Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Janeth Elias Mahawanga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JANETH E. MAHAWANGA aliuliza: - Je, Serikali ina Sera za kuwawezesha wanawake wajasiriamali kutumia teknolojia ya habari kuongeza ufanisi wa biashara zao?

Supplementary Question 1

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nilikuwa na swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ni kwa namna gani Serikali inashirikiana na sekta binafsi ili kuhakikisha wanawake wajasiriamali wanapata vifaa na mafunzo ya TEHAMA ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidigiti? (Makofi)

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mahawanga, ni kwamba Serikali tayari imeshaanza utaratibu wa kuhakikisha kwanza inashirikiana na sekta binafsi kupitia Mabaraza ya Biashara yaliyoko nchini kote katika mikoa, lakini pia Baraza la Biashara la Wilaya na ngazi hizo zinaratibiwa kupitia halmashauri pamoja na Baraza la Taifa la Biashara.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, upo mpango mwingine wa Serikali kupitia Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, vyote kwa pamoja vinafanya kazi kwanza ya kuwatambua wafanyabiashara, na pili kuwaratibu na kuwasajili, na hatua ya tatu, wanafanya mafunzo kwenye maeneo haya ya biashara, na ni biashara zote za wajasiriamali katika nafasi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, upo mkakati mzuri ambao umeanzishwa hivi karibuni kupitia agizo la Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri wa Viwanda na Biashara ambao unaitwa MKUMBI kama Mkakati wa Kuboresha Mazingira ya Biashara.

Mheshimiwa Spika, tayari wameshaanza kuangalia namna gani wanaweza kuboresha mazingira ya biashara ikiwemo hii ya mtandao na kupitia Sera ya Biashara Toleo la Mwaka 2023 ambayo inahusiana na masuala ya kuboresha biashara za mtandaoni.

Mheshimiwa Spika, pia, utoaji wa anwani za makazi kulingana na sera ya posta, zote hizi zimekuwa zikitumika kuweza kusaidia hawa wajasiriamali wadogo wadogo waweze kupata uratibu huo. Wanapata mawasiliano mazuri zaidi kupia Wizara ya Mawasiliano ambapo kwa Mfuko wa UCSAF wameanza kutoa kompyuta kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo shule na kuwaanda wafanyabiashara kupitia elimu ya TEHAMA. (Makofi)