Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Benjamin Lukubha Ngayiwa (4 total)

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika mjadala wa kujadili hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa wakati wa kufungua ama kuzindua Bunge letu la Kumi na Tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakupongeza kwa kuteuliwa kwako kuwa Naibu Spika wetu. Pia ninampongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kwa nafasi hiyo ambayo anaitumikia. Nichukue fursa hii pia kuwashukuru wapigakura na wananchi wenzangu wa Jimbo la Kahama Mjini kwa imani yao kubwa waliyonipatia kwa kunichagua kuwa mwakilishi wao Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni siku njema ambayo tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Rais, lakini ni siku pia ya kumbukizi ya kuzaliwa kwake. Kwa hiyo, tunampongeza na kumwombea maisha marefu huko aliko, aendelee kututumikia Watanzania kwa moyo wote kama ambavyo ameonesha kwa kipindi chote.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii ya Mheshimiwa Rais ni hotuba ya kwanza kabisa aliyoitoa tangu tulipomaliza uchaguzi wetu mkuu tangu Oktoba, 2025. Hotuba hii iliakisi na kugusa maeneo karibu yote muhimu ya kisekta katika kuonesha Dira ya Maendeleo ya Taifa letu na kuinua hali ya uchumi kwa mwananchi mmoja mmoja katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashahidi, Mheshimiwa Rais alipogusia kwa mfano, katika sekta ya ujenzi aliposema na ninamnukuu hapa anasema; “Tutaongeza pia bajeti na uwezo wa TARURA katika kuboresha barabara za ndani na za vijijini ili kuhakikisha zinapitika mwaka mzima na kuwa wakulima wanaweza kuyafikia masoko kwa urahisi.”

Mheshimiwa Naibu Spika, humu Waheshimiwa Wabunge tulimpongeza kwa kumpigia makofi mengi sana, ikionesha kwamba shida kubwa au sehemu kubwa ambayo inatakiwa tuelekeze nguvu zetu ni katika kuboresha miundombinu yetu hasa barabara za ndani na zile za vijijini. Mheshimiwa Rais ameonyesha dhamira hiyo ya kuongeza bajeti kwa TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA hii ikiwa na umri wa miaka minane, kwa kweli imefanya kazi nzuri sana, lakini bado tunatakiwa kuendelea kufanya kazi iliyo bora zaidi na katika kuonesha kwamba tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais katika adhima yake ya kuboresha hali ya miundombinu yetu ambayo yeye anatamani ipitike kwa mwaka mzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi ninawaomba tu watendaji wetu katika ngazi zote kwamba Mheshimiwa Rais anapohangaika usiku na mchana kutafuta fedha kwa ajili ya maendeleo, basi na sisi tuoneshe ile nia thabiti na dhamira ya kwenda kumuunga mkono katika kusimamia shughuli hizi za maendeleo ili wananchi wetu waweze kufaidika na jitihada hizi za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijielekeza katika ukurasa wa 25 wa hotuba ya Mheshimwa katika sekta ya madini, pia Mheshimiwa Rais ameonyesha kutambua mchango wa sekta ya madini katika maendeleo ya Taifa letu. Katika hotuba yake inaonesha kwamba kiwango cha mchango wa sekta ya madini katika pato la Taifa, kiliongezeka kutoka asilimia 6.8 mwaka 2020 mpaka kufikia asilimia 10.1 mwaka 2024.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameonesha utayari wa kuwaunga mkono na kuwa-support wachimbaji wadogo kwa kuwawezesha kuwapatia vifaa vya uchimbaji kama vile vya uchorongaji, lakini na taarifa za jiolojia kuonesha kwamba madini yanapatikana wapi? Kwa wingi gani? Ni madini ya aina gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninaiomba tu pia Wizara yetu ya Madini iende ikasimamie vizuri eneo hili kwa kuhakikisha kwamba ile mikopo ambayo Serikali inaenda kuitoa kwa wachimbaji wadogo, iende basi kwa walengwa ambao kweli wana uhitaji, mikopo isiende kwa wachimbaji ambao tayari wana uwezo wa kujiendesha wao wenyewe na kuendesha shughuli zao za uchimbaji, na tuende tukawaangalie wale vijana ambao wapo katika hali za kati ambazo sasa wanataka kupambana kuweza kuona kwamba wanaongeza tija ya uzalishaji katika sekta hii ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba hata asubuhi wakati wa michango ya Waheshimiwa Wabunge walieleza kuhusu masuala ya mirabaha ambapo wachimbaji wanaonekana wanatozwa mirabaha mara mbili pale ambapo wanakuwa wameshatoa mawe juu, lakini pale ambapo wanakuwa wameshachenjua dhahabu na penyewe pia dhahabu inaenda kutozwa mrabaha tena kwa mara nyingine.

