Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 7 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Waziri wa Mifugo na Uvuvi 63 2026-04-13

Name

Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Primary Question

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia wafugaji wa Korogwe Vijijini na Mkoa wa Tanga kwa ujumla kupata soko na bei ya uhakika ya maziwa?

Name

Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Ninaomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama Ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Taasisi ya Bodi ya Maziwa, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga na Chama cha Ushirika cha Wazalishaji Maziwa Mkoa wa Tanga (TDCU), wanaendelea na utatuzi wa changamoto za kiwanda cha kusindika maziwa cha Tanga almaarufu kama Tanga Fresh ambacho kina uwezo wa kusindika maziwa lita 120,000 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kiwanda hicho ndicho soko kubwa la maziwa yote ya Mkoa wa Tanga na Mikoa ya jirani. Changamoto za kiwanda hicho ni pamoja na upungufu wa mtaji na gharama kubwa za uendeshaji na hivyo kushindwa kununua maziwa ya wafugaji kwa bei ya uhakika. Kutatuliwa kwa changamoto hizo kutasaidia wafugaji wa Korogwe vijijini na Mkoa wa Tanga kwa ujumla kupata soko na bei ya uhakika ya maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatekeleza mradi wa miaka kumi wa mageuzi ya tasnia ya maziwa na mabadiliko ya tabianchi katika Mikoa 13 nchini, Mikoa nane Tanzania Bara na Mikoa mitano Zanzibar ikiwemo Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo utaboresha mnyororo wa thamani wa maziwa ikiwemo vituo vya kukusanyia maziwa kutoka kwa wafugaji kabla ya kupeleka kiwandani. Hatua hizi, zitasaidia wafugaji wa Korogwe Vijijini na Mkoa wa Tanga kwa ujumla kupata soko na bei ya uhakika ya maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.