Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Juma Ramadhani Mustafa (1 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. JUMA M. KAWAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia Hotuba ya Waziri Mkuu yenye mwelekeo na mapitio ya kazi za Serikali kwa mwaka 2026/2027. Kwanza kabisa, ninaanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia afya njema na ametujalia Wabunge wote kufika hapa siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani zangu za kipekee nazipeleka kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri na maono yake mazuri anayoendelea kulitumikia Taifa hili. Hakika uzalendo wake hauna mfano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumpongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, kwa hotuba yake nzuri inayoakisi mwelekeo chanya kwa kazi nzuri za Serikali na ziara zake anazoendelea kuzifanya ndani ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ninaomba niwashukuru wananchi wa Jimbo la Igalula kwa heshima kubwa waliyonipa na kunichagua kuwa Mbunge wao wa Jimbo la Igalula. Ninaahidi hapa sitawaangusha, na sitakubali kuona Igalula haipigi hatua za kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie. Ninaanza kwenye sekta ya afya. Serikali imeendelea kuwekeza miradi mingi ndani ya sekta ya afya. Hotuba inaeleza miradi 113 inatekelezwa, miradi 45 inatekelezwa ndani ya hospitali za mikoa, na miradi 48 inatekelezwa ndani ya hospitali za halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi 5,000 wameajiriwa ndani ya siku 100 za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Serikali imewekeza kwenye vifaatiba na dawa kutoka 80% mwaka 2024 mpaka sasa 89% mwaka 2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo, bado kuna changamoto zifuatazo ndani ya Jimbo langu la Igalula. Upungufu na ukamilishaji wa vituo vya afya na zahanati, uhaba wa wataalamu wa afya, na umbali mrefu wa wananchi kufuata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Igalula, ninapenda kuishauri Serikali yafuatayo: kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya katika ngazi ya kata zenye upungufu ikiwemo Kata ya Igalula, Goweko, Kizengi, Loya, Tula na Lutende; na ujenzi wa vituo vipya katika kata ambazo hazijafikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kupeleka watumishi wa afya ngazi ya msingi kwenye kata, vijiji na vitongoji, kuboresha upatikanaji wa dawa hususan katika vituo vya afya na zahanati, na kupandisha kituo cha afya walau kimoja katika Jimbo la Igalula kuwa na hadhi ya hospitali ya wilaya ili kuweza kuepuka adha za akina mama na watoto kutembea umbali mrefu kufuatana na nature ya Wilaya ya Uyui jinsi ilivyo kimuundo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mapambano dhidi ya UKIMWI, Serikali imeendelea kuwekeza fedha nyingi kwenye mapambano dhidi ya UKIMWI. Takwimu zinaonesha kwamba watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI ni takribani milioni 1.7. Uelewa wa watu wa hali ya maambukizi juu ya UKIMWI umefikia 92%, matumizi ya dawa za ARV yamefikia 98.5%, ufanisi wa dawa umefikia 98.1%, na vituo vya kutibu magonjwa ya UKIMWI vimeongezeka kutoka 7,803 mpaka 82,005. Dawa za ARV zinatolewa bure kwa 100%. Serikali pia imekusanya fedha shilingi bilioni 26.8 kupitia Mfuko wa Hifadhi ya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya mafanikio, ninapendekeza yafuatayo kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Igalula. Serikali kuongeza utoaji elimu kwa vijana juu ya masuala ya UKIMWI, Serikali kutoa elimu kwa vijana juu ya masuala ya UKIMWI, kuimarisha ushirikiano na wadau wa sekta ya maendeleo, kuunganisha huduma za VVU na huduma za magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, presha, moyo na afya ya akili, na Serikali kuongeza kwa kasi kuendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukamilishaji wa Kiwanda cha kutengeneza ARV kilichopo Arusha - TPI ili kuendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa dawa za ARV ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali kuwapatia support (moral and material support) watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI wanaotengeneza vifaa mbalimbali ili kutambulika na TBS na bidhaa zao kupata soko kwa uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, magonjwa yasiyoambukiza. kama vile Kisukari, Shinikizo la Damu, Saratani, na Afya ya Akili yanaongezeka kwa kasi hapa nchini na kuwa tishio kubwa kwa afya za wananchi wetu. Jambo la kupongeza ni kwamba Serikali imeendelea kuwekeza katika huduma za kibingwa na ubingwa bobezi pamoja na kuwekeza kwenye vifaatiba na dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ninaiomba Serikali kutengeneza mkakati maalumu wa kitaifa wa kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza, kuanzisha uchunguzi wa mara kwa mara katika vituo vya afya, kutoa elimu ya lishe bora na mtindo wa maisha kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie sekta ya miundombinu. Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya miundombinu ya nishati na huduma za kijamii. Hadi kufikia Februari 26 vitongoji 39,003 sawa na 61% vimeunganishwa na umeme. Hii ni hatua kubwa, lakini bado maeneo mengi ya Jimbo la Igalula hayajafikiwa kikamilifu na huduma hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali kuhakikisha upanuzi wa umeme vijijini ikiwemo jimbo la Igalula, kuboresha barabara kupitia Wakala wa Barabara Mjini na Vijijini ikiwemo barabara ya Isuli – Miyenze, Misole – Miyenze – Nyahua, Malongwe – Mabeshi, Goweko – Kigwa, Miswaki – Loya, Goweko – Igalula Mpakani na Igalula – Kigwa. Kujenga madaraja maeneo korofi ikiwemo eneo la Loya, Vumilia Kata ya Igalula, Mbulumbulu Kata ya Mmale, Mdaki kata ya Kizengi na Tulieni, Kata ya Tula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vijana na ajira, Serikali imetoa shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwekeza kwa vijana kiuchumi. Aidha, zaidi ya vikundi takribani 12,977 vimepatiwa mikopo ya 10% na ajira zimeongezeka kwa 31.4%. Pamoja na mafanikio hayo ...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umemalizika.

MHE. JUMA M. KAWAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimalizie. Pamoja na mafanikio hayo ninapenda kushauri, kwa ujumla ninaipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanya katika kuwaletea wananchi maendeleo. Hata hivyo, utekelezaji wake unapaswa kulenga zaidi wananchi wa vijijini ili kuleta usawa wa maendeleo mijini na vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, ninaunga mkono hoja kwa 100%.