Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Mhe. Dickson Nathan Lutevele (3 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. DICKSON N. LUTEVELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia Mpango huu wa 2026 - 2050. Kwanza kabisa ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wetu Profesa kwa kutusomea Mpango ambao kimsingi tuliuelewa umechanganua mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba nijikite kwenye eneo moja muhimu ambalo pengine linaweza likawa lina mchango mkubwa sana kwa Taifa letu kwenye Mpango huu ikiwa litafanyika kwa vitendo. Katika usomaji Mpango wa Mheshimiwa Waziri yapo maeneo ambayo yanawiana kabisa na Hotuba ya Mheshimiwa Rais. Eneo hilo mojawapo ni namna tutakavyoliendeleza Taifa letu kutoka kwenye uchumi tulionao hivi sasa kwenda kwenye uchumi wa kati na baadaye uchumi mkubwa zaidi. Katika kufanya hivyo tunajielekeza katika kujenga kongani za viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo ukisoma taarifa maeneo ya kongani za viwanda yameainishwa mle, lakini kwenye Mpango inasema tunafikiria kujenga katika kila wilaya. Sasa ninaomba nishauri kwamba mpango huu wa kongani za viwanda usiwe mpango wa maeneo fulani, halafu mawazo yakawa kwamba tunafikiria au tutafikiria kuweka katika kila wilaya. Kwa kuwa huu ni mpango ningeomba tujielekeze katika kuweka kongani za viwanda kwenye kila eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tuweke kwenye kila eneo? Hapa kwenye viwanda kuna eneo pana sana ambalo limeajiri watu ambao hata sasa wanafanya kazi kubwa na pengine hatujawafikia. Kwa mfano, katika nchi yetu hata sasa hivi ukitoka hapo nje unakuta kila baada ya mtaa kuna gereji vijana wanatengeneza magari, vijana wako wanafanya kazi za kuchonga (mafundi seremala) wamo humo, lakini hawa vijana hatujawakusanya sehemu moja na kwa kufanya hivi tunaathiri mambo makubwa mawili. Kwanza, miji yetu inakuwa haina mpangilio mzuri, lakini jambo la pili tunashindwa kukusanya mapato kwa sababu hawa vijana hatujawaweka sehemu moja na hatujawawekea Mpango mzuri unaotufanya turudi kuangalia maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wasiwasi wangu ni nini, ukisoma taarifa ya CAG kwenye Mpango wa BBT inaonesha kabisa kwamba mpango huu ulikuwa umelenga kuajiri vijana 9,724 ulianza na vijana hao, lakini mpaka 2024 kwenye taarifa ya CAG ya 2024 inasema vijana waliokuwa wamebakia walikuwa ni vijana 514 tu. Maana yake mpango huu umefeli. Kwenye conclusion anasema Wizara ya Kilimo na Wizara ya Umwagiliaji walifeli kwenye mpango huu. Pia, Mpango huu ulikuwa unasema tunakwenda mbele kwa miaka nane target yake, lakini ndani ya miaka miwili tayari inaonesha Mpango ulikuwa umefeli kwa sababu vijana 900 na, kwa mwaka mmoja wakashuka mpaka vijana 500 na, hawa vijana 400 na kitu wamekwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba mpango huu ulikuwa umefeli na sehemu gani ninaweza kusema ulifeli? Kwenye Mpango wa BBT yalikuwa yameainishwa maeneo ambayo mpango huo unatekelezwa. Wewe unamtoa kijana Mbinga unamleta atekeleze Mpango wa BBT Dodoma, hata mazingira tu yanakataa. Namna ya ufanyaji kazi wa watu wa huku na watu wa kule hayashabihiani, lakini tukiweka kongani za viwanda tutakuwa na faida zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, maeneo mengi katika nchi yetu watu watajiajiri. Leo hii tunajenga vyuo vya VETA katika kila wilaya lakini je, tumeshajiuliza hawa vijana tunaowajengea VETA, hawa watu wanaoingia VETA baada ya kutoka hapo watafanya kazi wapi? Tunasema kwamba mtu akisoma VETA atajiajiri. Kujiajiri siyo jambo la kufikirika ni jambo linalotaka mtaji. Kujiajiri siyo jambo la kuamka asubuhi ukasema ninajiajiri ni jambo linalotaka mwendelezo. Hivyo basi, ninaomba kushauri Wizara pamoja na taasisi zinazohusika kwenye haya mambo kwanza kabisa Mpango huu uwe ni wa kila wilaya ili tuwafikie watu wote kwenye nchi nzima? