Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. MUSA G. MBUGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi hii uliyonipatia. Nianze kwa kumshukukru Mwenyezi Mungu, Muumba wa Mbingu na Nchi kwa kunipatia nafasi hii, lakini hata kwa kukubali niwe sehemu ya hili Bunge la Kumi na Tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Rais, na pia ninampongeza kwa kura nyingi alizopata. Ninamshukuru kwa sababu ya kuidhinisha kuteua jina langu, na baada ya hapo kuingia kwenye mchakato na Mungu akanisaidia nikashinda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninawapongeza pia Mheshimiwa Dkt. Ali Hassan Mwinyi; Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ninampongeza hata Spika pamoja na Naibu Spika kwa kupata ridhaa ya kuwa sehemu ya uongozi wa Bunge hili. Ninawapongeza pia Mawaziri mbalimbali hususan ni Mawaziri ambao wamewasilisha Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa. Vilevile, ninawapongeza Wabunge kwa ujumla kwa kuaminiwa na wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kwa kueleza yale ambayo nimejifunza baada ya kusoma huu Mpango. Wakati ninausoma nimeona kwa sehemu kubwa umejibu haja za wananchi wetu. Umejibu mategemeo na matarajio ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninaangalia jinsi ambavyo Mpango wa Maendeleo umeandaliwa, ni vipaumbele gani ambavyo vimezingatiwa? Nikiangalia vipaumbele ambavyo vimezingatiwa kwenye mpango huu wa maendeleo na malengo ambayo yamewekwa, ninaona moja, Mpango umeeleza kwamba lengo ni kuimarisha uchumi imara; pia, kuimarisha uchumi jumuishi na kuongeza ushindani katika uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati ninaangalia hivi vipaumbele vimeandaliwa kwa kuzingatia nini, napo Mpango ukawa umejibu kwamba vipaumbele vimeandaliwa kwa kuzingatia namna ambavyo tumetekeleza ule Mpango wa Tatu wa Miaka Mitano. Pia, umeandaliwa kwa kuzingatia mabadiliko ya uchumi na mabadiliko ya jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita zaidi kwenye sekta ya kilimo na kwenye sekta ya mifugo. Mpango wetu umeeleza namna ambavyo utatekelezwa na ukawa umeeleza pia risk ambazo zinaweza zikajitokeza na namna ambavyo zinaweza kuwa mitigated. Umeeleza sehemu ya tathmini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana waandaaji pamoja na Tume ya Mipango kwa sababu wameweka hata ile Tume ya Mipango ambayo imehusika kuandaa hii kuwa sehemu ya tathmini. Ingeweza tu kuandaa, halafu ikakaa pembeni, lakini kwa kuwa inakuwa ni sehemu ya kufanya tathmini ya kile ambacho tutaenda kutekeleza, inatupa matumaini kwamba tutaenda kukiishi kile ambacho tumekiandika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ile ya risk imenifurahisha zaidi kwa sababu kupanga ni kitu kimoja, lakini ikiwa hautabaini risk ambazo zinaweza kujitokeza njiani unaweza kuwa na mipango mingi na isitekelezeke. Ndiyo maana wengi tunaanzisha vitu, lakini havifiki mwisho. Kwa hiyo, mpango umejibu kila kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sehemu ya Kilimo ambayo ndiyo najikita, kwa sababu mimi wananchi wangu ni wakulima, lakini wananchi ambao wameniamini ni wafugaji. Mpango wa Maendeleo umeeleza kwa kuzingatia ile reference ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo, umeeleza mafanikio ambayo tumeyapata kupitia huo mpango. Zipo changamoto ambazo nimeziona kwenye huu Mpango, kwa mfano, Mpango kwenye kilimo umeeleza kwamba, tutaenda kuboresha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukifanya reference ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa ile miaka mitano, ukiangalia tumepiga hatua kwa kiasi gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetoka hekta 695,000 mpaka hekta 983,000 kwa maana kwamba, kuna ongezeko la hekta 288,000. Sasa ukiangalia hizi zimeongezeka kwa muda gani? Utaona ule ukuaji hauendani na malengo yetu. Ikiwa tulikuwa tumejiwekea tufikie angalau hekta 1,200,000, maana yake tumepiga hatua kama kwa 24% tu. Ukiangalia kwa muda uliobaki kukamilika kwa utekelezaji huu utaona speed yetu haiendani na kile ambacho tumejipangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati ninaangalia hili ongezeko la hizi hekta, ninaona pia, halijaenda kwa usawa. Kwa mfano, jimboni kwangu mimi hakuna bwawa hata moja la umwagiliaji wala hakuna kisima hata kimoja kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Maeneo ambayo wengine tunatoka ni maeneo ambayo ni nusu jangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri tunapoenda kwenye Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano, ni vizuri yawe yanazingatiwa maeneo kwa kufuata vipaumbele. Yale maeneo ambayo yana hali ya jangwa zaidi yapewe vipaumbele ukilinganisha na maeneo ambayo siyo ya jangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango umeeleza kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya chakula. Ukiangalia tumeongeza tani 5,655,000 ambapo hii rate na lengo ambalo tulikuwa tumejiwekea, ni speed nzuri, lakini haijaonesha hapa benchmark. Ukiangalia tumetoka tani 17,148,000 mpaka tani 22,000, maana yake ni ongezeko la tani 5,000,000, lakini mpango hauoneshi kuwa tulikuwa tumejipangia nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikawa ninapata wasiwasi inapofika wakati wa kufanya tathmini, tutafanya tathmini kwa rejea ipi ikiwa hatukuweka lengo? Kwa hiyo, yapo madhaifu ambayo nimeyaona. Nikawa ninashauri, ni vizuri sasa kila sehemu tuweke benchmark, tuweke lengo la kulifikia, ili unapokuja wakati wa kufanya tathmini, inakuwa ni rahisi kurejea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kwenye sehemu ya kilimo imeeleza mazao ya biashara jinsi ambavyo yameongezeka. Sasa mimi ninataka niongelee zao la pamba kwa sababu, kwetu pamba ndiyo dhahabu, kwetu pamba ndiyo Tanzanite.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mpango wa Tatu wa Maendeleo zao la pamba lilikuwa kwenye kilimo cha mkataba na kilimo cha mkataba kilikuwa kinalazimisha mnunuzi mmoja. Kimeleta madhara makubwa kwa wananchi wetu kwa sababu, mnunuzi mmoja inafika hatua anazidiwa na wakulima, analazimika kuwakopa na wakati mwingine wanalazimika kutoa rushwa, ili walipwe haki yao. Kwa hiyo, kilimo cha mkataba kwenye zao la pamba hakijafanya vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, japokuwa kwa sehemu kubwa tume-address ulimaji wa tija, lakini hatujaangalia kwenye upande wa bei. Hata kama Soko la Dunia likiwa limeshuka, kama tuna wanunuzi wengi maana yake ni panakuwa na ushindani wa bei. Kwa hiyo, ninashauri tunapoenda kwenye Mpango wa Nne, ni vizuri zao la pamba, ikiwa tutaendelea na kilimo cha mkataba, basi tuangalie namna ya kuwa na wanunuzi wengi, ili kuwa na ushindani kwenye bei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa mifugo, tumefanya vizuri, lakini ili tuongeze tija, ni lazima tuhakikishe tunajenga majosho kila sehemu. Ni lazima pia, tuongeze malisho.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana, muda wako...
MHE. MUSA G. MBUGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. MUSA G. MBUGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi ya kuchangia hotuba hii. Ninaanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyeniazima uhai na ninaendelea kumwomba aendelee kuniazima ninapotimiza majukumu ya Wana-Kisesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoelekea kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ninaanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu, kwanza kwa fedha nyingi ambazo amezileta kwetu Kisesa na kwa maendeleo makubwa. Muda hauwezi kutosha kuelezea moja baada ya lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza pia wasaidizi wake; Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt. Nchimbi, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wote. Ninawapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri kwa sababu, kwanza wamekuwa ni wasikivu, wanatupa muda wa kutusikiliza na wanatatua kero zetu. Kwa hiyo, Waheshimiwa Mawaziri tunawashukuru na tunawapongeza sana pamoja na Waheshimiwa Manaibu Waziri wote. Hotuba yetu au ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imeeleza utekelezaji wa 2025/2026 na imeeleza mwelekeo wa Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mambo machache ya kushauri kutoka kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ni hotuba ambayo imesheheni mahitaji ya Watanzania na ni hotuba, ambayo inajibu hoja na haja nyingi sana za Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwenye suala la uratibu wa maafa. Pamoja na mambo mengi mazuri ambayo yameelezwa kwenye hotuba, ninalo jambo la kushauri kwenye uratibu wa maafa ambayo kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ni Ukurasa wa 95. Tumekuwa tunapitia maafa mengi na hata Jimboni kwangu Kisesa baada ya mvua hizi nyingi kutokea na hatuwezi kumlaumu yeyote, hizi mvua zilizonyesha ni baraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi baraka zimekuja na changamoto, Malaika wa awamu hii nadhani alipoambiwa kwenda kufungulia maji akafungulia zaidi ya kiwango kwa hiyo, kwa Kisesa ikaleta shida kubwa; yapo maafa makubwa maeneo mbalimbali, kwa mfano Kijiji cha Nh’anga na sehemu zingine nyingi. Sasa zinapotokea changamoto kama hizi tunajua upo Mfuko wa Maafa ambao uko chini ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini hauna bajeti ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkuu wetu wa Mkoa, pamoja na DC; kwanza ninawashukuru na ninawapongeza, Mheshimiwa Namlingi Macha pamoja na dada yangu Fauzia Ngatumbura. Wamekuwa wanajituma sana kwenye mambo mengi, lakini changamoto ni linapokuja suala la maafa bajeti haitoshi. Kwa hiyo, hata mwananchi anapopata shida ni suala la kwenda kumpa pole, lakini pole inasaidiaje wakati mtu hana chakula? Pole inasaidiaje mtu hana pa kujihifadhi? Kwa hiyo, ninaishauri Serikali, ninaishauri Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, iongeze bajeti kwenye kipengele cha maafa, ili zinapotokea changamoto kama hizi iweze kuwa rahisi kukabiliana nazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ambayo ninataka nishauri ni suala la maendeleo ya vijana, ambayo kwenye hotuba iko ukurasa wa 84, maendeleo ya vijana; Serikali ya Awamu ya Sita imechukua hatua madhubuti kabisa ikaanzisha Wizara maalum ya Vijana na tumeona hatua mbalimbali ambazo zimetolewa ikiwa ni pamoja na hii mikopo ya shilingi bilioni 200, kwa ajili ya vijana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho ninataka niishauri Serikali ni hizi fedha, ukiangalia zimetawanywa kwenye Wizara mbalimbali, zipo zilizoenda Wizara ya Mifugo tumeona wametoa shilingi bilioni saba na kitu, zipo zilizoenda kwenye Wizara ya Uvuvi huko na Kilimo na sehemu mbalimbali. Ninashauri hizi fedha zingekuwa centralized sehemu moja, pawepo na one stop center, kama ambavyo REA wamefanya kwenye ule mradi wa kujenga petrol station vijijini fedha zote zimepelekwa Azania kwa hiyo, yeyote anayetaka kujenga petrol station vijijini anaenda REA, anapata maelekezo, ana-comply na EWURA, anakutana na fedha Azania, inaondoa milolongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri pia, kwenye suala la maendeleo ya vijana hizi fedha zinazotolewa, kwa ajili ya wanawake, kwa ajili ya vijana, ziwe sehemu moja ambapo mwananchi anapokwenda anakutana na huduma zote. Pamoja na kwamba Wizara ya Vijana haina technical team ya kutosha, wanaweza wakachukuliwa wataalam kutoka Wizara ya Mifugo, Wizara ya Kilimo na Wizara zingine wakapelekwa kwenye Wizara ya Vijana, ili kijana wa Kitanzania anapojkwenda kuomba mkopo akutane na huduma zote. Sehemu moja inaondoa mkanganyiko, inaondoa tafsiri mbalimbali kwa hiyo, ninashauri suala la hii mikopo ya shilingi bilioni 200 iwe sehemu moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ninaishauri Serikali ni kilimo. Serikali imefanya vizuri sana kwenye mambo mengi. Ninajikita kwenye kilimo cha pamba maana wananchi wangu wa Kisesa ni walimaji wakubwa wa pamba na kilimo, kwenye hotuba yetu, kiko page ya 24 na 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya juhudi kubwa kwenye zao la pamba ikaanzisha kilimo cha mkataba, contract farming, lengo ni kuleta tija kwenye kilimo, kwa maana ya Mfumo wa BBT. Changamoto ya huu mfumo inakuja inapofika kwenye suala la ununuzi; suala la kuwa na mnunuzi mmoja linaondoa ushindani. Ni kweli, bei ya pamba ni suala la global, it's a global price kwa hiyo, inakuwa determined na market force.
Mheshimiwa Mwenyekiti, panapokuwa na ushindani kwenye ununuzi hata bei inapokuwa imeshuka ni rahisi kwa mwananchi, ni rahisi kwa mkulima kuamini kuwa, bei imeshuka kuliko panapokuwa na mnunuzi mmoja. Kwa hiyo, ninaishauri Serikali, kwenye hiki kilimo cha mkataba waangalie component ya kuwa na wanunuzi wengi kuliko kata nzima kuwa na mnunuzi mmoja na ukiangalia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu… (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.
MHE. MUSA G. MBUGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana, ninamalizia. Ukiangalia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza jinsi ambavyo wananchi wamekuwa wanakopa fedha zao kwa hiyo, ikiwa wataboresha hii sehemu tutaondoa hayo yote. Muda ungetosha ningeeleza mambo ya Tembwa, lakini itoshe tu kusema ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)