Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Dr. Emanuel Qambaji Nuwas (1 total)

MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS aliuliza: -
Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha Mradi wa Maji wa Dambiya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia kuwepo katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, pili, kwa heshima kabisa na unyenyekevu nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kuniamini ili niweze kumsaidia kazi kama Naibu Waziri wa maji kwa kipindi hiki cha Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Emanuel Nuwas, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa maji wa Dambiya - Haydom uliopo Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara. Miongoni mwa kazi zinazotekelezwa kupitia mradi huo ni pamoja na ujenzi wa nyumba ya mashine, ulazaji wa mabomba umbali wa kilometa 373, ujenzi wa matanki matatu yenye jumla ya ujazo wa lita 2,575,000, ujenzi wa vituo 192 vya kuchotea maji vyenye dira za malipo ya kabla, sambamba na ujenzi wa mbauti nne za kunyweshea mifugo.

Mheshimiwa Spika, mradi wa Dambiya - Haydom umefikia wastani wa 45% za utekelezaji na unatarajiwa kumalizika mwezi Novemba, 2027. Mradi huo unatarajiwa kunufaisha zaidi ya wananchi 133,737 waishio katika vijiji 21 kwa wilaya ya Mbulu utakapokamilika. Serikali itahakikisha inapeleka fedha za utekelezaji wa mradi huo ili uweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.