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, twende tukajifunze kwa Mataifa yaliyofanikiwa. Nilikuwa ninasoma taarifa ya namna wenzetu walivyofanikiwa, kwa mfano China, 12% ya pato la Taifa la China wanategemea viwanda vidogovidogo ambapo viwanda vidogovidogo vimeajiri takribani watu milioni 60. Idadi ya Watanzania wote imeajiriwa kwenye sekta moja tu Nchini China. Sasa twende maeneo hayo tujifunze. Twende India tujifunze kwa wenzetu waliofanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo mamlaka kwa mfano TanTrade; jana mchangiaji mmoja alisema tuwe tunafanya check and balance tukipanga mpango hata kama wa mwaka mmoja, jamani tuliwakabidhi hiki mmefika wapi? TanTrade atuambie kwa mwaka amepeleka vijana wangapi kupata exposure? Ukifuatilia unakuta wanaokwenda huwa ni wale wale, ni wale wale, ni wale wale, vijana walioko kijijini hawana exposure. Nguvu wanayo, uwezo wa kufanya kazi wanao, lakini kwa sababu tunakwenda taratibu hawana exposure. TanTrade chukua vijana 100 peleka China wakajifunze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa mfano, niliomba kwa TanTrade mara nyingi sana kwenda nikaangalie tu masuala ya machines, lakini nikakosa private sector ikanipeleka Dubai WoodShow. Wakati niko WoodShow nimekutana na masoko ya India, China na maeneo mengine niliporudi nimewapa Watanzania wenzangu masoko na wamefanya export. Kwa nini tusifanye haya? Kwa nini tusiwapeleke wale wanaolengwa na Serikali? Badala yake tunapeleka watu wale wale waliofanikiwa wenye viwanda vikubwa, tufikiri kuhusu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunafikiria Mpango wa Miaka 50 na kikubwa tunazungumzia viwanda. Tunapozungumzia hivyo viwanda, tuna viwanda ambavyo mpaka sasa vimeajiri watu wengi sana na havifanyi vizuri. Kwenye mpango havijaelezewa. Angalia Viwanda vya Chai kule Lupembe, angalia viwanda vya chai kule Mufindi. Angalia Viwanda vya Kahawa, kwenye Mpango huu tunasema tuna mpango gani wa kuhakikisha viwanda vile vinaendelea kufanya kazi. Kwa sababu katika viwanda vile wako babu zetu walitoa mashamba kwa ajili ya chai; walitoa mashamba kwa ajili ya kahawa; na walitoa mashamba kwa ajili ya Mikonge. Tunakuja na mpango gani wa kuhakikisha viwanda vile vinaendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninaomba sana sana nisisitize kwamba katika mpango huu twende kwanza field twende tukawaone vijana. Sasa hivi Serikali imejenga shule kila eneo, imejenga sekondari kila eneo na vijana wanafaulu, lakini wapo ambao hawafaulu kwa syllabus na wale vijana wakiingia kwenye ufundi kwenye magereji mafundi wa umeme mafundi wa magari wanafanya vizuri sana kwa sababu ubongo wao bado uko mbichi. Wale vijana kwenye Mpango huu tunawazungumziaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoangalia tutajikuta tunakwenda na Taifa la wasomi watupu, lakini kuna kundi kubwa nyuma tunaliacha na kundi hilo ndilo linalozalisha. Kwa hiyo, kwenye Mpango usijilengeshe pekee yake kwa waliosoma, tuangalie na wale wanaofeli kwa sababu ni Watanzania na wanashiriki kwenye kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DICKSON N. LUTEVELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza kabisa nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu; na nijielekeze moja kwa moja kwenye kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa heshima na taadhima niipongeze sana hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo kusema ukweli imesheheni mambo mengi sana. Tayari kwenye hotuba hii Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia, hasa wakipongeza sana kazi kubwa ambayo tayari viongozi wetu wanaendelea kuifanya. Sasa ninaomba nijikite kwenye maeneo matatu muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, ninaomba nimpongeze sana Rais wetu kwa kuendelea kuchapa kazi. Anachapa kazi kubwa na sisi tunaiona. Rais wetu ametuteulia Waziri Mkuu ambaye kwa kipindi hiki ndiye tuliyekuwa tunamtaka; Dkt. Lameck Mwigulu Nchemba, kwa sababu sote tumeona namna anavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo mengi ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu; sisi kwa ujumla hatuna mashaka na utendaji kazi wa Serikali yetu. Tumeona namna ambavyo Mawaziri wanafanya kazi usiku na mchana, wanafanya ziara wakienda maeneo yote katika idara zote kuhakikisha kwamba Watanzania tunaendelea kupata huduma kama ilivyo katika lengo la Serikali la kutupatia huduma. Tumemwona yeye mwenyewe Waziri wetu Mkuu akienda katika maeneo kadhaa na kutenda kazi kubwa sana katika kuibua na kujibu kero za Watanzania. Sasa, yako maeneo ambayo ninaomba nishauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tukirejea kwenye namna ambavyo tunaona