MHE. YAGI M. KIARATU aliuliza: -
Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa Chuo cha Maji katika Mkoa wa Singida?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Yagi Maulid Kiaratu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mjini, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, Chuo cha Maji ni Wakala wa Serikali ulio chini ya Wizara ya Maji ulioanzishwa Mwaka 1974 kwa lengo la kuzalisha wataalam wa maji pamoja na sekta nyingine zikiwemo umwagiliaji na ujenzi. Pamoja na majukumu mengine, chuo hicho kinatoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi ya kozi zipatazo 25 kwa ngazi ya Stashahada, Shahada ya kwanza na Shahada ya Uzamili kupitia Kampasi zake za Dar es Salaam na Singida.
Mheshimiwa Spika, Makao Makuu ya Chuo cha Maji yapo Jijini Dar es Salaam na hutumia majengo yaliyopo Ubungo kwa ajili ya shughuli za kitaaluma. Upande wa Kampasi ya Singida, Chuo cha Maji kinatumia Majengo ya Bodi ya Maji ya Bonde la Kati Singida kutolea mafunzo.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, katika mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali imepanga kuanza kwa awamu ujenzi wa majengo ya chuo kwa Kampasi ya Singida katika eneo lenye ukubwa wa ekari 41.5 lililopo katika Mtaa wa Mwankoko Manispaa ya Singida ili kurahisisha na kuongeza ufanisi katika utoaji wa mafunzo.