MHE. SELINA H. KINGALAME aliuliza: -
Je, Serikali haioni haja ya kuanzisha Mfumo wa Elimu ya Vitendo (Internship) kwa kada nyingine za elimu, kama ilivyo Elimu ya Utabibu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, ninaomba nijibu swali la Mheshimiwa Selina Henry Kingalame, Mbunge wa Viti Maalumu, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa mafunzo kwa vitendo (internship) katika kuimarisha ubora wa wahitimu. Kwa sasa Serikali kupitia vyuo vya kati na vya elimu ya juu, imeweka utaratibu wa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi, ambapo uendeshaji wake hutofautiana kulingana na kada na mahitaji ya taaluma husika kwa kutumia mfumo wa field practical na industrial trainings.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Serikali inaendelea kuboresha miongozo ya mafunzo kwa vitendo, ili kuongeza tija na kuhakikisha yanaendana na mahitaji ya soko la ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, katika kada ya ualimu, Serikali imeandaa Kiunzi cha Kitaifa cha Mafunzo ya Ualimu kwa Vitendo (National Teachers’ Internship Framework) cha Mwaka 2026 ambacho kitatekelezwa kwa mtindo unaofanana na kada ya utabibu na kinatarajiwa kuanza katika mwaka wa masomo 2026/2027. Hivyo, Serikali itaendelea kuboresha mfumo wa utoaji mafunzo kwa vitendo kadiri itakavyoonekana inafaa.