Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili nipate fursa ya kuchangia kwenye Mpango wa Maendeleo wa Taifa letu. Jambo la kwanza, ninaomba nitumie fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha kuwa sehemu ya Bunge hili Tukufu, Bunge la Kumi na Tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nimshukuru sana Dkt. Samia chini ya uongozi wake ndani ya chama kwa kuona kuwa nami ninafaa kuwa sehemu ya kuwakilisha Wananyamagana kwa kipindi hiki cha miaka mitano. Mwisho na kwa umuhimu niwashukuru sana wananchi wakazi wa Jimbo la Nyamagana kwa namna ambavyo alinipa imani na hata wanavyoendelea kushirikiana na mimi. Kwa wanavyonitia moyo inanipa faraja ya kusonga mbele katika kuwatumikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo; Mpango wote huu ambao umewasilishwa kwetu na Wizara ya Mipango pamoja na Wizara ya Fedha; tunafahamu kuwa chini ya uongozi wa Wizara hii ya Profesa Mkumbo amefanya kazi nzuri sana; na katika hili ninampongeza. Wizara ya Fedha pia imejikita katika kutuandalia mambo ambayo kwa kweli kama yatatekelezwa basi tutegemee kuona uchumi wa Taifa letu unapaa kwa kiwango kikubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Wabunge mtakubaliana nami, kwamba mpango huu tunaouzungumza unahitaji fedha, ndipo tutapowagusa Watanzania, hususan kundi la vijana. Nimejaribu kupitia mpango huu takriban kila ukurasa kijana wa Kitanzania ameguswa. Ajira ambazo tunazungumza kwenda kuzitengeneza ni ajira kwa ajili ya vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa kuufanikisha mpango huu ni lazima tuwe na fedha. Katika hili ninaomba nishauri katika maeneo makubwa matatu. Kwa sababu ninatoka kwenye kanda ya ziwa kwenye Jimbo la Nyamagana, wananchi wa Jimbo la Nyamagana walinituma nije niseme hapa, niishauri Serikali. Kwa muda mrefu sana kwa nature ya Mkoa wetu wa Mwanza tunao uwanja wetu wa ndege, ambao kama ungeweza kukamilishwa kujengwa na kupewa hadhi ya kimataifa, ninataka niwahakikishie, Serikali yetu na Taifa letu litapata fedha nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiutazama uwanja wetu huu wa Mwanza, kutoka Mwanza kwenda Serengeti si zaidi ya kilometa 140 peke yake; lakini Uwanja wetu huu wa Ndege wa Mwanza ndiyo uwanja nambari moja unaoongoza kwa kusafirisha dhahabu kutoka kwenye Taifa letu. Uwanja huu unahudumia kanda ya ziwa yote. Hii inaonesha ni kwa namna gani kukamilishwa kupewa hadhi ya uwanja huu kuwa wa kimataifa uchumi wa Jiji letu la Mwanza na Taifa kwa ujumla utapaa kwa kiwango kikubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niishauri Serikali kwamba, mwaka juzi ilisaini mkataba kwa zaidi ya bilioni 29, lakini cha kusikitisha mkandarasi sasa kwa taarifa nilizonazo na kwa macho yangu tayari anaondoa vifaa site, maana yake hakuna matumaini. Wanamwanza wanauhitaji sana uwanja huu kwa ukuaji wa uchumi wao. Niwahakikishie uwanja huu ukikamilika na ukiwa wa kimataifa tunakwenda kutengeneza ajira nyingi sana kwa vijana wakazi wa Mkoa wa Mwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili uwanja huu tukiupa kipaumbele Taifa letu litakwenda kuongeza fedha za kigeni kutokana na watalii tutakaowapata. Kwa kuonesha msisitizo, wakati Serikali inatangaza mpango wa kuupa hadhi Uwanja wetu huu wa Kimataifa wa Mwanza wenzetu wa Shirika la NSSF walikuja kuweza. Tunayo hoteli pale eneo la Kapri Point ambapo Serikali ya Tanzania imelaza zaidi ya bilioni 90. Mtu pekee aliyekuwa amelengwa kulala kwenye hiyo hoteli ya zaidi ya bilioni 90 alikuwa ni mtalii, tukiamini kwamba uwanja ukikamilika watalii wengi watapita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo fedha ya Serikali zaidi ya bilioni 90 imelala pale na Wanamwanza hawayaoni matumaini ambayo wangetamani wayapate. Kwa hiyo, ninaomba nishauri Serikali iweke jitihada za haraka kwamba kwenye mpango huu wa mwaka mmoja wa miaka mitano na miaka ishirini na tano iliyosalia tuhakikishe kuwa jambo hili tunalibeba kama la dharura kwa sababu tutapata fedha ambazo zitakuza Uchumi na zaidi ya yote tutatengeneza ajira