Mheshimiwa Niabu Spika, kwa hiyo, tuende tukaangalie maeneo haya ili wachimbaji wetu, sisi kule usikumani tunaita wasitegemee tu miganyalo. Miganyalo ni zile posho ndogo ndogo zinazopatikana kwa wachimbaji hawa wadogo wanapokuwa wanachimba katika maeneo yao hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa ambazo anazifanya na hotuba hii iende ikawe dira kwa taasisi zote za Serikali, taasisi binafsi, Wizara zote, tuweze kwenda kupita humu ambapo Mheshimiwa Rais wetu ameonesha dira kwamba sasa tunataka kuelekea upande gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili nichangie katika Mpango huu wa Taifa wa Maendeleo. Awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunijalia uhai na afya njema lakini pia niendelee kuwashukuru wananchi wema wa Jimbo la Kahama Mjini ambao walinichagua na kuniamini ili nije kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru pia familia yangu kwa maana ya mke wangu Happiness Kalugaba, lakini na Mama Gaudensia Ngayiwa na Mzee Ngayiwa Pascal Maziku na ndugu na jamaa wote wanaoendelea kunitia moyo katika kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Kahama Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijielekeze sasa katika kuchangia mapendekezo ya Mpango huu elekezi wa maendeleo wa muda mfupi, muda wa kati na mrefu. Niseme tu kwamba Mpango huu umetambua rasilimali zetu ambazo tupo nazo katika Nchi yetu tukufu ya Tanzania. Rasilimali hizo ni uoto wa asili; ardhi kubwa ambayo ina rutuba inayo support kilimo cha aina zote kwa maana ya mazao ya chakula na mazao ya biashara, lakini tuna water bodies ambayo ni mito; maziwa lakini na bahari ambayo yote haya yana support shughuli za uvuvi na kilimo lakini na matumizi mengine ya nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hoja yangu hapa, ninaamini Serikali yetu ambayo inaongozwa na Mheshimiwa mama yetu Rais mpendwa Mama Samia, ipo na nia thabiti na ya dhati katika kuwatumikia wananchi wetu. Kwa hiyo, hapa nishauri tu katika mikataba ambayo inajumuisha rasilimali zetu hizi nilizozitaja basi ipitie katika Bunge hili ili Wabunge tuweze kutoa ushauri wetu kwa sababu mikataba inayohusu rasilimali, inahusu pia kizazi chetu na dira hii ya maendeleo ya miaka 25, tunapoongelea mtoto wa miaka mitano, leo baada ya miaka 25 kufikia 2050 atakuwa ni mtoto mwenye miaka karibu 30. Sasa tunakuwa na Mpango huu wa maendeleo ambayo kwa kweli umelenga katika kuendeleza kizazi chetu ambacho kitakuja kunufaika na rasilimali hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mpango huu wa maendeleo umeweka vichocheo vya maendeleo ambavyo ni imetambua kuhusu nishati, logistics kwa maana ya uwekezaji katika miundombinu lakini sayansi na teknolojia, mageuzi ya kidijiti, mazingira ya biashara na uendelezaji wa uwekezaji katika kuboresha mifumo ya kisheria na kukuza ubia kati ya sekta za umma na sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa niseme tu kama wachangiaji waliotangulia kuchangia, idadi ya vijana kwa maana hawa ndiyo wabeba maono na watekelezaji wa huu Mpango wa Maendeleo wa Muda Mfupi, Muda wa Kati na Muda Mrefu. Hawa vijana kati ya umri wa miaka 15 na 35 ni zaidi ya 60% na hawa ndiyo nguvu kazi: kwa maana wale watoto na wazee ni tegemezi kwa nguvu kazi hii. Kwa hiyo, ni lazima tuangalie sera na mpango wetu katika kuwawezesha vijana wetu, waweze kuingia moja kwa moja katika kutumia hizi rasilimali nilizotaja hapa ikiwemo madini; ikiwemo rasilimali zetu za ardhi, lakini na maji ambayo tupo nayo katika mito, maziwa na bahari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Serikali