Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Mrisho Mashaka Gambo
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Arusha Mjini
Primary Question
MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza: - Je, lini Serikali itakamilisha mfumo wa maji taka Kiwanda cha A - Z ili kuondoa changamoto ya Wananchi wa Kata ya Olmot – Arusha?
Supplementary Question 1
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 26 mwezi wa sita mwaka 2024, wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu swali alisema kwamba, kufikia mwezi Disemba, mwaka 2024, mradi huu utakuwa umekamilika. Leo tena anajibu swali anasema hadi kufikia mwezi Juni, mwaka 2025 mradi utakuwa umekamilika. Sasa je, tuchukuwe majibu gani ya Serikali, ili tuweze kuwapelekea wananchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Sasa hivi anasema tumefika 78%, kwa hiyo, zimebakia kama 22%, kama kwa miaka isiyopungua mitatu wameweza kutekeleza kwa asilimia 78. Je, ana uhakika gani kwa muda uliobaki wa mwezi mmoja kuweza kumaliza 22%? Kama haijatekelezeka, yupo tayari kujiuzulu?
Name
Kundo Andrea Mathew
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Bariadi Mjini
Answer
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninamshukuru sana kaka yangu, Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge mahiri kabisa wa Arusha na kazi anayoifanya ya kuwatetea wananchi wake. Sisi, Serikali tunaendelea kushirikiananaye kuhakikisha kwamba, tunaendelea kutatua changamoto za maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maendeleo ni hatua kwa hatua na hatua hizo zinategemea na upatikanaji wa fedha. Mheshimiwa Mbunge anatambua hata katika jimbo lake, kila jambo amelipanga kwa wakati na kulingana na fedha zinavyopatikana. Serikali inaendelea kuhakikisha kwamba, inachukua hatua stahiki kila inapopata fedha, ilimradi tu wananchi ambao wanahitaji kupatiwa huduma ya maji au kuondolewa majitaka kazi hiyo iwe imekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge nikutoe wasiwasi, majibu ya Serikali ni kwamba, mradi huu utakamilika kwa sababu, tunatambua kipindi cha hapo mwanzo kulikuwa na changamoto na mkandarasi, lakini tatizo hilo tumeshalimaliza. Tumekaa na mkandarasi, tumeelekezana na ndiyo maana mradi huu ulikuwa 50% na kitu sasa upo 78%.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna uhakika kabisa kwamba, mpaka itakapofika muda wa mkataba wake, mradi huu unatakiwa uwe umekamilika. Kama mradi utakuwa haujakamilika, basi itabidi mkandarasi tumchukulie hatua stahiki kulingana na makubaliano katika mkataba.
Name
Margaret Simwanza Sitta
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Urambo
Primary Question
MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza: - Je, lini Serikali itakamilisha mfumo wa maji taka Kiwanda cha A - Z ili kuondoa changamoto ya Wananchi wa Kata ya Olmot – Arusha?
Supplementary Question 2
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Wananchi wa Urambo wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu sana upatikanaji wa maji kutoka Lake Victoria kutokana na shida kubwa ya maji tuliyonayo. Je, ni lini sasa mradi huu utakamilika?
Name
Kundo Andrea Mathew
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Bariadi Mjini
Answer
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninapenda kujibu swali la mama yangu, Mheshimiwa Margaret Sitta. Mradi wa Urambo, Kaliua pamoja na maeneo mengine unagharimu shilingi bilioni 143. Mradi huu umeshafikia 70%. Vilevile kuna maeneo ambayo tayari kulikuwa na existing infrastructure, tulitoa maelekezo na tayari sasa wameshaanza kufanya tathmini ya kuona kuna umbali gani kutoka kwenye matenki na kwenda kwenye exiting infrastructure.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimtoe hofu kwamba tayari wataalamu wetu wapo site wanafanya kazi. Muda siyo mrefu mradi utakapokamilika wataanza kupata huduma ya maji safi na salama kutoka Ziwa Viktoria, ahsante.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved