Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Christina Solomon Mndeme
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. CHRISTINA S. MNDEME aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kupanua wigo wa huduma za Watoto Njiti katika Vituo vya Afya vya Mkoa wa Tabora?
Supplementary Question 1
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuboresha Sekta ya Afya. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, zimekuwepo changamoto ambazo huwapata baadhi ya wakinamama ambao baada ya kuruhusiwa kutoka hospitali kukosa uelewa thabiti wa kuendelea na malezi ya mtoto njiti mara wanaporudi nyumbani. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu ya malezi kwa wakinamama wanapokuwa wamerudi nyumbani ili aendelee kumlea vizuri mtoto anapokuwa nyumbani ili kupunguza uwezekano wa kutokea vifo vya mtoto njiti anapokuwa nyumbani?
Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, kuna utafiti wowote umefanyika ili kupunguza hili tatizo la watoto kuzaliwa kabla ya muda na kama utafiti huo umefanyika, je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu hii kwa wananchi? (Makofi)
Name
Dr. Florence George Samizi
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Muhambwe
Answer
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kutoka Tabora kwa jinsi ambavyo anawapigania wanawake wa Tabora ili waendelee kupata watoto waliozaliwa njiti na kuwa salama. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, ninaomba kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali imeweka mwongozo kwa ajili ya kutoa elimu kwa wakinamama hawa wanapokwenda nyumbani ili elimu hii itolewe kwa mtiririko.
Mheshimiwa Spika, watoto hawa wanaozaliwa njiti ikumbukwe kwamba viungo vyao ambavyo vinawasaidia wao kuishi ikiwemo ini, mifupa, Ngozi, vyote navyo vimezaliwa vikiwa havijakomaa. Hivyo, msingi wa elimu hii ni kuwasaidia waweze kujua jinsi ya kuwakinga, waweze kuwalinda na wale watoto wawe salama ikiwemo kwanza kabisa, kuwasaidia kuwapatia joto.
Mheshimiwa Spika, elimu tunayowapatia ni kuendelea kufanya mamakangaroo ambapo mama huyu anatakiwa kumlea huyu mtoto wakati wote huku amemweka kifuani na akiendelea kupata joto la mama kwa kushikana ngozi kwa ngozi.
Mheshimiwa Spika, vilevile, tunaendelea kumfundisha huyu mama umuhimu wa kumnyonyesha ziwa la mama ambalo lina faida zaidi ya chakula. Mtoto huyu amezaliwa akiwa kinga yake pia ipo chini. Kwa hiyo, kwa kumnyonyesha ziwa la mama inamsaidia pia huyu mtoto aweze kupata kinga ili aepukane na magonjwa. Pia, kwa vile huyu mtoto njiti amezaliwa bila ya kuwa na kinga, tunamfundisha mama aendelee kumtenga huyu mtoto na watu wengine ili asiweze kupata maambukizi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tunamfundisha huyu mama jinsi ya kuendelea kumpatia huyu mtoto chanjo pale muda utakapofika ili asiweze kupata maambukizi. Tunaendelea kumwambia huyu mama amlete mtoto kliniki kwa kufuata tarehe tulizompangia ili tuweze kuendelea kumpa elimu zaidi, na vile vile kuendelea kumpatia huyu mtoto huduma muhimu.
Mheshimiwa Spika, mwisho siyo kwa umuhimu, tunamfundisha dalili zote hatarishi ikiwemo kama kubadilika rangi mtoto, kuwa manjano, maana ini pia halijakomaa ikiwepo dalili ya mtoto kushindwa kupumua kwa sababu mapafu pia hayajakomaa na dalili yoyote ya hatari ambayo akiiona tu basi afike hospitalini haraka ili aweze kupata ushauri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili Mheshimiwa Mbunge alitaka kujua kama kuna utafiti wowote umefanyika. Zipo tafiti nyingi zimefanyika Kitaifa na Kimataifa, lakini pia Shirika la Afya Duniani, limefanya tafiti na kuona kwamba watoto wanaozaliwa njiti wanaongezeka kila mwaka na tafiti zimeonesha kwamba watoto hawa wanaongezeka kila mwaka kwa 10% mpaka 15% kwa watoto wanaozaliwa. Mfano, watoto wanaozaliwa Tanzania kwa mwaka ni kati ya watoto 1,900,000 mpaka 2,200,000. Kwa hiyo, tuna watoto 250,000 mpaka watoto 300,000 kwa mwaka ambao ni njiti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la (b) kwamba kama tumefanya tafiti, je tumetoa elimu? Serikali kupitia Wizara ya Afya, tumeendelea kutoa elimu kwa wamama wote wajawazito pale wanapofika kliniki. Maana matatizo yanayosababisha watoto kuzaliwa kabla ya wakati, yapo ambayo yanaweza kuzuilika ikiwemo maambukizi ambayo yanaweza kuleta homa kama vile Malaria, UTI, Pneumonia na mengine ikiwemo kiasi kidogo cha damu kwa mama mjamzito kinaweza kuleta kuzaliwa mtoto njiti, magonjwa sugu kama vile kisukari na shinikizo la damu kuwa juu.
Mheshimiwa Spika, hivyo ni visababishi ambavyo mama akifika mapema, basi tunampa elimu ili tumtibu vizuri ili asiweze kujifungua mtoto ambaye hajatimia. Vipo visababishi ambavyo huwezi kuvizuia kama vile kuwa na mimba ya watoto mapacha. Tunawashauri wamama wafike mapema ili tuwape uangalizi wa karibu ili kuzuia wasiweze kujifungua watoto njiti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved