Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 8 Works, Transport and Communication Wizara ya Uchukuzi 85 2026-04-14

Name

Janeth Elias Mahawanga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JANETH E. MAHAWANGA aliuliza: -

Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha wanawake wanashiriki katika miradi mikubwa ya uchukuzi, ikiwemo Mradi wa SGR?

Name

David Mwakiposa Kihenzile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kusini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Janeth Elias Mahawanga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeweka sera, sheria na miongozo mbalimbali inayolenga kuhimiza na kuhakikisha usawa wa kijinsia katika ajira. Katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo ujenzi wa SGR, wakandarasi na washauri wanawajibika kuzingatia masharti ya mikataba, pamoja na sera za Kitaifa ambazo zinataka utoaji wa fursa sawa za ajira kwa wanawake na wanaume katika kada mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa masharti ya mikataba ya ujenzi inayotumika katika Ujenzi wa SGR, mkandarasi na mshauri, wanatakiwa kufuata sheria zote za nchi, zikiwemo zile zinazohusu ajira, kazi na usawa wa kijinsia. Hivyo, Serikali imeendelea kusisitiza utekelezaji wa matakwa haya ili kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika miradi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia, inaendelea kufanya ufuatiliaji na tathmini ya mara kwa mara ya utekelezaji wa sera na miongozo hiyo kwa lengo la kuhakikisha kuwa, malengo ya usawa wa kijinsia yanafikiwa na wanawake wanapata fursa stahiki za kushiriki katika miradi mikubwa ya kimaendeleo nchini.