MHE. CLAYTON R. CHIPANDO aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kushughulikia wakandarasi wanaochelewesha miradi kama Mradi wa Delta ya Mto Luiche unaoendelea kwa kasi ndogo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya kutokukamilika kwa wakati kwa baadhi ya miradi ya maendeleo ikiwemo mradi wa umwagiliaji wa Delta ya Mto Luiche. Mradi wa Luiche wenye jumla ya thamani ya shilingi bilioni 65.16 unajumuisha ujenzi wa bwawa na miundombinu ya mashambani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, mwaka 2025 ilifanya mapitio ya usanifu wa mradi husika ili kuendana na mahitaji ya sasa na hivyo kuongeza muda wa utekelezaji wa mradi hadi mwaka 2027. Baada ya mapitio hayo, mradi umeanza utekelezaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa mradi wa Delta ya Mto Luiche kutanufaisha eneo la umwagiliaji lenye ukubwa wa hekta 3,000 na kunufaisha wakulima zaidi ya 9,620 katika Vijiji vya Kagera, Matiazo, Mungonya, Kamala, Kasuku na Simbo.