Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 27 2026-04-08

Name

Edibily Kinyoma Kazala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Vijijini

Primary Question

MHE. EDIBILY K. KINYOMA aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wananufaika na uwepo wa mwekezaji wa Kitalu cha Makere Forest Reserve?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wameendelea kunufaika na uwepo wa mwekezaji katika Kitalu cha Makere Forest Reserve kwa kupata mgao wa fedha za maendeleo ya jamii kiasi kisichopungua shilingi milioni 12 kila mwaka kinacholipwa na mwekezaji na kugawanywa kwa vijiji ili kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kuzingatia vipaumbele vya vijiji husika. Mathalani, katika mwaka wa fedha 2024/2025 Vijiji vya Kagera Nkanda, Chekenya na Kabulanzwili vililipwa shilingi 4,356,435.67 kila kimoja kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo ya jamii. Vilevile, mgao wa fedha zinazotokana na 25% ya ada ya wanyamapori wanaowindwa katika kitalu husika kwa mujibu wa kifungu cha 137 cha Sheria ya Fedha ya mwaka 2025 zinalipwa na Serikali kwa halmashauri husika. Asilimia 60 ya fedha hizo hutumika kutekeleza miradi ya maendeleo na 40% shughuli za uhifadhi katika vijiji vinavyozunguka kitalu husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na manufaa yaliyotajwa, katika kipindi cha mwaka 2024/2025 na 2025/2026 mwekezaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania wamechangia miradi ya jamii yenye thamani ya shilingi 166,475,000. Fedha hizo zimetumika kufadhili kambi ya huduma ya matibabu ya macho katika Halmashauri ya Kasulu, madawati 100 ambapo katika Shule ya Msingi Chekenya wamepata madawati 25, Shule ya Msingi Nyakasanda walipata madawati 25 na Shule ya Msingi Nyantuku ambao wamepata madawati 50. Vilevile na uchimbaji wa visima vya maji sita katika Shule za Msingi Kamganza, Kasasa, Mwitiri, Chekenya na Nyantuki pamoja na Kituo cha Afya cha Kagerankanda. (Makofi)