MHE. ENOCK Z. KOOLA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Mheshimiwa Rais kwenye sekta ya kilimo, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa Serikali ilitangaza mpango wa kuchimba visima virefu 500 nchi nzima kwa mwaka wa fedha 2025/2026. Je, Serikali inaweza kutoa taarifa kuhusu idadi ya visima vilivyopangwa kutekelezwa katika Jimbo la Vunjo ili kusaidia vijana na wanawake wanaoshughulika na kilimo cha mbogamboga?
Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa tayari Serikali imeanza kutekeleza ahadi ya kutoa miche mipya ya kahawa na tulishazindua hiyo ziara kwenye Jimbo letu la Vunjo kwa wakulima wa Jimbo la Vunjo, je, Serikali ina mkakati gani wa kufufua skimu ya mifereji ya asili, ukanda wa juu itakayowawezesha wakulima kumwagilia miche hii mipya ya kahawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nami ninampongeza Mheshimiwa Koola, Mbunge wa Vunjo kwa maswali yake ya msingi.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha ambao tunaendeleanao, na katika bajeti ya kilimo tulikuwa tumepanga kuchimba walau visima vitano katika kila Jimbo nchini kwa ajili ya miradi ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Wizara ya Kilimo tumesha-hire magari kwa ajili ya kufanya shughuli hiyo na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji pamoja na Wizara, kupitia miradi mbalimbali tuliyonayo pale, wanaendelea na shughuli hiyo.
Mheshimiwa Spika, namhakikishia tu kwamba tayari Wizara ya Kilimo tumeshapokea magari kwa ajili ya kufanya shughuli hiyo. Tume ya Taifa ya Umwagiliaji pamoja na Wizara kupitia miradi mbalimbali tuliyonayo pale, wanaendelea na shughuli hiyo.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kufufua skimu za asili kwa ajili ya kumwagilia kahawa, hilo ndilo jukumu letu. Tunaendelea kuzifufua zile za asili pamoja na kuzikarabati zilizopo ili kuhakikisha kuwa wananchi wa Vunjo na maeneo mengine nchini wananufaika na Wizara ya Kilimo ambayo ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Ahsante sana.