Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 2 Sitting 6 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Waziri wa Mifugo na Uvuvi 103 2026-02-03

Name

Mgore Miraji Kigera

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. MGORE M. KIGERA aliuliza: -

Je, Serikali ipo tayari kutoa mikopo kwa wafugaji wa samaki wa vizimba Musoma ili kutoa ajira kwa vijana?

Name

Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, ninaomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mgore Miraji Kigera, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) inaendelea na zoezi la utoaji wa mikopo ya pembejeo za ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba ambapo katika mikopo ya awamu ya kwanza jumla ya vizimba 47 vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.126 vimetolewa, kama mikopo ya masharti nafuu isiyo na riba kwa wanufaika 130 nchini ikiwemo vijana kutoka Musoma Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa kuongeza ushiriki wa vijana katika ufugaji wa samaki kwa vizimba, Wizara inatekeleza Programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (BBT-Uvuvi) kwa kutoa mafunzo kwa vitendo na mikopo yenye masharti nafuu. Lengo ni kuongeza uzalishaji na kutoa ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Wizara imepokea kiasi cha shilingi bilioni saba kutoka Hazina kwa ajili ya kuwezesha vijana kupata mitaji kupitia mikopo yenye masharti nafuu. Fedha hizo zitatumika kukopesha vijana 308 waliohitimu mafunzo hayo wakiwemo vijana 14 kutoka Musoma Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Wizara inatarajia kupokea sehemu ya shilingi bilioni 200 ambazo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ndani ya siku 100 zitakazoelekezwa katika kuwezesha mikopo ya vizimba. Katika mgao wa fedha hizo, vijana wa Musoma watafaidika na mikopo hiyo. Aidha, Wizara inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya fedha ili kuendelea kutoa mikopo ya ufugaji wa samaki kwa vizimba katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.