kwa vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu Shirika letu la Ndege la Air Tanzania. Mapato linayoyapata kwa mwaka zaidi ya 75% yanazalishwa na Kiwanja cha Ndege cha Mwanza. Ni namna gani Serikali inaweza ikaonesha commitment ya kwamba hata kwa namna ambavyo shirika letu la ndege; maana bila Mwanza nina hakika haliwezi kujiendesha; kwa sababu kama ni 75% tafsiri yake ni kwamba Air Tanzania ipo kwa ajili ya Mwanza kabla ya kuwaza kwingine kokote kwa sababu ndipo mapato hasa yanakotoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye sekta nyingine ya uvuvi. Mkoa wetu wa Mwanza na Jimbo la Nyamagana Mungu ametupa neema ya kipekee sana. Tunalo ziwa ambalo hawajapewa kwingine kokote kule. Ukiangalia ziwa hili kama Serikali hatujalitumia ipasavyo. Miaka ya 2000 wataalam wetu walikaa chini wakawaza wakaleta samaki aina ya sangara akaja akapandikizwa. Kulitokea mfumuko mkubwa sana wa ujenzi wa viwanda vya Samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunavyozungumza Mwanza tumebaki na viwanda saba peke yake. Kupitia viwanda vile tulitengeneza ajira, pia Serikali ilipata fedha na wananchi mmoja mmoja uchumi wao ulikuwa sana. Mimi ni shuhuda kwa sababu niko pale mjini. Wapo watu maarufu ambao wana majina ya samaki, samaki ambao walikuwa wanatoka ndani ya Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niiombe Serikali kwa msisitizo mkubwa sana. Serikali yetu kwa mipango ambayo nimeisoma kwenye mpango huu, kama ikiamua kwa dhati, ikaamua kutekeleza kama ambavyo imejielekeza basi Ziwa letu Victoria linaweza likawanufaisha Watanzania wengi na tukatengeneza ajira kwa vijana wetu walioko ndani ya Mkoa wa Mwanza na Jiji letu la Mwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili, ninataka niiombe Serikali, kwamba tuondokane na uvuvi huu wa kizamani. Uvuvi haramu unaofanyika kule ndiyo umesababisha kupotea viwanda zaidi ya 16 kwa sababu ya kukosa malighafi ya samaki. Serikali ni lazima ije na mpango mkakati wa kuhakikisha inawaza ni kwa namna gani tunakwenda kufanya transformation kwenye sekta ya uvuvi ili tutengeneze ajira tupate fedha za kigeni; na zaidi ya yote Taifa letu la Tanzania lipate fedha za kutosha, fedha ambazo zitatengeneza miradi mingi ya kimaendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipande kingine ambacho ningependa nichangie ni kuhusu barabara. Mpango huu uliowasilishwa na Profesa Kitila Mkumbo ni wa kisayansi sana, lakini…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa, muda umekwisha.
MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia; kwa sababu ya muda; Dkt. Samia Suluhu Hassan popote alipo atembee kifua mbele kwa sababu kazi nzuri ameifanya. Miradi inatekelezwa kule kwetu Mwanza, barabara zinajengwa. Katika yote, ninaomba nimhakikishie kwamba Wanamwanza wanamuunga mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja na ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kabla sijasema ninaomba nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia afya na uzima na hata tumekutana hapa tukiwa salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza ninachangia kwenye hoja hii na kusimama mbele ya Bunge hili, nitumie fursa hii sana kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Nyamagana kwa namna ambavyo wananipa ushirikiano na hivyo kuifanya kazi yangu ya Ubunge kuwa nyepesi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimeyasema hayo ninaomba sasa nami nichangie kwenye maeneo machache ambayo yameguswa kwenye hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitapita kidogo upande wa TAMISEMI. Kwa bahati njema nimekuwa Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI, nimepata fursa ya kuyachakata kwa upana masuala yanayowagusa Watanzania moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI Profesa Shemdoe. Kwa kipindi kifupi ambacho nimekaa naye Mheshimiwa Profesa ameonesha uhodari mkubwa sana. Sambamba na Profesa Shemdoe nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mwigulu. Kwa kipindi ambacho ameifanya kazi ya kupita kwenye mikoa mbalimbali amefanya kazi nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alipokuja kule kwetu Mwanza, Wanamwanza walimwona kama mtu wa tofauti sana kutokana na kazi njema alizokuja kuzifanya. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kipindi kifupi ameleta matumaini pale ambapo Watanzania walionesha kukata tamaa, ameleta nuru pale ambapo Watanzania waliona giza. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameleta matumaini na kuwaunganisha watu ndani ya kipindi kifupi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mantiki hiyo nikubaliane na wenzangu; ya kwamba kazi zote hizi zinazofanywa na wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI pamoja na Mheshimiwa Waziri, Mkuu ni kazi ambazo zinaakisi mipango na nia njema ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo imejielekeza kuleta maendeleo sawasawa na mapenzi ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Wizara hii ya TAMISEMI nimeisoma bajeti hii kwa mapana, lakini nimeiona ipo changamoto kubwa sana upande wa TARURA. Waheshimiwa Wabunge wenzangu watakubaliana na mimi; ninapochangia kwenye mpango huu wa bajeti tumekaa sana na Profesa Shemdoe, lipo jambo la dharura kwenye upande wa TARURA. Barabara nyingi kwenye majimbo yetu zimeharibika sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo yalitoka yakapelekwa kwa Mameneja wa TARURA, wameleta maombi ya dharura, Wizara imekwishafanya tathmini ambapo tayari imebaini kinahitajika kiasi cha zaidi ya bilioni 90 kwenda kukabiliana na changamoto ya dharura ya mafuriko na kuharibika kwa miundombinu ya barabara kwenye majimbo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kuishauri Serikali, kwa sababu kazi nzuri imekwishafanyika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ai-push Serikali iweze kutoa fedha ili tukaweze kupambana na kuondoa adha ya changamoto za barabara ambazo zimekatika katika majimbo yote. Hii haihitaji kuchukua muda mrefu sana kwa sababu fedha hizi ni kwa mpango wa dharura. Haitakuwa na maana kubwa sana fedha zimeombwa mwezi Machi wakati wa mahitaji halafu ziletwe mwezi Juni au Julai; dhana halisi ya dharura haitakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande huo huo wa TARURA ipo sheria moja ambayo pengine tuliipitisha kwenye Bunge hili hili ambayo inatufanya kurudi huko tulikotoka. Sheria hii ni kandamizi sana. Watendaji wa TARURA chini ya Waziri wa TAMISEMI wanafahamu. Ipo changamoto ya kuharibika kwa barabara. Unaweza ukakuta barabara imetoboka shimo kidogo tu, imeharibika sehemu ndogo sana, lakini kwa namna sheria hii ilivyo Meneja wa TARURA wa Wilaya ambaye si Meneja wa TARURA wa Mkoa hana mamlaka ya kuidhinisha fedha kwenda kufanya ukarabati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninajaribu kufanya analysis katika Jimbo langu la Nyamagana; kuna changamoto kubwa sana ya mashimo pale Liberty. Nilijaribu kuzungumza na meneja wangu wa TARURA akaniambia thamani ya fedha iliyokuwa inahitajika kuziba pale haivuki hata milioni tano; lakini kwa utaratibu ulivyo hata kama kingelikuwa ni kiraka cha shilingi milioni moja ni lazima aandikiwe Meneja wa Mkoa aletewe Waziri ije kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndani ya Bunge hili ili ipitishwe kwenda kuziba kiraka cha shilingi milioni moja; kitu ambacho hatuwatendei haki Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tukubaliane; maisha ya Watanzania wengi tunaowawakilisha kwenye majimbo yetu yanaguswa moja kwa moja kwenye suala la miundombinu ya barabara. Ninataka nikwambie, katika Jimbo langu la Nyamagana, mtandao wa barabara ni zaidi ya kilometa 1,225. Nilikuwa ninajaribu kufanya hesabu kidogo kwa haraka haraka, nikasema kama tutakwenda na utaratibu wa namna fedha zinavyokwenda kutengeneza hizi barabara itatuchuku zaidi ya miaka 150 Nyamagana kuenea lami kwenye mitaa yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini kifanyike; nimekwisha kushauri huko nje na hapa ninaomba nishauri. Jimbo la Nyamagana ambalo ndilo Jiji la Mwanza makusanyo