Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Denis Lazaro Londo (4 total)

MHE. JOHN J. NCHIMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza baada ya kupata majibu haya mazuri. Swali la kwanza; Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami kwamba Mheshimiwa Rais anapokuwa ametoa ahadi na pia ahadi hiyo inapokuwa imewekwa katika Ilani ya chama ni ahadi ambayo inatakiwa itekelezwe na Serikali na siyo kuwasubiri Private Sectors ambao wanaweza wakaja muda wanaopenda wao na ikapita hata miaka mitano inayotarajiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je Serikali haioni umuhimu wa kukusanya wataalam wake waende kuwasaidia wananchi wa wilaya yangu kuwezeshwa kusaidiwa kupata mikopo ambayo ni ya riba nafuu kutoka maeneo ya Serikali kama Agricultural Bank, TIB na Benki ya Ushirika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimshukuru Mheshimiwa John John Nchimbi kwa maswali yake mawili ya nyongeza. Ni kweli ninaungana naye Mheshimiwa Rais anapotoa ahadi jukumu letu sisi kama Serikali ni utekelezaji wa ahadi hiyo. Kimsingi Serikali imeshaanza utekelezaji wa ahadi hiyo na ndiyo maana Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa imeshatoa miche 2,000,000 kwa wakulima wa kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo wameshanunua eneo kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda, uzalishaji wa kahawa Nyasa umeongezeka na ndiyo maana kuna umuhimu wa ujenzi wa kiwanda. Ukisoma Dira ya 2050 inazungumzia ushirikishwaji kwa maana tunazungumzia Uchumi Jumuishi na Sekta Binafsi ina mchango wa 70%. Ndiyo maana Serikali kupitia taasisi za fedha, kupitia wadau kama Vyama vya Ushirika tunaendelea kuhamasisha kuwekeza katika viwanda vya kati ili kushiriki kikamilifu katika dhana ya Uchumi Jumuishi kama nguzo ya Dira ya 2050 inavyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la uwezeshaji wa Serikali ninaungana na Mheshimiwa Mbunge. Ndiyo maana sisi kama Serikali tumeshatoa mwongozo kwa halmashauri kuona kwamba mazao ambayo yanatokana na maeneo husika tunaenda kuyajengea uwezo Vyama vya Ushirika. Pia kuomba fedha maalum kupitia bajeti ya Serikali kuona uwezeshaji wa ujenzi wa viwanda hivyo ili kuongeza mnyororo wa thamani, kuongeza thamani ya mazao, kupunguza gharama ya uzalishaji na kuchochea uzalishaji katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.
MHE. IBRAHIM M. SHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri, Moshi ni Mji ambao ulikuwa na viwanda vingi sana, lakini viwanda vile sasa hivi vimekufa na vimechukuliwa na wawekezaji na wale wawekezaji hawawekezi wamevichukua tu kama magofu. Ni lini Serikali itaweza kuwanyang’anya viwanda vile na kuvifanyia kazi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilivitoa viwanda hivi kwa wawekezaji kwa nia ya uzalishaji. Mkataba wa makabidhiano wa viwanda hivi kwa hao wawekezaji unawataka wauheshimu kwa maana ya kuendelea na shughuli za uzalishaji. Ndiyo maana kwa Moshi kuna Kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools ambacho mimi mwenyewe nilikuwa pale wiki mbili zilizopita kazi za uzalishaji inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo mengine ambayo wawekezaji wamepewa viwanda hivi na havizalishi, rai yetu ni moja tu kuwaambia kwamba, aidha warudi kwenye uzalishaji ama Serikali itachukua hatua ya kuwapatia viwanda hivyo wawekezaji ambao wana nia ya dhati ya kushiriki katika ujenzi wa Dira ya 2050 kwenye Uchumi wa Viwanda na Uzalishaji kwa ajili ya shughuli ya kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao yetu.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, kufuatia majibu ya Serikali, kwanza kabisa ningependa kusema wazi wawekezaji wengi hasa wale wakubwa wanapenda kuwekeza Mkoa wa Pwani, labda kwa sababu kupo karibu na Dar es Salaam. Huku pembezoni na kama ilivyo Mji wa Tarime, siyo rahisi sana kuweza kuvutia wawekezaji wakubwa kuja kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru Serikali imekiri kwamba kwa jiografia ya Mji wa Tarime, tuna upatikanaji mkubwa wa malighafi za kilimo, mifugo pamoja na madini. Pia, Mji wetu wa Tarime uko mpakani, na hivyo kuifanya Tarime Mji kuwa kituo kizuri tu cha kiwanda cha kuzalisha thamani.

