Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Haji Kombo Mdowe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 1

MHE. MDOWE HAJI KOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa ruhusa yako. Kwanza ninaomba niishukuru na kuipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kazi kubwa ambayo inaendelea kuifanya katika nchi yetu. Pia ninashukuru kwa majibu yao ambayo wamenipa, kwa sababu majibu haya yametoa mwongozo mzuri katika suala letu hili. Hata hivyo, ninayo maswali mawili ya nyongeza katika jambo hili: -

(a) Je, ni vigezo gani vya kiulinzi, kiutawala na kimiundombinu vinavyotakiwa kukamilika ili kituo cha Polisi kiweze kupandishwa hadhi?

(b) Je, ni jukumu la nani hasa kukamilisha vigezo vya kiulinzi na kimiundombinu katika vituo vya Polisi nchini?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mdowe Haji Kombo, Mbunge wa Jimbo la Nungwi kwa maswali yake mawili ya nyongeza, ambayo ni muhimu sana. Ninapenda kumfahamisha Mheshimiwa Mdowe kwamba, vigezo vya kimiundombinu ni madaraja ya majengo ya Jeshi la Polisi ambayo yapo kwenye daraja la C1, C, B na E, kutegemeana na aina au eneo linalotaka kujengwa kituo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ombi ambalo wamewasilisha wao kwa Kituo cha Polisi cha Nungwi, kwa sasa kipo kwenye daraja C. Kwa hiyo, kinaomba kupandishwa hadhi kwenda kwenye daraja B. Ili kufikia kiwango cha daraja B, basi ni lazima miundombinu hiyo ya jengo la kituo cha Polisi iwe imekidhi vigezo vya daraja B la vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika vigezo vya kiulinzi ni kuangalia parameter za eneo ambalo linaombewa kupandishwa daraja la eneo hilo. Kwa mfano, hivi sasa Jeshi la Polisi linayo maeneo ambayo yamepewa hadhi ya mikoa, lakini kiutawala yapo hadhi ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano halisi ni kwa Mkoa wa Dar es Salaam ambao umepewa kanda maalum, na ndani yake zile wilaya zimepewa hadhi ya mikoa. Hiyo inatokana na hali ya kiutawala, na pia mahitaji ya kiulinzi katika eneo la Mkoa husika wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa vigezo hivyo, watakapowasilisha maombi yao kupitia Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, kwa maana ya Kamati ya Usalama ya Wilaya, itaweza kuchakata na kutathmini hali ya vigezo vyote vitatu kama vitakuwa vimefikiwa na kushauri ipasavyo kwenye ngazi inayofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili kwamba, ni nani ambaye ana jukumu hilo, nilieleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, ninauomba uongozi wa Jimbo la Nungwi kwamba uwasilishe pendekezo hilo kwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, kwa maana ya Kamati ya Usalama ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.

Name

Imamu Mtumwa Vuai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magomeni

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 2

MHE. IMAMU MTUMWA VUAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutumia teknolojia ya kisasa kama CCTV Camera na mifumo ya kidigitali katika kuboresha ulinzi nchini badala ya kutegemea vituo vya Polisi pekee?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninampongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Imamu Vuai, Mbunge wa Magomeni kwa swali lake la msingi na muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba, dunia kwa sasa imekua kwa kiasi kikubwa kwenye eneo la teknolojia. Kutokana na kukua huko, hata Dira yetu ya Maendeleo ya 2050 imeelekeza kwamba tutumie teknolojia katika kukuza uchumi na kuimarisha ufanisi. Hivyo nikubaliane na rai yake inayosema kwamba sasa Jeshi la Polisi au vyombo vya ulinzi na usalama vijielekeze zaidi kwenye teknolojia katika kuimarisha mifumo ya kiulinzi, na huko ndipo ambapo kwa sasa dunia ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kujielekeza huko kuna faida nyingi, zikiwemo kupunguza idadi ya makosa (crime rates) kwenye maeneo mbalimbali, vilevile kuna kupatikana kwa usahihi wa taarifa za kiusalama au kwa wale wanaotenda makosa na bila ya kumwonea mtu kwa sababu tumetumia teknolojia. Aidha, tunaweza kupunguza matumizi makubwa ya rasilimali watu na kutumia mifumo na vifaa badala ya idadi kubwa ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo hili, na kwa kuona umuhimu huu, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeanza mchakato wa kuliangalia upya jambo hili. Kwa bahati nzuri, kwa upande wa Zanzibar jambo hili lilishaanza kwa muda kidogo. Tumeona katika eneo la Mji Mkongwe limeondoa au kupunguza kwa kiasi kikubwa sana crime rate kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeliangalia jambo hili katika maeneo makuu matatu. Kwa kuanzia, kwanza, Serikali inataka kwenda kwenye miji salama (safer city), na itaanza miji mikubwa; pili, tunataka kwenda kwenye barabara salama kuhakikisha kwamba tunapunguza ajali kwa kutumia mifumo; na tatu, katika ukaguzi wa magari kwa maana vehicle inspection, nalo hilo tuko katika mwelekeo wa kuelekea huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.

