Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Yagi Maulid Kiaratu (2 total)

MHE. YAGI M. KIARATU: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninapenda tu kumkumbusha kwamba chuo hicho cha Singida kimeanza muda mfupi uliopita kikiwa na wanafunzi 39, lakini hadi leo tunapoongea wapo wanafunzi 450, mwitikio ni mkubwa.

Mheshimiwa Spika, chuo kina ekari 41 kama alivyosema, lakini tayari wamefanya usanifu. Kinachosumbua sasa ni gharama kubwa za uendeshaji. Pale ukumbi wa Bonde wameshahama, wamepanga eneo ambalo wanalipa shilingi 150,000,000 kwa mwaka.

Myheshimiwa Spika, kutokana na ongezeko la wanafunzi, chuo pia kimeongeza program za mafunzo kutoka programu mbili hadi nane. Mpaka ikifika Oktoba mwaka huu chuo kinakusudia kupokea wanafunzi 1,500. Kwa maana hiyo, eneo lile walilopo sasa halitatosha, lakini pia gharama za uendeshaji zitaendelea kuwa kubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba commitment ya Serikali, chuo hicho ni kikubwa na bado wanafunzi wanapata shida kupata masomo hayo, na ukizingatia chuo hicho sasa kinatoa mafunzo yanayofundishwa na VETA, kwa hiyo, idadi ya wanafunzi itaendelea kuwa kubwa. Naomba majibu mazuri ya Serikali.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na ninamshukuru sana Mheshimiwa Yagi kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya. Kikubwa zaidi, kwa muda mfupi kabisa ameelewa kazi kubwa inayofanywa na vyuo vyetu vya maji hususan katika hiki Chuo cha Maji Singida. Kiuhalisia, alichokiongea Mheshimiwa Mbunge ni ukweli kabisa kwamba tulianza na wanafunzi wachache, na sasa wanafunzi wamezidi kuongezeka. Hii maana yake ni kwamba, imani ya Watanzania katika chuo hiki imezidi kuwa kubwa na uhitaji wa majengo umekuwa mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Serikali kupitia Wizara ya Maji, tumeamua kuweka kwenye Mpango na kwenye bajeti ya mwaka 2026/2027 ili kuhakikisha sasa tunaanza ujenzi ili kuweza ku-accommodate wanafunzi ambao watakuwa wanadahiliwa katika chuo hiki ili kuepusha chuo kuingia kwenye gharama za kupanga majengo ambayo yatasababisha hasara, badala ya kujikita katika kuboresha huduma ya utoaji wa mafunzo.

Mheshimiwa Spika, Serikali tumepokea na ninakushukuru sana.
MHE. YAGI M. KIARATU: Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Singida wana hamu sana ya kupata usafiri wa anga. Pamoja na kuchagiza shughuli za kiuchumi, usafiri na usafirishaji Singida ni katikati ya nchi. Singida ni jirani na Dodoma, ikitokea rubani akashindwa kutua Dodoma, mji wa karibu kutua ni Singida; lakini kwa sababu, Singida ni Katikati, itakuwa kiungo kizuri cha usafirishaji ndani ya nchi. Ninaomba kauli ya Serikali, ni lini sasa Singida watajengewa uwanja wa ndege? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Mbunge wa Singida Mjini na Mheshimiwa Mstahiki Meya Mstaafu kwa ufuatiliaji wake wa uwanja huu mzuri na muhimu kwa Taifa letu. Kama alivyoeleza yeye mwenyewe, uwanja huu ulijengwa miaka ya 1950 na Serikali imekuwa ikiutumia, lakini kwa kweli, kiwango chake kiko chini ni wa changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na maombi ya Waheshimiwa Wabunge na wakati mwingine viongozi, Serikali imepokea kilio hicho na imeanza kufanya usanifu. Ninamhakikishia, tunakwenda kujenga Uwanja wa Singida na mwaka wa fedha 2026/2027 tunaingiza kwenye bajeti. Tunaenda kuongeza runway kutoka 1,000 mpaka 2,000, tunaweka lami pamoja na kuhakikisha kwamba, tunaweka taa, ili uwanja utumike mchana na usiku.