kwenye maeneo yetu; viongozi wakubwa wanafanya kazi kubwa sana lakini wale wanao deliver zile huduma kule chini utendaji kazi wao kila Mheshimiwa Mbunge humu ndani anaulalamikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta Afisa wa Kilimo amepewa kishikwambi, amepewa pikipiki lakini akiondoka asubuhi ofisini kwa Mkurugenzi, akifika kule kijijini kuna sehemu maalumu ameweka, pale wanamjua, huwa anafika saa mbili na nusu, atakunywa supu, chakula cha mchana huwa anakula saa nane, hajaenda kule ambako Serikali imemuwezesha na imemnunulia vifaa kwa ajili ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mtindo huu hatuwezi kusubiri hadi Waziri Mkuu aje, au hadi Mkuu wa Mkoa ashuke kule chini. Tutafute namna ya kuwafanyia tathmini ya namna wanavyofanya kazi hawa wataalam wetu. Sisi kule kwetu yako maeneo ambayo wananchi wanahitaji ng’ombe watibiwe; lakini Mganga wa kutibu ng’ombe mpaka apigiwe simu na pengine atoe ratiba mwezi mzima hajakanyaga; ng’ombe wanakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe ushauri kwa Serikali. Kwa kuwa tuko kwenye mpango wa dira ya miaka hamsini, yawezekana Mheshimiwa Waziri Mkuu tuanze kuangalia; mfumo tunaoutumia wa ajira unamfanya mtu asiwajibike. Kumbe sasa, ikiwezekana tuweke mfumo kwenye dira yetu. Tuweke mfumo wa ajira ya mkataba. Mtu akifanya kazi miaka mitatu, amefanya vizuri, ataendelea. Hajafanya vizuri, wasomi wako wengi nje wanasubiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo huu tunaoutumia sasa hivi ulifaa sana wakati ambao wasomi ni wachache. Sasa hivi kila nyumba ina mtu anamiliki masters. Watu wafanye kazi kwa mikataba, wasisubiri kustaafu (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijielekeze katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ameeleza kwamba katika pato la Taifa sekta binafsi inachangia pato la Taifa kwa 70%. Sasa, ni lazima tuangalie kwamba 70% hii tunaiendeleza vipi? Ninaomba nitoe ushauri kwamba; katika kuziendeleza sekta binafsi, lazima tupunguze utitiri wa mamlaka zinazokwenda kwenye sekta binafsi. Tutengeneze one stop center. Kama ni tozo, mtu anatakiwa alipe laki moja na nusu, basi ijumulishwe alipe mara moja, siyo kila baada ya siku imekuja mamlaka hii, kila bada ya siku imekuja mamlaka hii. Hii hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kubwa. Ni kweli kwamba Mamlaka yetu ya Mapato, TRA, inapongezwa na imekuwa ikifanya vizuri sana. Kila baada ya msimu wanapotutangazia wanakuwa wamevuka lengo na wameenda asilimia kubwa sana. Ni lazima kama Serikali pia tuangalie, asilimia kubwa hii je, wale kule wanakokusanya kodi maendeleo yao yakoje? Isije ikawa inakusanywa sana kodi, halafu kule wananchi wanafilisika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa mfano, leo hii, wafanyabiashara pale Kariakoo lazima takwimu zipo, tutazame miaka 10 nyuma biashara ilikuwa inafanyikaje? Watanzania walikuwa wana import kontena ngapi? Leo hii pale Kariakoo tunaanza kuwashangilia mawinga, kumbe wale mawinga kwa asilimia kubwa ni biashara ya wafanyabiashara wageni, wafanyabiashara wenzetu wenyeji wamefunga biashara wameondoka kwa sababu mitaji yao imekufa. Kwa hiyo ninaomba Serikali, pamoja na ukusanyaji mzuri wa mapato, lazima tuhakikishe ng’ombe huyu anaendelea kupata majani na furaha, anaendelea kufurahi kukusanya kodi. Vinginevyo tutajikuta tunazidi kubomoa kile ambacho tumekijenga jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ninaomba nitoe ushauri. Kama ikimpendeza Waziri, ninashauri mamlaka zetu zipite kuangalia namna ambavyo wafanyabiashara wetu nchi nzima wanavyofanya biashara zao. Wachukue hata rekodi ya miaka mitatu nyuma, waangalie ili tunapokusanya kodi tukusanye kwa watu ambao wanafurahi kulipa kodi kwenye nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ningeomba na ningeshauri; Watanzania wanafurahishwa sana na kasi ya Serikali, wamefurahi, wanafurahi mno, lakini wana jambo moja ambalo wanaliomba, kwamba kazi kubwa zinafanyika matibabu, afya, barabara na kila kitu. Barabara zetu za vumbi zitengenezwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, Watanzania wanaomba mtaani kidogo shilingi iongezeke. Mtu akifanya biashara basi aone hela inapatikana kwa wingi mtaani. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Nilimwita Mheshimiwa...

