Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 8 Planning and Investment Ofisi ya Rais: Mipango na Uwekezaji 77 2026-04-14

Name

Mgore Miraji Kigera

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. MGORE M. KIGERA aliuliza: -

Je, upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha mwekezaji wa Kiwanda cha MUTEX anaanza uzalishaji kwa haraka?

Name

Dr. Pius Stephen Chaya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgore Miraji Kigera, Mbunge kutoka Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Musoma Textile Mills Tanzania Limited (MUTEX) kilianzishwa kwa lengo la kuongeza thamani ya pamba iliyozalishwa nchini, kutoa ajira na kuchangia maendeleo ya viwanda katika Ukanda wa Ziwa Victoria na Tanzania kwa ujumla. Hata hivyo, hadi sasa kiwanda hiki hakifanyi kazi, na hivyo kinasimamiwa na Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika juhudi za kufufua kiwanda hiki, Serikali ilipokea maombi ya mwekezaji mwenye nia ya kuwekeza kwenye eneo hili. Hivyo basi, Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, walianza mara moja mchakato wa kufanya majadiliano na mwekezaji huyo ambapo pande zote mbili zilifikia makubaliano kuhusu masharti mapya ya uwekezaji. Kufuatia makubaliano hayo, rasimu ya mkataba iliandaliwa na kuwasilishwa kwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya mapitio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mchakato wa kufanyia kazi maboresho yaliyopendekezwa kwenye mkataba unaendelea na mara tu utakapokamilika, mkataba utasainiwa rasmi kati ya Serikali na mwekezaji. Hatua hiyo itafuatiwa na kukabidhiwa kwa kiwanda pamoja na nyaraka zote za umiliki kwa mwekezaji ili aweze kuanza utekelezaji wa uwekezaji na kurejesha uzalishaji wa kiwanda hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.