MHE. AISHA M. MDUYAH aliuliza:-
Je, lini Serikali itaridhia na kuanza utekelezaji wa Itifaki ya Afrika kuhusu Haki za Watu Wenye Ulemavu (African Disability Protocol)?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, URATIBU NA WENYE ULEMAVU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kukamilisha taratibu muhimu kabla ya kuridhia na kuanza kutekeleza Itifaki ya Afrika kuhusu Haki za Watu wenye Ulemavu Barani Afrika (African Disability Protocol). Hadi sasa Serikali imeshafanya mapitio ya kisera na kisheria na tayari imeshakusanya maoni ya wadau kutoka kwenye vyama na mashirikisho ya watu wenye ulemavu kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, likiwemo Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) na Shirikisho la Jumuiya za Watu Wenye Ulemavu Zanzibar (SHIJUWAZA). Vilevile, maoni ya Serikali zote mbili yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar yamekusanywa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hatua hizo muhimu kukamilika, tayari rasimu ya itifaki imeshaandaliwa na wakati wowote kuanzia sasa itawasilishwa kwenye vikao vya maamuzi, kabla ya kuwasilishwa Bungeni kwa kuzingatia matakwa ya Ibara ya 63(3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 ambayo inalipa Bunge mamlaka ya kujadili na kuridhia mikataba yote inayohusu Jamhuri ya Muungano na ambayo kwa masharti yake inahitaji kuridhiwa. Ahsante. (Makofi)