Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Yannick Ikayo Ndoinyo (3 total)

MHE. YANNICK I. NDOINYO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kabla sijauliza kwa kweli ninatoa shukrani nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutimiza ile ahadi yake ya kutujengea Barabara ya Gamba Gumu kutoka Ngorongoro kwenda kule mbugani Serengeti kwa kuwa ile barabara imeanza. Kwa kweli tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza kwa Wizara hii ya Mifugo, kama ambavyo tunatambua, viwanda ni nyenzo muhimu sana ya kuongeza thamani ya mifugo na kuongeza masoko na kipato cha wananchi wafugaji. Wilaya yangu ya Ngorongoro wananchi wakazi karibu 98%…

SPIKA: Mheshimiwa nenda kwenye swali moja kwa moja.

MHE. YANNICK I. NDOINYO: Mheshimiwa Spika, je, Wizara hii ina mpango gani wa kutujengea kiwanda cha nyama cha kusindika mazao ya mifugo ili kuongeza kipato kama vile inafanya kwa samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Serikali iko katika utaratibu wa kufanya mambo yafuatayo ili kuhakikisha tunaongeza uwekezaji wa viwanda vya nyama na kuongeza tija kwa wafugaji wetu. Kwanza ni kuendelea kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ili waweze kuwekeza katika sekta hii ambayo kwa kiasi kikubwa ina uwezo wa kuchangia katika pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, pili, tunaendelea kuwahamasisha wafugaji wetu ili kuendelea kufanya ufugaji wa kisasa kuongeza tija na ubora wa mifugo yao ili pindi tunapofanya uwekezaji huu, basi mazao haya tunayoyapata katika mifugo yetu yaweze kuwa na ubora mzuri ili kukidhi soko la ndani na nje katika nchi yetu. Ninakushukuru sana.
MHE. YANNICK I. NDOINYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Langu ni ombi na ushauri kwa Wizara kufanya utafiti wa uzalishaji wa zao la maziwa katika Wilaya yangu ya Ngorongoro ili kuwashauri na kuwasaidia wazalishaji wa maziwa wapate soko la uhakika na kuongeza kipato chao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ushauri na ombi kwa Wizara. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana, ninamshukuru sana Mbunge wa Ngorongoro, ushauri wake ni mzuri na tumeupokea kwa ajili ya kuufanyia kazi. Ahsante sana.
MHE. YANNICK I. NDOINYO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sekta hii ya ufugaji inaathirika sana na mabadiliko ya tabianchi, je, Serikali inaweza kuchukua hatua zipi za dharura kuwaandaa wafugaji kabla na wakati wa nyakati za ukame ili wasipoteze mifugo yao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, ni mikakati gani Wizara inaichukua kuwatembelea na kuwaandaa wadau pamoja na wafugaji kujiandaa na hiyo mikakati ya miaka mitano mnayoipanga kama Wizara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Ngorongoro, kwani tangu ameapishwa hapa mbele ya Bunge lako Tukufu amekuwa akifuatilia kwa ukaribu sana changamoto mbalimbali zinazowakumba wafugaji wake.

Mheshimiwa Spika, nikijielekeza katika kujibu maswali yake mawili ya nyongeza; moja linalohusika na hatua za dharura ambazo tunazichukua kuwaandaa wafugaji wetu. Kwanza kabisa ni kuendelea kutoa taarifa kupitia vyombo vyetu habari ambavyo vimekuwa vikitoa taarifa kila siku juu ya mabadiliko ya tabianchi na mipango ya hali ya hewa inavyoendelea.

Mheshimiwa Spika, lakini swali lake la pili, kulingana na mipango ambayo tunayo kwa wafugaji wetu kwa kipindi hiki cha miaka mitano, ni kweli, Serikali inatambua kwamba nchi yetu ya Tanzania kama zilivyo nchi nyingine, zimekuwa zikikumbwa na mabadiliko ya tabianchi ambayo yameleta ukame ambao kwa kiasi kikubwa umeathiri wafugaji wetu. Kwa kulitambua hilo, sisi kama Serikali, tumechukua hatua zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, moja, ni pamoja na miradi mikubwa ya ujenzi wa mabwawa tunayoendelea nayo katika sehemu mbalimbali nchi nzima. Pia tunatambua kwamba miradi hii inachukua muda na fedha nyingi, hivyo tumekuja na mipango ya dharura. Kwanza, kuanza kufanya tathmini kwa ajili ya kuanza kujenga visima virefu katika maeneo mbalimbali ya wafugaji wetu.

Mheshimiwa Spika, pili, tumeendelea kufanya mazungumzo na Wizara ya Kilimo ambayo kwa kiasi kikubwa inayo bajeti kubwa kupitia Tume yake ya Umwagiliaji ambayo inajenga mabwawa ya kumwagilia kwenye sekta ya kilimo sehemu mbalimbali nchi nzima ili kupitia mabwawa hayo, basi na wafugaji wetu waweze kutengenezewa majosho kwa ajili ya kunywesha mifugo yao.

Mheshimiwa Spika, pili, Wizara yetu kwa kutambua changamoto ya malisho tuliyonayo, tumeendelea kufanya tafiti mbalimbali kwa ajili ya kupata majani ya malisho ya wanyama wetu. Majani haya tumeyafanyia tafiti, ni majani ambayo yanalimwa kwa kiasi kidogo na kupata mavuno mengi ambayo yanaweza kulisha wanyama wetu kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, tatu, pamoja na kuendeleza mashamba yetu yaliyo katika sehemu mbalimbali nchi nzima ikiwepo Shamba letu la Vikuge lililopo Pwani, lakini Shamba letu la Lagwira lililopo Mbeya na taasisi zetu mbalimbali kama TARI na LITA zinazozalisha malisho.

Mheshimiwa Spika, pia, tumeendelea kuhamasisha sekta binafsi na wafugaji wetu kuendelea kulima malisho mbalimbali. Kupitia hili, Serikali yetu kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumeshatenga fedha, shilingi milioni 223 ambazo tutakwenda kuanzisha mashamba darasa ya malisho ya mifugo 300 nchi nzima katika halmashauri zote ili wafugaji wetu pale wanapohitaji mbegu, basi ziwafikie kwa ukaribu na kwa wepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, kwa maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuhakikisha wafugaji wetu wanapata malisho haya kwa wepesi alituelekeza sisi tupunguze bei ya malisho haya ambayo tulikuwa tunauza hapo awali kwa shilingi 4,000 kwa kilo na kwa sasa kwa maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Rais, wafugaji wetu watapata malisho haya (mbegu hizi za malisho) kwa shilingi 1,000 tu kwa kilo ili waweze kuyapata kwa wepesi.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa tunaendelea kuwahamasisha wafugaji wetu…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, ameshakuelewa ahsante.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante.