Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Yagi Maulid Kiaratu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Singida Mjini

Primary Question

MHE. YAGI M. KIARATU aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa Chuo cha Maji katika Mkoa wa Singida?

Supplementary Question 1

MHE. YAGI M. KIARATU: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninapenda tu kumkumbusha kwamba chuo hicho cha Singida kimeanza muda mfupi uliopita kikiwa na wanafunzi 39, lakini hadi leo tunapoongea wapo wanafunzi 450, mwitikio ni mkubwa.

Mheshimiwa Spika, chuo kina ekari 41 kama alivyosema, lakini tayari wamefanya usanifu. Kinachosumbua sasa ni gharama kubwa za uendeshaji. Pale ukumbi wa Bonde wameshahama, wamepanga eneo ambalo wanalipa shilingi 150,000,000 kwa mwaka.

Myheshimiwa Spika, kutokana na ongezeko la wanafunzi, chuo pia kimeongeza program za mafunzo kutoka programu mbili hadi nane. Mpaka ikifika Oktoba mwaka huu chuo kinakusudia kupokea wanafunzi 1,500. Kwa maana hiyo, eneo lile walilopo sasa halitatosha, lakini pia gharama za uendeshaji zitaendelea kuwa kubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba commitment ya Serikali, chuo hicho ni kikubwa na bado wanafunzi wanapata shida kupata masomo hayo, na ukizingatia chuo hicho sasa kinatoa mafunzo yanayofundishwa na VETA, kwa hiyo, idadi ya wanafunzi itaendelea kuwa kubwa. Naomba majibu mazuri ya Serikali.

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na ninamshukuru sana Mheshimiwa Yagi kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya. Kikubwa zaidi, kwa muda mfupi kabisa ameelewa kazi kubwa inayofanywa na vyuo vyetu vya maji hususan katika hiki Chuo cha Maji Singida. Kiuhalisia, alichokiongea Mheshimiwa Mbunge ni ukweli kabisa kwamba tulianza na wanafunzi wachache, na sasa wanafunzi wamezidi kuongezeka. Hii maana yake ni kwamba, imani ya Watanzania katika chuo hiki imezidi kuwa kubwa na uhitaji wa majengo umekuwa mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Serikali kupitia Wizara ya Maji, tumeamua kuweka kwenye Mpango na kwenye bajeti ya mwaka 2026/2027 ili kuhakikisha sasa tunaanza ujenzi ili kuweza ku-accommodate wanafunzi ambao watakuwa wanadahiliwa katika chuo hiki ili kuepusha chuo kuingia kwenye gharama za kupanga majengo ambayo yatasababisha hasara, badala ya kujikita katika kuboresha huduma ya utoaji wa mafunzo.

Mheshimiwa Spika, Serikali tumepokea na ninakushukuru sana.