Name

Ado Shaibu Ado

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Tunduru Kaskazini

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 3

MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa, Kituo Kikukuu cha Polisi cha Wilaya ya Tunduru ni kikongwe na kidogo, katika mazingira ambayo yanalazimisha sisi akina Ado ambao huitwa mara kwa mara pale kuhojiwa, tumewashuhudia makamanda wetu wakiwa wanaendesha mahojiano ndani ya chumba kimoja kwa watuhumiwa zaidi ya mmoja, hali ambayo inaondoa kabisa weledi, je, ni lini, Serikali itafikiria kujenga kituo kipya cha Wilaya ya Tunduru ili makamanda wetu wafanye kazi kwa weledi na utaratibu unaohitajika, ikiwemo faragha?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru na kumpomgeza sana Mheshimiwa Ado Shaibu, lakini ninaomba nimkumbushe tu kwamba kituo cha Polisi alichokitaja na vituo vyote vya Polisi nchini, uwepo wake siyo kwa ajili ya akina Ado Shaibu, ni kwa ajili ya wale wote ambao watakuwa wanahalifu sheria za nchi hii. kwa hiyo, Serikali inaendelea na hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa vituo vya Polisi vya ngazi ya wilaya, ambavyo kwa taarifa yetu ya awali tulisema kwamba tuna vituo vya Polisi 75 vya ngazi ya wilaya, ambavyo ama vinahitaji ukarabati au vinahitaji kujengwa upya kwa lengo la kufikisha hadhi ya daraja B, kwa maana ya kituo cha wilaya, kwa hiyo, na kituo cha wilaya ambayo Mheshimiwa Ado Shaibu amekitamka, nacho kipo kwenye mpango huo. Kadiri ya hali ya upatikanaji wa fedha tutaendelea kujenga vituo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.

Name

Salum Khamis Salim

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bububu

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 4

MHE. SALUM KHAMIS SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye Jimbo langu la Bububu kumejengwa kituo cha ghorofa kwa kuzingatia matumizi ya eneo husika kabla ya uhuru. Je, ni kigezo gani kilichotumika kujenga nyumba ya chini ilhali matumizi yamekua na pia unyeti wa eneo?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Salum Salim, Mheshimiwa Mbunge ambaye amesema kwamba, kwenye jimbo lake kumejengwa kituo cha Polisi kabla ya uhuru na ni cha ghorofa. Sasa, anataka kujua ni kigezo gani kilichotumika kujenga nyumba ya chini badala ya ghorofa kama ambavyo kwa wakati huo vituo vimejengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za makazi kwa ajili ya Askari ni moja kati ya hitaji kubwa tulilonalo katika Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama. Tunakiri kwamba kadiri siku zinavyoendelea na ongezeko la idadi ya watu linakua kubwa na matumzi ya ardhi yanazidi kuwa makubwa. Hivyo, inapendekezwa na kushauriwa kwamba, kadiri iwezekanavyo, tujenge nyumba za ghorofa badala ya nyumba za chini kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya hali ya kibajeti na kwa mujibu wa uharaka na uhitaji wa makazi katika eneo hilo, ndiyo sababu kuu inayosababisha kujenga nyumba za chini katika baadhi ya maeneo. Vilevile kuendelea na ujenzi wa nyumba za ghorofa kwenye yale maeneo ambayo tayari fedha zipo, na pia kule ambapo wamekosa maeneo ya kujenga nyumba za chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Dodoma hapa tulipo, tayari tunaendelea na ujenzi wa zaidi ya nyumba sita za ghorofa kwa ajili ya makazi ya Askari. Kabla ya ukoloni kulikuwa kuna nyumba za chini ndogo ndogo ambazo hazina hadhi na hali nzuri. Kwa hiyo, kazi ya ujenzi wa nyumba za ghorofa inaendelea nchi nzima kwa kadiri ya hali ya fedha, kwa maana ya bajeti, itakavyoruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.

Name

Japhael Masanja Lufungija

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 5

MHE. JAPHAEL M. LUFUNGIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi. Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Maaskari wa Polisi katika Jimbo la Ulyankulu, wafanyabiashara wa Kata ya Uyowa Kijiji cha Mwamnange, pamoja na wafanyabiashara wa Kata ya Kona Nne Kijiji cha King'wangoko walijenga kituo cha Polisi kwa ajili ya malengo ya kuimarisha usalama wao. Hata hivyo, vituo hivi vimeshindwa kukamilika. Mbaya zaidi, Kituo cha Polisi cha Kona Nne kimepanga kwenye nyumba ya mtu, ambapo zaidi ya miaka tisa hajalipwa. Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na kukamilika kwa vituo vya Polisi hivi viwili?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Lufungija kwa hoja yake ya kukamilisha vituo vya Polisi katika eneo la Ulyankulu kama ambavyo ameainisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati najibu swali la msingi na la awali katika Bunge hili, nilieleza kwamba vipo vituo 77 vya Polisi katika kata mbalimbali ambavyo bado havijamalizika, na vipo katika ngazi ya maboma. Tulieleza kwamba kwenye awamu ya kwanza ya ujenzi wa vituo, vituo 77 hivi vitaingia kwa ajili ya kumaliziwa na vile vipya kuweza kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Ulyankulu kwamba, mara baada ya kutenga fedha na kupata bajeti hiyo mwaka wa fedha 2026/2027, tutaanza kukamilisha maboma haya ya vituo vya Polisi ambavyo bado havijakamalika.

Name

Nuru Issa Kashakari

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Kusini

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 6

MHE. NURU I. KASHAKARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Kigoma Kusini lina vituo vya Polisi vitano ambavyo ni Kituo cha Polisi Kazuramimba, Kituo cha Polisi Sigunga, Kituo cha Polisi Ilagala, na Kituo cha Polisi Buhingu. Vituo hivi havina majengo, badala yake wamekodi majengo binafsi kwa watu. Je, ni lini Serikali itajenga vituo hivi vya Polisi ili kuleta hadhi ya Jeshi la Polisi?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Nuru, Mbunge wa Kigoma Kusini kwa hoja yake ya kuimarisha vituo vya Polisi na kujenga vituo vya Polisi kwenye maeneo aliyoyatamka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyoeleza kwamba kimsingi, maswali yanayoongezeka tayari majibu yake tulishayatoa, sasa na hili swali kuhusu lini; maana yake ni kwamba tutaanza mwaka wa fedha wa 2026/2027 kama mpango wetu tulivyoutoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru na ninaomba kuwasilisha.

Name

Asha Omar Rashid

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 7

MHE. ASHA OMAR RASHID: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii na mimi niulize swali la nyongeza. Ninaishukuru sana Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kutujengea Kituo cha Polisi pale Matangatuani, lakini pale bado hatuna makazi ya Polisi. Je, ni lini Serikali itajenga makazi bora ya nyumba za Polisi pale Matangatuani Wilaya ya Micheweni Pemba? (Makofi)

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, makazi ya Askari yanaendelea kujengwa hivi sasa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Mkoa wa Kaskazini Pemba. Eneo la Matangatuani lipo kwenye mpango. Sasa, kwamba ni lini, itategemea na hali ya upatikanaji wa fedha ili tuweze kukamilisha ujenzi na pia kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.

Name

Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 8

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Maswa hatuna kabisa kituo cha Polisi kwa ajili ya OCD wa wilaya yetu. Mwaka 2025 tuliambiwa Serikali ilikuwa imetenga fedha kwa ajili ya kuanza kujenga Kituo cha Polisi cha Wilaya. Je, mpango huo umeishia wapi, kwa sababu mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Mashimba, Mbunge wa Maswa kwa swali lake la msingi na muhimu kama ambavyo imeelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa fedha zilitengwa mwaka wa fedha 2025/2026 na bado tunaendelea na muda wa utekelezaji wa bajeti hiyo. Ninapenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutampa taarifa rasmi ya kwamba lini kazi ya ujenzi wa kituo chake kwa mujibu wa hali ya upatikanaji wa fedha katika kipindi kilichobaki itaweza kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.