kupitia Wizara na ninashukuru kwamba Wizara ya Vijana imeanzishwa, kwa hiyo tuweke sera ambazo zitaenda kuwawezesha vijana wetu kwa mitaji, lakini kuwawezesha vijana wetu kwa skills kwa maana ya teknolojia ili waweze kuhimili ushindani wa kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliposema kwamba tuboreshe miundombinu…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi Jimbo langu la Kahama Mjini…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Benjamin, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Nilitaka kumpa taarifa mchangiaji, anachangia vizuri kabisa kwenye kuishauri Serikali jinsi ya kuhakikisha kwamba vijana ambao ndiyo nguvu kazi wanawezeshwa kuhakikisha kwamba wote wanakuwa ni wazalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu za sasa hivi 87% ya population tuliyo nayo ni tegemezi, kwa maana watoto chini ya miaka 15 na wazee kuanzia miaka 65. Kwa hiyo, wazalishaji tu ni 13%, sasa Serikali ikichukua hizo takwimu ikazifanyia kazi kwa vile anavyosema mchangiaji pale ni hakika sasa hii percent ndogo ambao ndio wazalishaji ambao ndiyo wanabeba jukumu kubwa la kuwasaidia hao wengine ambao ni tegemezi itasaidia kukwamua hilo eneo ambalo linategemea sana 87%.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Benjamin, taarifa ya Mheshimiwa Matiko, unaipokea?
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea na ninaomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naongea hapa kuhusu uboreshaji wa miundombinu, lakini na mazingira ya kibiashara. Pale Jimboni kwangu Kahama ni jimbo zuri na lina watu ambao wanajituma sana katika kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali iwawezeshe wafanyabiashara pale ambao Mji wa Kahama ni kama lango la kuingia na kutokea katika nchi yetu ambayo inaunganisha Nchi zaidi ya nne; tunaunganisha Burundi, Rwanda, Kongo, Sudani na Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pale ningeomba sana wafanyabiashara wale wawezeshwe kwa mitaji, lakini na zile kodi, sipingi kwamba Serikali ikusanye kodi, lakini tuangalie namna ya kuwawezesha wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale pia kuna ujenzi wa ghala la biashara kwa maana ya kuweka kitovu cha kuuza mazao ya biashara na chakula nchi jirani. Ninaomba lile soko liweze kumaliziwa, lakini na miundombinu kama ambavyo Mheshimiwa Rais, alieleza katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge, kwamba ipitike muda wote wa mwaka mzima wa kiangazi na masika, basi twende kuiboresha ili wananchi wetu waweze kusafirisha mazao yao kutoka sehemu nyingine na kufanya biashara bila bugudha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, wawekezaji kupitia EPZ na SEZ wawezeshwe wapunguziwe masharti ili waje nchini waweze kuwekeza. Pale Kahama tuna kongani ya viwanda pale katika Mgodi wa Buzwagi. Wawekezaji wapunguziwe masharti waje wafungue viwanda, waweze kuzalisha ajira kwa vijana wetu na hapo Serikali inaweza ikaanza kukusanya kodi kwa maana ya kwamba zile raw materials wanazozitumia, lakini na huduma nyingine kwa maana ya service levy, watakuwa wameweza kulipia na wakati huo huo wakiwa wameajiri sehemu ya vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waache kucheza mabonaza vijana wetu, kwa sababu mabonaza haya kwanza ninapendekeza hata Serikali iangalie kuyatokomeza kabisa, yasiwepo katika nchi yetu ya Tanzania. Mabonaza haya yamekuwa tu mufilisi kwa vijana na wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi kuwa mchangiaji wa pili kwenye Hotuba hii nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri, tumemwona anazunguka katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu na kwa kweli, amesaidia sana kurudisha tabasamu kwa wananchi wetu. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawapongeza pia, Mawaziri wote waliowasilisha leo na Wenyeviti wote wa Kamati ambazo ziko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kipekee zaidi ninamshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwa mtulivu na focused kwenye ile mipango yake ya miaka mitano kuhakikisha kwamba, wananchi wetu wanaenda kupata maendeleo kama ambavyo tumeweza kujipangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kupita katika eneo la TARURA kwa udharura na umuhimu wake. Mheshimiwa Rais wakati anafungua Bunge letu alieleza kwamba, anaenda kuongeza bajeti. Tumesikia pia, katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, Serikali inaenda kuongeza bajeti, sasa ninaendelea kusisitiza na kuiomba Serikali kwamba, bajeti hizi zielekezwe upande wa TARURA, ili waweze kukidhi na kutekeleza ile miradi yote ya maendeleo ambayo ipo huko imekwama kwa muda mrefu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia, kutoa maoni hapo kama ambavyo tumeweza kujadili katika Kamati yetu ya TAMISEMI kwamba, tumeshuhudia kila mwaka wa fedha, Serikali imekuwa inatenga fedha, kwa ajili ya kukarabati na kutengeneza barabara hizo kila mwaka. Unakuta ndani ya miaka mitatu, miaka minne, barabara moja imetumia shilingi milioni mia wakati mwingine zaidi ya shilingi milioni mia moja, lakini mwaka unaofuata unakuta barabara hiyo bado ni mbovu na haipitiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukashauri kwamba, kama ambavyo tumekuwa tunatenga fedha za 10% za mikopo, halmashauri hizi zetu pia, zielekezwe kutenga kiasi cha fedha, kwa ajili ya kuhudumia hizi barabara, kuzijenga na kuzikarabati, ili ziwe imara na ziweze kupitika msimu mzima wa kiangazi na msimu wa mvua. Pia, hapa kama inawezekana itungwe sera, ili kuziwezesha hizi halmashauri zikope fedha, kwa ajili ya kuzipeleka katika hii sekta ya miundombinu; tutajikuta kwamba, tunapunguza gharama ya kutengeneza barabara hizi kila mwaka kwa kukopa hizo fedha, tunapata wakandarasi wanatengeneza hizi barabara kwa uimara kwa kuweka mifereji na barabara zetu zikawa nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifika pale Jimboni kwangu Kahama, Jimbo ni zuri sana, Mji wa Kahama ni mzuri sana, lakini changamoto ya barabara inaweza ikakufanya utamani kuondoka kesho yake kwa hiyo, hali iko hivi katika maeneo mengi. Pale Kahama tuna mtandao wa barabara karibu kilometa 923, hizi ziko chini ya TARURA, lakini lami tunayo kilometa 14 tu. Kuna halmashauri zingine zina kilomita saba, mbili kwa hiyo, kwa kweli, TARURA tuiongezee uwezo wa kuangalia uwezekano wa kuweza kuzifanya halmashauri zetu zikope, ziweze kuzielekeza katika maeneo haya au ziweze kutenga 10% nyingine, kwa ajili ya kuhudumia barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najielekeza pia, katika 10% ya mikopo kule kwenye Local Government. Kama alivyotangulia kusema mchangiaji aliyepita, Mheshimiwa Wambura Chege hapa, zile idara zetu za maendeleo ya jamii kwa kweli, inabidi waongeze uwezo na wapite kuelimisha vikundi hivi vya vijana, vikundi vya akinamama na watu wenye ulemavu, ili waweze kukopa na kuweza kurejesha ile mikopo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapitia taarifa kutoka mikoa mbalimbali tumeona tangu Juni, 2024 mpaka Februari, 2026 halmashauri imekopesha fedha nyingi sana, lakini vilevile fedha hizo nyingi hazijarejeshwa. Hii ni kwa sababu gani? Inaonyesha kwamba, ama vikundi hivi na watu hawa waliokopa hawajapata elimu nzuri ya kwenda kutumia hizi fedha ili warejeshe au ufuatiliaji wa madeni haya, ili waweze kukopesha tena hauendi vizuri. Sasa tulikuwa tunajiuliza, tutaendelea kutenga hizi fedha mpaka lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina nia njema ya kukopesha watu wetu, wananchi wetu wafanye biashara, waweze kuinua vipato vyao, lakini fedha zinazodaiwa ni nyingi sana. Pia, fedha nyingi zinazotengwa wakati mwingine unakuta hazikopeshwi, zinakaa benki wakati watu wetu kule wanalalamika; vikundi viko safi vinatimiza masharti, lakini havikopesheki, havikopeshwi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana hilo eneo twende tukaliboreshe, elimu itolewe na watu waweze kukopesheka. Wakati mwingine tukawa tunatamani hata wasikopeshwe fedha labda, wakopeshwe vitu vya kwenda kufanyia ile biashara; kama mtu anataka kwenda kufanya biashara ya kutotolesha mayai anunuliwe mashine ya kutotolesha mayai na aweze kuendelea kuliko kupewa fedha ambazo wakati mwingine anaishia kuzitumia katika matumizi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamalizia eneo la bakaa. Tumeona halmashauri nyingi zimekuwa zinavuka na bakaa nyingi sana na kisingizio chake wakati mwingine watu wanasema mtandao au huu mfumo wetu wa NeSTS. Kwa kweli, NeSTS pamoja na mazuri yake mengi na ninaunga mkono kwamba, hali ilivyokuwa hapo nyuma na kwa sasa tulivyo na huu Mfumo wa NeSTS unahitaji kuboreshwa tu, ni mfumo mzuri unaotakiwa kuboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaweza nikakwambia baada ya ziara yetu ya Kamati ya TAMISEMI tumeweza kushuhudia kwamba, mkandarasi mmoja anapewa miradi zaidi ya saba kwenye mkoa mmoja. Wakati mwingine kwenye nchi nzima ukifuatilia ana barabara kilometa tatu Geita, ana barabara kilometa saba Kahama, ana barabara kilometa nne Songea. Sasa ukiangalia katika kutengeneza barabara inahitaji mobilization ya mitambo, upeleke kule wataalam, upeleke capital, sasa unakuta wakati mwingine mashine hizi na mitambo inakuwa ni michache. Kwa hiyo, unakuta huyu mkandarasi anagusa kidogo Mradi wa Songea, anagusa kidogo Mradi wa Geita, anagusa kidogo Mradi wa Kahama na yote haikamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapendekeza pale kwenye NeSTS, ule mfumo uweze kuwekwa vizuri. Kwamba, uweze kuwezesha hii miradi midogomidogo ya kilometa mbili, kilometa tatu, wachukuliwe wakandarasi wa eneo husika waweze kufanya hiyo kazi kwa umahiri na kwa muda, ndani ya muda ambao unatarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi bakaa pia, tunaomba Serikali iweze kupeleka hizi fedha timely. Halmashauri nyingi zinapokea fedha baada ya nusu ya mwaka kupita, sasa wakianza kutangaza tender; kwa mfano, tuliona Mkoa wa Lindi kule unakuta mkandarasi ameomba tender, anaenda mpaka site, halafu akifika anaona ile kazi haimlipi ana-withdraw, halmashauri inaamua kutangaza upya, inatangaza mpaka mara tatu. Kwa hiyo, tuangalie pia, hii michakato ya ku-award tender tusiende tu kwa ku-award hawa wanao-tender, kwa wale low bidder wanaotenda kwa chini halafu na hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, huwezi kumpa mtu a-supply apple kwa shilingi mia mbili wakati linauzwa shilingi mia tano na wewe unampa huyo kazi, unajua kabisa atafeli. Kwa hiyo, tuangalie kabisa tathimini ifanyike vizuri hata mtu anayepewa hiyo tender tunajua kabisa anaenda kufanikisha hiyo kazi na kuifanya kwa umahiri mkubwa. Ninakushukuru sana na ninaomba niunge hoja mkono. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi kuwa mchangiaji wa pili kwenye Hotuba hii nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri, tumemwona anazunguka katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu na kwa kweli, amesaidia sana kurudisha tabasamu kwa wananchi wetu. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawapongeza pia, Mawaziri wote waliowasilisha leo na Wenyeviti wote wa Kamati ambazo ziko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kipekee zaidi ninamshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwa mtulivu na focused kwenye ile mipango yake ya miaka mitano kuhakikisha kwamba, wananchi wetu wanaenda kupata maendeleo kama ambavyo tumeweza kujipangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kupita katika eneo la TARURA kwa udharura na umuhimu wake. Mheshimiwa Rais wakati anafungua Bunge letu alieleza kwamba, anaenda kuongeza bajeti. Tumesikia pia, katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, Serikali inaenda kuongeza bajeti, sasa ninaendelea kusisitiza na kuiomba Serikali kwamba, bajeti hizi zielekezwe upande wa TARURA, ili waweze kukidhi na kutekeleza ile miradi yote ya maendeleo ambayo ipo huko imekwama kwa muda mrefu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia, kutoa maoni hapo kama ambavyo tumeweza kujadili katika Kamati yetu ya TAMISEMI kwamba, tumeshuhudia kila mwaka wa fedha, Serikali imekuwa inatenga fedha, kwa ajili ya kukarabati na kutengeneza barabara hizo kila mwaka. Unakuta ndani ya miaka mitatu, miaka minne, barabara moja imetumia shilingi milioni mia wakati mwingine zaidi ya shilingi milioni mia moja, lakini mwaka unaofuata unakuta barabara hiyo bado ni mbovu na haipitiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukashauri kwamba, kama ambavyo tumekuwa tunatenga fedha za 10% za mikopo, halmashauri hizi zetu pia, zielekezwe kutenga kiasi cha fedha, kwa ajili ya kuhudumia hizi barabara, kuzijenga na kuzikarabati, ili ziwe imara na ziweze kupitika msimu mzima wa kiangazi na msimu wa mvua. Pia, hapa kama inawezekana itungwe sera, ili kuziwezesha hizi halmashauri zikope fedha, kwa ajili ya kuzipeleka katika hii sekta ya miundombinu; tutajikuta kwamba, tunapunguza gharama ya kutengeneza barabara hizi kila mwaka kwa kukopa hizo fedha, tunapata wakandarasi wanatengeneza hizi barabara kwa uimara kwa kuweka mifereji na barabara zetu zikawa nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifika pale Jimboni kwangu Kahama, Jimbo ni zuri sana, Mji wa Kahama ni mzuri sana, lakini changamoto ya barabara inaweza ikakufanya utamani kuondoka kesho yake kwa hiyo, hali iko hivi katika maeneo mengi. Pale Kahama tuna mtandao wa barabara karibu kilometa 923, hizi ziko chini ya TARURA, lakini lami tunayo kilometa 14 tu. Kuna halmashauri zingine zina kilomita saba, mbili kwa hiyo, kwa kweli, TARURA tuiongezee uwezo wa kuangalia uwezekano wa kuweza kuzifanya halmashauri zetu zikope, ziweze kuzielekeza katika maeneo haya au ziweze kutenga 10% nyingine, kwa ajili ya kuhudumia barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najielekeza pia, katika 10% ya mikopo kule kwenye Local Government. Kama alivyotangulia kusema mchangiaji aliyepita, Mheshimiwa Wambura Chege hapa, zile idara zetu za maendeleo ya jamii kwa kweli, inabidi waongeze uwezo na wapite kuelimisha vikundi hivi vya vijana, vikundi vya akinamama na watu wenye ulemavu, ili waweze kukopa na kuweza kurejesha ile mikopo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapitia taarifa kutoka mikoa mbalimbali tumeona tangu Juni, 2024 mpaka Februari, 2026 halmashauri imekopesha fedha nyingi sana, lakini vilevile fedha hizo nyingi