Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Masache Njelu Kasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, lini Selikali itapeleka Vifaatiba na Wataalam katika Zahanati za Wilaya ya Chunya?

Supplementary Question 1

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwa kuendelea kuajiri na kutuletea wataalam pamoja na vifaatiba, lakini naomba niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kasi kubwa ya ujenzi wa zahanati pamoja na vituo vya afya, uhitaji wa vifaatiba bado ni mkubwa sana. Je, ni upi mpango wa Serikali wa haraka kwa Wilaya yetu ya Chunya kuweza kutuletea vifaatiba kwa kuwa tayari vituo vya afya vya Sangambi, Mafyeko na Matwiga vimeshakamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Pamoja na kutuletea madaktari pamoja na watumishi wa ngazi mbalimbali ndani ya Wilaya ya Chunya, bado tuna upungufu wa watumishi wasiopungua 719. Je, Serikali ina mkakati upi wa haraka itakayotuletea sisi wananchi wa Wilaya ya Chunya, ili kupunguza upungufu huo wa watumishi wa sekta ya afya?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka hii miwili ya fedha, Serikali imetenga fedha zaidi ya shilingi bilioni 100 na kuzipeleka kwenye halmashauri zetu kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba. Moja ya halmashauri ambazo zimepata fedha hizo ni pamoja na Jimbo la Chunya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Kasaka kwamba fedha za vifaatiba zinaendelea kutolewa. Katika huu mwaka wa fedha Serikali imetenga zaidi ya shilingi bilioni 63.7 kwa ajili ya vifaatiba katika halmashauri zote 184 ikiwemo halmashauri ya Chunya. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutaendelea kupeleka fedha kwenye vituo vya afya ambavyo amevitaja ili viweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali la pili la uhitaji wa watumishi na nyumba za watumishi, Serikali pia imeweka mpango kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga nyumba za watumishi pamoja na kuhakikisha kwamba watumishi wanaendelea kuajiriwa. Ndiyo maana watumishi waliojiriwa katika kipindi cha miaka minne ni zaidi ya 34,720. Zoezi hili ni endelevu, na Serikali itaendelea kuweka kibali cha ajira na kuendelea kuajiri watumishi katika halmashauri zetu.

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, lini Selikali itapeleka Vifaatiba na Wataalam katika Zahanati za Wilaya ya Chunya?

Supplementary Question 2

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwa kumaliza zahanati yetu katika Kata ya Misha ambayo inaitwa Igambilo lakini zahanati ile bado ina upungufu mkubwa wa vifaatiba. Je, ni lini Serikali itatupelekea vifaatiba katika zahanati ile?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mwakasaka kwamba tayari Serikali imeshapeleka fedha katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kwa ajili ya kununua vifaatiba kwenye zahanati zote mpya ambazo zimekamilika ikiwemo Zahanati ya Misha. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kumwelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora kufanya haraka iwezekanavyo kuhakikisha kwamba vifaatiba ambavyo vimepelekwa katika halmashauri yake vinapelekwa pia katika Zahanati ya Misha ili ianze kutoa huduma ambazo zinatarajiwa kwa wananchi.

Name

Dr. Charles Stephen Kimei

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, lini Selikali itapeleka Vifaatiba na Wataalam katika Zahanati za Wilaya ya Chunya?

Supplementary Question 3

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninaomba niiulize Serikali, je, ni lini watapeleka X-Ray kwenye Kituo cha Afya pale Kahe Magharibi ambacho kinahudumia wananchi zaidi ya 60,000 kutoka kwenye Kata za Njia Panda, Kirua-Vunjo Kusini, Kahe Magharibi yenyewe pamoja na Kahe Mashariki?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Ntahi Magharibi katika Jimbo la Vunjo ni moja ya vituo ambavyo vimewekwa kwenye awamu ya pili ambavyo tutanunua digital X-Ray 350 kwa ajili ya kupeleka kwenye hivyo vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inatambua uhitaji wa X-Ray katika kituo hicho cha afya, na tayari imeshaweka mpango wa ununuzi wa X-Ray hizo katika mwaka wa fedha ujao. (Makofi)