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa kujua kwa kuwa hasa bidhaa za ujenzi ni ghali sana kwa kule kwetu Mkoa wa Mara, na asilimia kubwa inatoa Kenya, Serikali haioni kwamba ni wakati mwafaka kuhakikisha kwamba inavutia wawekezaji wakubwa wa vifaa vya ujenzi kama uzalishaji wa mabati, nondo, vifaa vya maji ili waje kuwekeza kule ili kupunguza watu kwenda Kenya au kupata bidhaa Tanzania kwa gharama kubwa zaidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa malighafi za kilimo zinapatikana, na pia tungependa kupata mwekezaji mkubwa ambaye anaweza kuchakata na kuwa na Kiwanda cha Biskuti kwa sababu tuna viazi vingi sana vinasafirishwa kuja huko mikoani au crips ambazo zinatokana na ndizi. Serikali haioni pia kuna haja sasa ya kumleta mwekezaji huyu mkubwa kuacha wale wadogo ambao umeeleza kwenye jibu lako la msingi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, kwanza nikiri maelezo ya Mheshimiwa Mbunge. Tarime ni Wilaya ya kimkakati na hasa tunapozungumzia Jumuiya ya Afrika Mashariki iko mpakani na iko kimkakati, na ndio maana mkakati ambao tunao sasa hivi ni kuimarisha biashara katika mtengamano huu wa Jumuiya ya Afrika Mashiriki na kutumia Tarime na mikoa ya mipakani kama maeneo ya kimkakati wa Tanzania ku-access masoko katika Jumuiya hiyo.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Serikali inatoa rai kwamba tunatangaza vivutio ambavyo ni vya kikodi na visivyo vya kikodi hususan kwenye miradi ya kimkakati ambayo inaweza kuwekezwa katika maeneo maalum ya kiuchumi na hii ikiwemo misamaha na nafuu ya kikodi ili kuhamasisha wawekezaji kwenda nje ya maeneo ambayo tumeyazoea hasa katika mikoa ya Pwani ili ku-access soko kubwa zaidi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwemo Tarime ambalo ni eneo la kimkakati ku-access masoko hayo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kuhusiana na suala la kutafuta wawekezaji wakubwa. Kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Dira ya 2020-2050, lengo letu ni kuongeza thamani ya mazao, thamani ya madini yetu ambayo tunazalisha nchini, viwanda vya kimkakati ambavyo vinatoa ajira na kutuhakikishia pia uwepo wetu katika Jumuiya na ku-access masoko ya SADC pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha.
MHE. DICKSON N. LUTEVELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wafanyakazi hawa wa Kiwanda cha SPM - Mgololo walishinda kesi ya msingi mwaka 2007 na katika kesi hiyo ya msingi Mahakama iliamuru wadai hawa walipwe kwa pande zote mbili, kwa maana ya mwekezaji kwa wale wafanyakazi wachache aliokuwa amewachukua, lakini na Serikali iwalipe wale wafanyakazi 760 ambao walikuwa hawajapewa barua ya kusitishiwa ajira yao na wala hawaendelei na kazi; kwa maana kwamba walikuwa wameachwa hewani. Mahakama ikaamuru kwamba walipwe tokea mwaka 2007.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; sasa je, Serikali haioni kama ipo haja ya kuumaliza huu mgogoro ili Watanzania hawa ambao walifanya kazi kubwa ya uzalishaji katika kiwanda kile, katika kujenga nchi yetu na wao wakapata haki yao ambayo wameitumikia kwa muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Rais wetu mpendwa kupitia Bunge hili alisema anatamani wakati anaondoka, angeacha tabasamu kwa Watanzania. Serikali haioni kama ipo haja ya kuumaliza huu mgogoro kwa kuona ni namna gani wanawafidia wafanyakazi wale ambao kwa kipindi kirefu sasa wanaisubiri hii fedha na kiwanda kile kilikuwa kikifanyiwa kazi na Watanzania kutoka nchi nzima na wanashindwa kuondoka Mgololo kwa sababu wamefanya kazi muda mrefu, hawana fedha na hawajapata mafao yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba majibu ya Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi na utu ndiyo kaulimbiu yetu na tabasamu la utu katika utumishi ni moja ya malengo ambayo tunayafanyia kazi chini ya maelekezo yake Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ni Rais wetu. Kwa muktadha huo, ninaomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Lutevele, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaingia hapa kwa sababu yenyewe ndiyo ilikuwa mmiliki wa kiwanda hiki kabla ya ubinafsishwaji wake. Kimsingi ninaomba nikiri kwamba madai haya chimbuko lake ni kupunguzwa kazi kwa baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda hiki na mwekezaji ameshalipa madai ambayo yanayomhusu kwa upande wake. Uhakiki ulifanyika kwa upande wa Serikali katika dhana ile ile ya kuacha tabasamu la utu na tayari Serikali ilifikia tamati kwa kupata kiwango cha fedha ambacho ni malipo stahiki kwa watumishi wa kiwanda hicho. Serikali ilitoa fedha hizo katika mwaka 2017 na 2018. Hata hivyo, wafanyakazi hao walikataa kuchukua kiasi hicho kwa madai kwamba ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa, Serikali imeshtakiwa na suala hili bado liko Mahakamani na kinachogombewa hapa ni kwamba, kiwango ambacho kimetoka ni kidogo, lakini nia ya Serikali ni kumaliza mgogoro huo ili wananchi hawa wapate haki yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.