yetu ya fedha za ndani ni zaidi ya bilioni 30. Nilikuwa ninataka kuishauri Serikali na kuiomba sana; sisi watu tunaotoka kwenye Majiji, tunaotoka kwenye Manispaa watupe vibali ili tuweze kukopa fedha tujenge barabara kwa wakati ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu kuondokana na changamoto hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni simple logic tu, dunia ya leo nikirejea maneno ya marehemu Mengi, aliwahi kusema wakati anazungumza na moja ya makongamano ya vijana. Alisema kuwa huwezi kuwa tajiri bila kukopa na ndiyo maana hata sisi mradi wetu wa reli tulilazimika kukopa na hatimaye tunayaona manufaa yake leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakitupa kibali sisi watu wa Mwanza wa Jimbo la Nyamagana tukaenda benki tukachukua fedha bilioni 50 au 60, kwa kuanzia, barabara ambazo tungezijenga kwa zaidi ya miaka 30, ninataka nikuhakikishie kuwa ndani ya kipindi cha miaka mitatu karibu robo ya barabara zote ndani ya Jimbo la Nyamagana zitakuwa zimejengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nje na hilo nigusie kidogo upande wa 4:4:2; kwa maana ya fedha ya 10% ya vijana, akina mama na watu wenye ulemavu. Tunafahamu kuwa huko nyuma fedha hizi zilikuwa zinatoka kwa utaratibu maalum; lakini hapo katikati zikasimama. Kwa dhamira ya dhati na upendo wa Mheshimiwa Dkt. Samia kwa Watanzania fedha hizi zimerejeshwa tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nikwambieni ukweli, kwamba malengo ya fedha hizi kwenda kuwahudumia wananchi wetu ili waweze kupata mikopo kwenye halmashauri zetu si sawa na vile ambavyo ilikusudiwa. Watanzania wengi wenye sifa hawapati hizi fedha; na mimi nimejaribu kufuatilia kwa research ndogo, takriban 75% – 80% ya waombaji hawapati hizi fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii yote ni kwa sababu ya ukiritimba. Lipo jambo moja ambalo wakati wa kupita pita lilikuwa linanisikitisha sana. Ukienda huko chini kwenye kila kata tuna Maafisa wa Maendeleo ya Jamii. Utaratibu wa kuzitoa fedha hizi unavyofanyika; wanaweka hayo matangazo, lakini hakuna taarifa inayopelekwa kwa wananchi kwenda kuwahamasisha na kuwapa elimu. Maafisa wetu wa Maendeleo ya Jamii wamebaki kuwa ni watu wa ofisini kusubiria kupokea maombi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhana halisi ya kuwatumikia Watanzania, jambo la kwanza wanapaswa watoke wawafuate wananchi walipo, wakaitishe mikutano, wawahamasishe wawaeleze masharti na namna gani wanaweza wakazipata hizi fedha ili ziweze kuwasaidia kuinua uchumi wa mmoja mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi letu la vijana linahangaika na ajira na hii ni ajenda ya nchi ama pengine ni ajenda ya dunia. Serikali haiwezi kuajiri watu wote. Namna pekee ya kuwasaidia vijana wapate ajira ilikuwa ni kupitia fedha hizi za 10% kwa vijana pamoja na watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niishauri sana Serikali, Profesa Shemdoe, waangalie namna mpya ya usimamizi wa hizi fedha, fedha hizi kwenye baadhi ya maeneo zinakwenda benki, zinakaa huko zaidi ya mwaka hazijawahi kuguswa wakati Watanzania wenye uhitaji wapo wengi. Kwa hiyo nitumie sana fursa hii kuiomba Wizara husika pamoja na Serikali, iangalie namna bora ambayo itaweza kuwasaidia Watanzania na hatimaye kijana wa Kitanzania, mama wa Kitanzania na watu wenye ulemavu waliopo ndani ya nchi yetu waweze kunufaika na mikopo hii ambayo Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuitoa kwenye Taifa letu…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.
MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapohitimisha nitumie fursa hii kumpongeza sana Dkt. Samia, amefanya kazi nzuri, nchi imetulia, wananchi wanafanya kazi zao kwa amani. Niwahakikishie tu wananchi ambao wanatusikiliza, sisi wawakilishi wao tupo macho kuifanya kazi iliyo njema ya kuishauri Serikali. Zaidi ya yote nina uhakika, kwamba matumaini aliyoyaahidi Mheshimiwa Dkt. Samia ifikapo 2030 yanakwenda kuonekana kwa vitendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)