MHE. DICKSON N. LUTEVELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja.
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda mrefu 2026/2027 - 2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/2027 – 2030/2031) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2026/2027 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali katika Muda wa Kati ya 2026/2027 - 2028/2029
MHE. DICKSON N. LUTEVELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia Mpango huu wa 2026 - 2050. Kwanza kabisa ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wetu Profesa kwa kutusomea Mpango ambao kimsingi tuliuelewa umechanganua mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba nijikite kwenye eneo moja muhimu ambalo pengine linaweza likawa lina mchango mkubwa sana kwa Taifa letu kwenye Mpango huu ikiwa litafanyika kwa vitendo. Katika usomaji Mpango wa Mheshimiwa Waziri yapo maeneo ambayo yanawiana kabisa na Hotuba ya Mheshimiwa Rais. Eneo hilo mojawapo ni namna tutakavyoliendeleza Taifa letu kutoka kwenye uchumi tulionao hivi sasa kwenda kwenye uchumi wa kati na baadaye uchumi mkubwa zaidi. Katika kufanya hivyo tunajielekeza katika kujenga kongani za viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo ukisoma taarifa maeneo ya kongani za viwanda yameainishwa mle, lakini kwenye Mpango inasema tunafikiria kujenga katika kila wilaya. Sasa ninaomba nishauri kwamba mpango huu wa kongani za viwanda usiwe mpango wa maeneo fulani, halafu mawazo yakawa kwamba tunafikiria au tutafikiria kuweka katika kila wilaya. Kwa kuwa huu ni mpango ningeomba tujielekeze katika kuweka kongani za viwanda kwenye kila eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tuweke kwenye kila eneo? Hapa kwenye viwanda kuna eneo pana sana ambalo limeajiri watu ambao hata sasa wanafanya kazi kubwa na pengine hatujawafikia. Kwa mfano, katika nchi yetu hata sasa hivi ukitoka hapo nje unakuta kila baada ya mtaa kuna gereji vijana wanatengeneza magari, vijana wako wanafanya kazi za kuchonga (mafundi seremala) wamo humo, lakini hawa vijana hatujawakusanya sehemu moja na kwa kufanya hivi tunaathiri mambo makubwa mawili. Kwanza, miji yetu inakuwa haina mpangilio mzuri, lakini jambo la pili tunashindwa kukusanya mapato kwa sababu hawa vijana hatujawaweka sehemu moja na hatujawawekea Mpango mzuri unaotufanya turudi kuangalia maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wasiwasi wangu ni nini, ukisoma taarifa ya CAG kwenye Mpango wa BBT inaonesha kabisa kwamba mpango huu ulikuwa umelenga kuajiri vijana 9,724 ulianza na vijana hao, lakini mpaka 2024 kwenye taarifa ya CAG ya 2024 inasema vijana waliokuwa wamebakia walikuwa ni vijana 514 tu. Maana yake mpango huu umefeli. Kwenye conclusion anasema Wizara ya Kilimo na Wizara ya Umwagiliaji walifeli kwenye mpango huu. Pia, Mpango huu ulikuwa unasema tunakwenda mbele kwa miaka nane target yake, lakini ndani ya miaka miwili tayari inaonesha Mpango ulikuwa umefeli kwa sababu vijana 900 na, kwa mwaka mmoja wakashuka mpaka vijana 500 na, hawa vijana 400 na kitu wamekwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba mpango huu ulikuwa umefeli na sehemu gani ninaweza kusema ulifeli? Kwenye Mpango wa BBT yalikuwa yameainishwa maeneo ambayo mpango huo unatekelezwa. Wewe unamtoa kijana Mbinga unamleta atekeleze Mpango wa BBT Dodoma, hata mazingira tu yanakataa. Namna ya ufanyaji kazi wa watu wa huku na watu wa kule hayashabihiani, lakini tukiweka kongani za viwanda tutakuwa na faida zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, maeneo mengi katika nchi yetu watu watajiajiri. Leo hii tunajenga vyuo vya VETA katika kila wilaya lakini je, tumeshajiuliza hawa vijana tunaowajengea VETA, hawa watu wanaoingia VETA baada ya kutoka hapo watafanya kazi wapi? Tunasema kwamba mtu akisoma VETA atajiajiri. Kujiajiri siyo jambo la kufikirika ni jambo linalotaka mtaji. Kujiajiri siyo jambo la kuamka asubuhi ukasema ninajiajiri ni jambo linalotaka mwendelezo. Hivyo basi, ninaomba kushauri Wizara pamoja na taasisi zinazohusika kwenye haya mambo kwanza kabisa Mpango huu uwe ni wa kila wilaya ili tuwafikie watu wote kwenye nchi nzima? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, twende tukajifunze kwa Mataifa yaliyofanikiwa. Nilikuwa ninasoma taarifa ya namna wenzetu walivyofanikiwa, kwa mfano China, 12% ya pato la Taifa la China wanategemea viwanda vidogovidogo ambapo viwanda vidogovidogo vimeajiri takribani watu milioni 60. Idadi ya Watanzania wote imeajiriwa kwenye sekta moja tu Nchini China. Sasa twende maeneo hayo tujifunze. Twende India tujifunze kwa wenzetu waliofanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo mamlaka kwa mfano TanTrade; jana mchangiaji mmoja alisema tuwe tunafanya check and balance tukipanga mpango hata kama wa mwaka mmoja, jamani tuliwakabidhi hiki mmefika wapi? TanTrade atuambie kwa mwaka amepeleka vijana wangapi kupata exposure? Ukifuatilia unakuta wanaokwenda huwa ni wale wale, ni wale wale, ni wale wale, vijana walioko kijijini hawana exposure. Nguvu wanayo, uwezo wa kufanya kazi wanao, lakini kwa sababu tunakwenda taratibu hawana exposure. TanTrade chukua vijana 100 peleka China wakajifunze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa mfano, niliomba kwa TanTrade mara nyingi sana kwenda nikaangalie tu masuala ya machines, lakini nikakosa private sector ikanipeleka Dubai WoodShow. Wakati niko WoodShow nimekutana na masoko ya India, China na maeneo mengine niliporudi nimewapa Watanzania wenzangu masoko na wamefanya export. Kwa nini tusifanye haya? Kwa nini tusiwapeleke wale wanaolengwa na Serikali? Badala yake tunapeleka watu wale wale waliofanikiwa wenye viwanda vikubwa, tufikiri kuhusu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunafikiria Mpango wa Miaka 50 na kikubwa tunazungumzia viwanda. Tunapozungumzia hivyo viwanda, tuna viwanda ambavyo mpaka sasa vimeajiri watu wengi sana na havifanyi vizuri. Kwenye mpango havijaelezewa. Angalia Viwanda vya Chai kule Lupembe, angalia viwanda vya chai kule Mufindi. Angalia Viwanda vya Kahawa, kwenye Mpango huu tunasema tuna mpango gani wa kuhakikisha viwanda vile vinaendelea kufanya kazi. Kwa sababu katika viwanda vile wako babu zetu walitoa mashamba kwa ajili ya chai; walitoa mashamba kwa ajili ya kahawa; na walitoa mashamba kwa ajili ya Mikonge. Tunakuja na mpango gani wa kuhakikisha viwanda vile vinaendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninaomba sana sana nisisitize kwamba katika mpango huu twende kwanza field twende tukawaone vijana. Sasa hivi Serikali imejenga shule kila eneo, imejenga sekondari kila eneo na vijana wanafaulu, lakini wapo ambao hawafaulu kwa syllabus na wale vijana wakiingia kwenye ufundi kwenye magereji mafundi wa umeme mafundi wa magari wanafanya vizuri sana kwa sababu ubongo wao bado uko mbichi. Wale vijana kwenye Mpango huu tunawazungumziaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoangalia tutajikuta tunakwenda na Taifa la wasomi watupu, lakini kuna kundi kubwa nyuma tunaliacha na kundi hilo ndilo linalozalisha. Kwa hiyo, kwenye Mpango usijilengeshe pekee yake kwa waliosoma, tuangalie na wale wanaofeli kwa sababu ni Watanzania na wanashiriki kwenye kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kushukuru sana. (Makofi)