Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Sheila Edward Lukuba (2 total)


MHE. SHEILA E. LUKUBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majawabu mazuri ya Serikali, nina majibu madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kihonda na Lukobe hazikuwahi kupata mafuriko huko nyuma, lakini baada ya ujenzi mkubwa wa Reli ya Kisasa ya SGR kumeibuka makorongo makubwa yaliyopo Kwa Wagogo, Juhudi, Azimio. Makorongo haya kwa ujumla yamekuwa yakisababisha mafuriko makubwa na kuathiri mali na miundombinu ya wananchi. Je, lini Serikali itajenga miundombinu imara ili kudhibiti mafuriko na ili kunusuru maisha ya wananchi hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Mkoa wa Morogoro ni wanufaika wakubwa wa Mradi wa SGR na sisi sote ni mashahidi tumekuwa tukitumia, lakini kuna changamoto ya vivuko katika Kata ya Lukobe Mtaa wa Tushikamane, karibu na Shule ya Sekondari Mji Mpya na Mtaa wa Kambi Tano ambao ni mpaka wa Mvomero na Morogoro Mjini. Nini kauli ya Serikali juu ya vivuko hivyo? Kwa sababu imekuwa ahadi ya muda mrefu kwamba wananchi hawa watatengenezewa, nini kauli ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza ninampongeza sana Mheshimiwa Sheila Edward Lukuba, Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Morogoro, amekuwa mfuatiliaji wa karibu sana wa shughuli za ustawi wa wananchi wa Mkoa wa Morogoro lakini na Watanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninamhakikishia tu Mheshimiwa Mbunge Lukuba kwamba, kwanza Serikali inatambua kwamba tuna changamoto ya mafuriko katika mitaa ya wananchi katika Kata ya Lukobe na Kihonda Morogoro Manispaa, na tayari tumeshatuma wataalamu. Timu ya wataalamu inafanya tathmini maeneo gani yanahitaji miundombinu ya aina gani na gharama za fedha zinazohitajika, ili baada ya kukamilisha tathmini ya mahitaji na design tutapeleka fedha kwa ajili ya kujenga mfereji wa kupeleka maji yale ya mafuriko kwenye Mto Ngerengere ili kuondoa mafuriko hayo. Kwa hiyo, ninakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kihonda na Lukobe kwamba, Serikali inalifanyia kazi na tutakwenda kumaliza changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la pili, tunafahamu kwamba viko vivuko ambavyo vinahitaji kujengwa, na kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema, kivuko cha eneo la Tushikamane lakini pia kivuko cha Mtaa wa Kambi Tano. Ninaomba nimhakikishie tu kwamba, wakati wa ujenzi wa mfereji huo tutapeleka package ambayo pia itakwenda kujenga madaraja lakini pia kujenga vivuko hivyo ili kuondoa changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.
MHE. SHEILA E. LUKUBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha na kutangaza geti la Msolwa - Kilombero kuelekea Hifadhi ya Nyerere ili kukuza zaidi utalii?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimthibitishie tu Mheshimiwa Sheila kwamba, geti la Msolwa ni moja ya geti ama ninaweza nikasema ni kanda maalum kwa ajili ya Kanda ya Solwa kuelekea Hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii imepanga kuandaa siku maalum kwa ajili ya uzinduzi wa geti hilo jipya la Msolwa ili iwe kama sehemu ya kimkakati ama promotion ya kutangaza sekta ya utalii pamoja na uwekezaji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuko katika hatua za mwisho, na hivi karibuni Mheshimiwa Mbunge atapata hiyo taarifa na ataona Wizara ikitekeleza.