MHE. MARYAM USSI YAHYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali la nyongeza. Pamoja na kwamba kuna uvamizi wa ardhi, lakini bado tuna migogoro mingi ya ardhi hapa nchini. Je, Serikali sasa haioni ni muda muafaka wa kuanzisha mfumo maalum kama vile ilivyo Samia Legal Aid, sasa uanzishwe mfumo maalum wa kusikiliza changamoto ya migogoro ya ardhi ili kuweza kutatulika kwa haraka?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Mariam kwa swali zuri na nia yake njema ya kuwafanya wananchi wetu waishi bila migogoro kwenye maeneo yao wanayoishi na kufanya shughuli za kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niwapongeze sana Mamlaka ya Serikari za Mitaa hususan Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya mpaka Wakurugenzi waliopo katika halmashauri zetu, wamejiwekea utaratibu wa kusikiliza kero za wananchi, na kila wiki wamepanga siku moja au siku mbili mahususi kusikiliza na kupokea kero za ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tu nitoe rai yangu kwa Watanzania wote kwanza, nimesema Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa sababu tunao Maasifa wa Ardhi waliomo kwenye maeneo hayo ambao nao ni sehemu ya timu ambayo Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa wanatumia katika kusikiliza changamoto hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Wizara ya Ardhi imejitanabahisha kabisa, tutaweza kutatua changamoto hizi kwa mfumo niliyoeleza, huu wa kusema vijiji vyote vipimwe. Licha ya hivyo, tuna utaratibu wa kuwa na kliniki maalum ya kusikiliza zile kero ambazo zimeshindikana katika ngazi ya wilaya au ngazi ya mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi wenyewe ni mashahidi, tumetoka juzi tu hapa kufanya kliniki ya wiki moja Tanzania nzima, hii ambayo tuliita jina kubwa kabisa, Samia Ardhi Kliniki, tuliweza kusikiliza wananchi wengi na tuliweza kutatua changamoto nyingi na tukawapatia wengine hati za umiliki wa maeneo ambayo wameomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Wabunge wakiwa sehemu ya wananchi ambao wanawatumikia, tuungane na Serikali hususan Wizara yetu ya Ardhi kuweza kuwasikiliza wananchi katika mikutano yetu tunayokwenda kuongea nao na kutatua matatizo. Kwa kuwa matatizo mengine ni ya kiutawala, lakini yale mengine sisi kama Wizara ya Ardhi, tuko tayari kusaidiana kwenye mikutano au ziara ambazo tutaziweka.