Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Eng. Mshamu Ali Munde (1 total)

MHE. HARAN N. SANGA aliuliza: -

Je, lini wafanyakazi wa Tanzania watapunguziwa riba ya mikopo na kufikia asilimia saba au nane?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Haran Nyakisa Sanga, Mbunge wa Kigamboni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na sera za uchumi wa nchi yetu, riba za mikopo zinazotolewa na taasisi za fedha nchini kwa wateja mbalimbali, ikiwemo wafanyakazi huamuliwa na soko (market determined). Hivyo, Serikali inaona kuwa kuelekeza taasisi za fedha kuweka viwango vya riba vya asilimia saba au kiwango chochote mahususi au maalumu kwa ajili ya wafanyakazi itakuwa inakinzana na maelekezo ya sera za soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua kuwa swali hili lina msingi wa kwamba taasisi za fedha, maeneo pekee ambayo yanapata faida kwa kukopesha ni kwa watumishi ambao mishahara yao kukatwa ni rahisi. Hata hivyo, taasisi ya fedha inaweza kuweka kiwango cha riba kwenye mikopo ya wafanyakazi au mkopaji yeyote kufikia asilimia saba au pungufu ya hapo, kama itaona inafaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, wafanyakazi au mkopaji yeyote anaweza kukubaliana na taasisi ya fedha na kupata kiwango cha riba cha asilimia saba au pungufu kwa kadri itakavyowezekana. Vilevile, wafanyakazi kupitia waajiri wao wanayo fursa ya kuwasiliana na benki husika na kukubaliana riba wanayoweza kutoza wafanyakazi hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.