi tunaagiza kutoka nje ya nchi, na mahitaji ya DAP duniani sasa hivi yameongezeka hususan Brazil na nchi ya India.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mahitaji makubwa, maana yake sasa kumekuwa kama tunanyang’anyana katika ununuzi wa zile mbolea. Kwa hiyo, wale waagizaji wote waliopewa leseni za uagizaji waliweka order, na zilichelewa kutokana na mahitaji makubwa ambapo order zilikuwa zimefanyika kule nje ya nchi kwa maana ya India pamoja na Brazil

Mheshimiwa Spika, sasa kutokana na mahitaji yao kuwa makubwa, sisi tumeendelea kuzileta hizo mbolea hapa nchini na tumeendelea kuzisambaza japo zilichelewa kufika kwa wakati. Kwa hiyo, nikiri kwamba sisi kama Serikali tumeahidi katika msimu wa kilimo unaofuatia tutahakikisha waagizaji wa mbolea wanafanya hivyo kabla ya ule muda ambao msimu unakuwa umetarajia kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, suala la pili kuhusu kauli ya Serikali, sisi tunachokisema ni kwamba, moja, wananchi ama wakulima wote nchini wawe wananunua mbolea kupitia kwenye mfumo rasmi ambayo tumeuainisha, na tumetoa hiyo elimu kwa wananchi ili inapotokea mwananchi amenunua mbolea haijaleta matokeo, sisi kama Wizara tumkamate yule msambazaji wa mbolea ama wakala.

Mheshimiwa Spika, tutamkamata, tutamfungia leseni yake na vilevile tutakuwa na nafasi sasa ya kumshurutisha ikiwemo kulipa fidia kwa wananchi ambao wameathirika. Sasa, hiyo ndiyo kauli ya Serikali na ninataka wananchi wasimamie hivyo kwa kununua mbolea katika mifumo rasmi ambayo tumeiainisha kote.