Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 9 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 93 2026-04-15

Name

Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza: -

Je, zipo sheria zinazolinda maeneo ya wazi na viwanja vya michezo kwenye majiji na miji nchini?

Name

Kaspar Kaspar Mmuya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba sasa nijibu swali Na. 93 la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalumu Tanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, upangaji na usimamizi wa matumizi ya ardhi unaongozwa na sera, sheria na kanuni mbalimbali za usimamizi wa maeneo ya wazi ambayo yanajumuisha maeneo ya viwanja vya michezo. Sera na sheria hizo ni pamoja na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Makazi ya Mwaka 2000, Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995 (Toleo la Mwaka 2023) na Sheria ya Mipango Miji, Sura ya 355 na Kanuni zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 4(3)(9) ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Makazi ya Mwaka 2,000 imeelekeza kulindwa kwa maeneo ya wazi kwa ajili ya matumizi ya umma. Aidha, Kanuni ya 6(3)(a) ya Kanuni za Mipango Miji iliyochapishwa katika Gazeti la Serikali Na. 91 la Mwaka 2018 inazuia kubadilisha matumizi ya maeneo ya wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika, Sheria ya Mipango Miji, Sura ya 355 kama ilivyorekebishwa mwaka 2023 ilizipatia Mamlaka za Upangaji jukumu la kupanga, kupima, kutunza na kusimamia maeneo ya wazi kwa kuzingatia mipaka yao ya kiutawala. Vilevile, Kanuni ya 4(7) ya Kanuni za Sheria ya Mipango Miji za Mwaka 2018 zilizotangazwa kupitia Gazeti la Serikali Na. 88 la Mwaka 2018 imetoa utaratibu wa udhibiti na usimamizi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, ninaomba kutoa rai kwa Mamlaka za Upangaji kuhakikisha maeneo ya wazi nchini yanatengwa, yanalindwa na kuendelezwa kwa kuzingatia sera, sheria na kanuni zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.