Name

Mahesh Shah Bolisha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Micheweni

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 9

MHE. MAHESH SHAH AKLUSHA BOLISHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Wizara ina mpango wowote wa kujenga kituo kidogo katika Wadi ya Kiuyu karibu na eneo la Mabutu kwa kuwa eneo hili limewekwa kwa ajili ya uwekezaji, na ni prime location kwa ajili ya wawekezaji kutoka nje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafikiri tuna kituo kikubwa kinajengwa cha Polisi ndani ya Jimbo la Micheweni, lakini patakuwa ni mbali kidogo kutoka Mabutu mpaka hapo kituo kinapojengwa. Je, tuna mpango wowote wa kujenga kituo kidogo katika eneo la Mabutu karibu na eneo la uwekezaji kwa ajili ya security? Ahsante.

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mahesh, Mbunge wa Micheweni kwa swali lake ambalo ameomba kujengewa kituo kidogo katika eneo la Kiuyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulieleza kwenye mpango wa jumla wa ujenzi wa vituo vya Polisi kwamba, azma ya Serikali ni kufikisha huduma za kiusalama katika kila kata kuwe na kituo cha Polisi, lakini utekelezaji wa azma hiyo utategemea sana hali halisi ya upatikanaji wa fedha, na vile vile mpango wa hali ya usalama katika maeneo husika. Ndiyo maana tukaja na ule mpango mkuu wa kwamba tutaanza na maeneo ambayo yamebainika kiusalama yana uhitaji wa haraka zaidi halafu baadaye twende kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwahidi tu Mheshimiwa Mahesh kwamba hoja yake tunaichukua, na ikiwa Kituo cha Kiuyu kipo kwenye mpango wa dharura, basi kitaweza kujengwa katika utaratibu wa mpango huu.

Name

Morris Joseph Makoi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 10

MHE. MORRIS J. MAKOI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Katika Jimbo la Moshi Vijijini, wananchi wamekuwa mstari wa mbele sana kujenga vituo vya Polisi kwa kujitolea na hapa tunapoongea vituo vingi vya Polisi vimekamilika kikiwemo Kituo cha Polisi cha Kata ya Okaoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, Serikali ina mpango gani kuongeza Askari katika vituo hivi katika Jimbo la Moshi Vijijini kwa kuwa vituo vyote ambavyo vimejengwa na wananchi vina Askari mmoja mmoja na wakati…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Makoi, jambo la kwanza unauliza swali la pili. Sasa ni sababu majina hatuyashiki vizuri, kwa hiyo, ungeuliza kifupi zaidi.

MHE. MORRIS J. MAKOI: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninaomba niulize moja. Serikali ina mpango gani kuongeza Askari katika vituo mbalimbali vya Polisi katika Jimbo la Moshi Vijijini ambavyo wananchi wamejenga kwa kujitolea?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Morris, Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini kwa swali lake la msingi. Kwanza ninampongeza na kuwapongeza wananchi wa Moshi Vijijini kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuunga mkono Serikali kwa ujenzi wa vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimhakikishie kwamba maeneo yote nchini ambayo yatakuwa yamekamilika ujenzi wa vituo na vikawa vimefikia katika vile viwango ambavyo nimevieleza katika majibu ya awali, basi tutaendelea kupeleka Askari kwa mujibu wa uhitaji katika maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.

Name

Hemed Sumry Haidary

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 11

MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Jimbo la Mpanda Mjini, Kituo cha Polisi cha Wilaya kilikuwa katikati ya Mji wa Mpanda na baadaye Jeshi la Polisi wakajenga kituo kipya nje ya mji. Nilitaka kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, ni lini sasa pale katikati ya Mji wa Mpanda ambapo ndiyo kuna shughuli nyingi za kiuchumi watatuwekea kituo kidogo ambacho kitaendelea kusaidiana na kile kituo kikubwa ambacho kiko umbali wa kilometa sita mpaka 10 kutoka kwenye baadhi ya kata?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge wa Mpanda Mjini kwa hoja yake ya msingi na muhimu. Kwanza ninadhani tumshukuru kwa kupongeza jitihada za Serikali za ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Jimbo la Mpanda Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhusu ni lini kituo kidogo kitajengwa kwenye karibu na maeneo ya makazi ya watu ambapo kuna mkusanyiko, nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakaa pamoja, tuone namna gani tunaweza kushirikiana na wananchi kwenye eneo hilo, kwa vile ni kituo kidogo cha daraja C ili kusudi tuweze kukijenga kwa haraka zaidi.

Name

Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 12

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Kituo cha Wilaya ya Masasi kilijengwa mwaka 1958 na hakina hadhi ya kuwa kituo cha wilaya, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo kipya cha Polisi chenye hadhi ya wilaya ya Masasi?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake la kuimarisha Kituo cha Masasi ambacho kimejengwa kwa muda mrefu na kipo katika hadhi au ngazi ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili nimeshalijibu, lakini naomba niongezee kwamba Kituo cha Masasi ni miongoni mwa vituo 75 vya ngazi ya wilaya ambavyo ama tutavifanyia ukarabati au kuvijenga upya katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuanzia mwaka wa fedha 2026/2027 tutaendelea na mpango wetu wa utekelezaji wa kuimarisha vituo hivi 75 vya wilaya kikiwepo Kituo cha Wilaya cha Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.

Name

Zainab Rashid Kawawa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 13

MHE. ZAINAB R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Liwale katika Mkoa wa Lindi haina kituo rasmi cha Polisi na wilaya hiyo ilishatenga eneo kubwa na zuri kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi cha Wilaya. Je, ni lini sasa Serikali itatujengea kituo cha Polisi cha daraja A?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Zainab kwa swali lake la msingi la kuomba Kituo cha Polisi cha Wilaya ambapo kwa sasa hakipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuweke vizuri kumbukumbu; kwa kuwa ni Kituo cha Polisi cha Wilaya, maana yake hakitakuwa daraja A, kitakuwa ni daraja B. Kwa hiyo, nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tunachukua hoja yake, na kama nilivyoeleza kwenye jibu la msingi ni kwamba katika vituo 75 vya wilaya na cha kwake kipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutatoa umuhimu kwenye maeneo ambayo hayana kabisa vituo vya Polisi vya wilaya ili kusudi naye tuweze kumjengea.

Name

Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 14

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Tumbi ni moja kati ya kata za pembezoni katika Jimbo la Tabora Mjini, lakini haina kituo cha Polisi kabisa, hivyo kusababisha Askari watoke mjini kwenda Tumbi kwa ajili ya kushughulikia matukio ya kihalifu. Nini mpango wa Serikali kuhakikisha wanajenga Kituo cha Polisi katika Kata ya Tumbi?

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Hawa, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kwa swali lake la msingi. Niseme tu kwamba nilivyokuwa nikieleza mpango wetu wa Serikali wa kujenga vituo vya Polisi, nilisema kuwa tuna uhitaji wa ujenzi wa vituo vya Polisi kwenye kata 3,900 na kata hii aliyoieleza Mheshimiwa Mbunge ni miongoni mwa kata hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lini? Itategemea na mpango ulivyoelekeza na hali ya upatikanaji wa fedha tuweze kumpatia kituo cha Polisi kwenye kata hiyo. Ahsante

Name

Moshi Selemani Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tanganyika

Primary Question

MHE. MDOWE HAJI KOMBO aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kukipandisha hadhi Kituo cha Polisi Nungwi kutokana na ukuaji wa mji huo kiutalii?

Supplementary Question 15

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Tanganyika ni miongoni mwa wilaya ambazo hazina kituo cha Polisi na halmashauri ya wilaya ilianzisha ujenzi, na mimi kama Mbunge, nimechangia kwenye hicho kituo; na Serikali iliahidi kutoa shilingi milioni 20, lakini mpaka sasa ni mwaka wa tatu. Ni lini Serikali itakamilisha Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Tanganyika? Ahsante.

Name

Mohammed Mahmoud Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chaani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Selemani kwa swali lake la msingi na ninawapongeza sana kwa kuchangia fedha kwenye ujenzi wa vituo vya Polisi ambao ni uhitaji mkubwa kwa usalama wa raia na mali zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumpongeza Mheshimiwa Selemani, nimjibu tu kwamba vituo ambavyo havijamalizika nilitoa maelezo ya jumla hapa kwenye maboma 77 na nimeeleza kwamba tutaendelea kusaidia ili kukamilisha vituo hivyo kikiwemo kituo chake Mheshimiwa Selemani na tumhakikishie tu kwamba tutajitahidi mwaka wa fedha 2026/2027 tuweze kumsaidia na kukamilisha hiyo fedha ambayo tumeahidi kutoa ili tuweze kukamilisha kituo hicho. Ahsante sana.