Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge, Zima ninashukuru sana kwa kuniona ili na mimi nitoe mchango wangu juu ya mipango iliyowasilishwa mbele ya Kamati yetu ya Bunge Zima. Ni lazima nikiri kwamba, leo ni moja ya kati ya siku za kipekee sana kwangu. Hii ni kwa sababu, zaidi ya mwongo mmoja uliopita, nikiwa nafanya kazi ya kujitolea katika Kigoda cha Mwalimu Nyerere juu ya umajumui wa Afrika. Yuko bwana mmoja aliniita katika moja ya migahawa ya Jiji la Dar es Salaam. Bwana huyo alinipa mawazo yake kwamba, kwa kadiri anavyonifahamu anadhani ninaweza kutoa mchango fulani kwenye jamii iwapo nitajiunga na siasa ya vyama vya siasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakiri kwamba, nilimkatalia kwa sababu zangu binafsi, lakini baadaye kutokana na bidii yake juu ya jambo hili, na tafakuri yangu ya binafsi, niliamua kumkubalia. Bwana huyo ndiye ambaye leo Wizara yake imeandaa mipango tutakayoijadili hapa sambamba na ile ya Wizara ya Fedha. Bwana huyo ni Mheshimiwa Prof. Kitila Alexander Mkumbo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasimama hapa kwa kujiamini sana kwamba, licha ya utofauti wetu wa kiitikadi Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo hatarajii hata kidogo kwamba, mimi nitasimama mbele ya Kamati hii nikajikita kumsifia peke yake. Ninafahamu kwamba, Mheshimiwa Prof. atafadhaika iwapo mimi nitajikita katika kuonesha changamoto bila kuonesha majawabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ndiyo siasa ninayoifahamu, hiyo ndiyo siasa ninayoitamani, na hiyo ndiyo siasa ninayoiota. Siasa ya kupingana kwa hoja bila kugombana, siasa ya kupishana bila kuumizana, siasa ambayo ninaamini siku moja isiyo ya mbali, siasa ya namna hiyo itakita mizizi tena katika duru za kisiasa za nchi yetu, ili kwa pamoja tuweze kutoa mchango wetu wa kuijenga nchi kwa upendo na mshikamano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa kwanza juu ya mipango yetu, kwa sababu, mawazo mengi yametolewa hapa na sitaki kurudia; la kwanza, ni mpango wowote ni lazima pia, utazame vihatarishi vya utekelezaji wa mpango ule. Mimi ninaona mpango haujatazama kwa kina vihatarishi vya Kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifuatilia siasa ya dunia hivi sasa mwenendo wa mambo katika siasa za Kimataifa unakuonesha kwamba, kuna mabadiliko ya kasi sana miongoni mwa Mataifa, hasa juu ya sera zao za mahusiano ya kimaendeleo na kudorora kwa nafasi na ushawishi wa majukwaa ya Kimataifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo linatutaka tuchukue tahadhari hasa katika kuhakikisha tunaweka vizuri masuala yetu ya ndani. Kama hatuweki vizuri masuala yetu ya ndani yatakayotufanya tuzalishe vizuri kwa utulivu, tukawa focused, tunaweza kujikuta tunapata changamoto katika financing ya mipango yetu na tukajikuta tunajikita katika kuwaumiza Watanzania kwa kuwabebesha mzigo mkubwa wa kodi ama kuingia katika mikopo ya kibiashara yenye masharti magumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninarudia rai yangu, tutengeneze nyumba yetu vizuri, tujenge mshikamano wa Kitaifa, tuweke mazingira mazuri ya kisheria, kikatiba na muafaka wa Kitaifa utakaotufanya mipango yetu ya uzalishaji. Kimakusanyo inabaki kama ambavyo tumeipanga, hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili. Mipango yetu inasema kwamba, sekta binafsi itakuwa ndiyo engine ya utekelezaji wa mipango ile. Kwenye financing ya mipango yetu inasema kwamba, 70% itakuwa kwa sekta binafsi na 30% kwa sekta ya umma. Ninaunga mkono rai iliyotolewa na Wabunge wengi kwamba, ni lazima tuendelee kuweka mazingira wezeshi yatakayoifanya sekta binafsi iweze kushamiri na itoe mchango wake katika uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi bado ninadhani hatuja-define na hatujaipambanua sekta binafsi tunayoitaka. Ni lazima tujiulize maswali magumu, sekta binafsi tunayoitaka sisi ni sekta gani? Je, ni sekta ya wachuuzi wa kigeni wanaopambana na wajasiriamali Kariakoo? Au ni sekta binafsi isiyozingatia utu, mazingira na maslahi mapana ya Tanzania?