hazijarejeshwa. Hii ni kwa sababu gani? Inaonyesha kwamba, ama vikundi hivi na watu hawa waliokopa hawajapata elimu nzuri ya kwenda kutumia hizi fedha ili warejeshe au ufuatiliaji wa madeni haya, ili waweze kukopesha tena hauendi vizuri. Sasa tulikuwa tunajiuliza, tutaendelea kutenga hizi fedha mpaka lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina nia njema ya kukopesha watu wetu, wananchi wetu wafanye biashara, waweze kuinua vipato vyao, lakini fedha zinazodaiwa ni nyingi sana. Pia, fedha nyingi zinazotengwa wakati mwingine unakuta hazikopeshwi, zinakaa benki wakati watu wetu kule wanalalamika; vikundi viko safi vinatimiza masharti, lakini havikopesheki, havikopeshwi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana hilo eneo twende tukaliboreshe, elimu itolewe na watu waweze kukopesheka. Wakati mwingine tukawa tunatamani hata wasikopeshwe fedha labda, wakopeshwe vitu vya kwenda kufanyia ile biashara; kama mtu anataka kwenda kufanya biashara ya kutotolesha mayai anunuliwe mashine ya kutotolesha mayai na aweze kuendelea kuliko kupewa fedha ambazo wakati mwingine anaishia kuzitumia katika matumizi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamalizia eneo la bakaa. Tumeona halmashauri nyingi zimekuwa zinavuka na bakaa nyingi sana na kisingizio chake wakati mwingine watu wanasema mtandao au huu mfumo wetu wa NeSTS. Kwa kweli, NeSTS pamoja na mazuri yake mengi na ninaunga mkono kwamba, hali ilivyokuwa hapo nyuma na kwa sasa tulivyo na huu Mfumo wa NeSTS unahitaji kuboreshwa tu, ni mfumo mzuri unaotakiwa kuboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaweza nikakwambia baada ya ziara yetu ya Kamati ya TAMISEMI tumeweza kushuhudia kwamba, mkandarasi mmoja anapewa miradi zaidi ya saba kwenye mkoa mmoja. Wakati mwingine kwenye nchi nzima ukifuatilia ana barabara kilometa tatu Geita, ana barabara kilometa saba Kahama, ana barabara kilometa nne Songea. Sasa ukiangalia katika kutengeneza barabara inahitaji mobilization ya mitambo, upeleke kule wataalam, upeleke capital, sasa unakuta wakati mwingine mashine hizi na mitambo inakuwa ni michache. Kwa hiyo, unakuta huyu mkandarasi anagusa kidogo Mradi wa Songea, anagusa kidogo Mradi wa Geita, anagusa kidogo Mradi wa Kahama na yote haikamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapendekeza pale kwenye NeSTS, ule mfumo uweze kuwekwa vizuri. Kwamba, uweze kuwezesha hii miradi midogomidogo ya kilometa mbili, kilometa tatu, wachukuliwe wakandarasi wa eneo husika waweze kufanya hiyo kazi kwa umahiri na kwa muda, ndani ya muda ambao unatarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi bakaa pia, tunaomba Serikali iweze kupeleka hizi fedha timely. Halmashauri nyingi zinapokea fedha baada ya nusu ya mwaka kupita, sasa wakianza kutangaza tender; kwa mfano, tuliona Mkoa wa Lindi kule unakuta mkandarasi ameomba tender, anaenda mpaka site, halafu akifika anaona ile kazi haimlipi ana-withdraw, halmashauri inaamua kutangaza upya, inatangaza mpaka mara tatu. Kwa hiyo, tuangalie pia, hii michakato ya ku-award tender tusiende tu kwa ku-award hawa wanao-tender, kwa wale low bidder wanaotenda kwa chini halafu na hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, huwezi kumpa mtu a-supply apple kwa shilingi mia mbili wakati linauzwa shilingi mia tano na wewe unampa huyo kazi, unajua kabisa atafeli. Kwa hiyo, tuangalie kabisa tathimini ifanyike vizuri hata mtu anayepewa hiyo tender tunajua kabisa anaenda kufanikisha hiyo kazi na kuifanya kwa umahiri mkubwa. Ninakushukuru sana na ninaomba niunge hoja mkono. Ahsante sana. (Makofi)