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu, ni lazima tuiongoze sekta binafsi. Sekta binafsi isiyopangiliwa, sekta binafsi isiyoongozwa, haiwezi kuwa engine ya uchumi, itakuwa ni bomu linaloangamiza uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu, nimesoma Mipango hii, nimeangalia maeneo ya kielelezo, programu za kielelezo, ziko programu 14 na nikajaribu kuchambua. Nimeona katika kila programu tuna miradi ya kimkakati, kwa maana ya flagship projects. Tuna hatua kadhaa za kuchukuliwa na tuna Mipango mbalimbali. Hii maana yake ni kwamba tuna makumi na makumi ya masuala ya kuyafanyia kazi. Nimeangalia katika mpango wa muda wa kati, nimeona tuna miradi saba ya kielelezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu ni kwamba Tanzania haijawahi kuwa na uhaba wa mipango tangu tupate uhuru, kwa maana ya Tanganyika na Mapinduzi ya Zanzibar. Changamoto yetu kubwa ni utekelezaji wa mipango tunayojiwekea. Nina wasiwasi tukipata shock yoyote katika Mipango, baadhi ya Mipango hii itapewa kipaumbele na baadhi itawekwa kapuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima tuwe na Mpango fulani ambao tutauita, Mpango wa Kufa na Kupona. Kwamba, hata tukipata shida yoyote, kama Taifa, hili eneo ndiyo kipaumbele chetu namba moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siyo mchumi, lakini maoni yangu ninaomba Mradi wa Mchuchuma na Liganga ndiyo uwe wa kufa na kupona kwa sababu, Mchuchuma na Liganga ndiyo drive ya mapinduzi ya viwanda vya Tanzania kama tunataka kuhama kutoka katika maendeleo bandia ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunasema tuna maendeleo ya viwanda vya kuunganisha magari. Kwa maoni yangu, yale siyo maendeleo halisi ya viwanda, tena tusipokuwa makini unaweza kukuta ule ni uchochoro wa watu kuikosesha mapato Serikali. Yaani unakuta mtu vipuri vyote 100% anaagiza kutoka nje, anapata misamaha ya kodi, halafu akishaunganisha bila kujali ajira gani anazalisha sisi tunasema hayo ni mapinduzi ya viwanda. Mapinduzi ya kweli ya viwanda yataletwa na uzalishaji wa chuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mwenyezi Mungu ametupa chuma na makaa ya mawe hapo hapo, Mchuchuma na Liganga. Suala lisilosemwa sana ni palepale Mchuchuma na Liganga kuna madini ya kimkakati ya titanium na vanadium, ambayo yana thamani kubwa zaidi kuliko hata hicho chuma. Kwa hiyo, Mradi wa Mchuchuma na Liganga na Mradi wake shikizi wa Reli ya Kusini, kwa maana ya Reli ya Mtwara mpaka Bandari ya Mbamba Bay, ambao utakuwa na Tawi lake la Mchuchuma na Liganga uwe ndiyo mradi wa kufa na kupona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika neno langu la kuhitimisha, nimejipa homework ya kwamba, kila nikisimama nitakuwa ninakumbusha juu ya Katiba Mpya. Leo ninakumbusha tena kwamba, Katiba Mpya ndiyo funguo ya muafaka wa Kitaifa. Mchakato wake uanze mara moja, uwe wazi, ili wadau wote waweze kushiriki.
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana. (Makofi)