Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Haji Kombo Mdowe (1 total)

MHE. MDOWE HAJI KOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa ruhusa yako. Kwanza ninaomba niishukuru na kuipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kazi kubwa ambayo inaendelea kuifanya katika nchi yetu. Pia ninashukuru kwa majibu yao ambayo wamenipa, kwa sababu majibu haya yametoa mwongozo mzuri katika suala letu hili. Hata hivyo, ninayo maswali mawili ya nyongeza katika jambo hili: -

(a) Je, ni vigezo gani vya kiulinzi, kiutawala na kimiundombinu vinavyotakiwa kukamilika ili kituo cha Polisi kiweze kupandishwa hadhi?

(b) Je, ni jukumu la nani hasa kukamilisha vigezo vya kiulinzi na kimiundombinu katika vituo vya Polisi nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mdowe Haji Kombo, Mbunge wa Jimbo la Nungwi kwa maswali yake mawili ya nyongeza, ambayo ni muhimu sana. Ninapenda kumfahamisha Mheshimiwa Mdowe kwamba, vigezo vya kimiundombinu ni madaraja ya majengo ya Jeshi la Polisi ambayo yapo kwenye daraja la C1, C, B na E, kutegemeana na aina au eneo linalotaka kujengwa kituo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ombi ambalo wamewasilisha wao kwa Kituo cha Polisi cha Nungwi, kwa sasa kipo kwenye daraja C. Kwa hiyo, kinaomba kupandishwa hadhi kwenda kwenye daraja B. Ili kufikia kiwango cha daraja B, basi ni lazima miundombinu hiyo ya jengo la kituo cha Polisi iwe imekidhi vigezo vya daraja B la vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika vigezo vya kiulinzi ni kuangalia parameter za eneo ambalo linaombewa kupandishwa daraja la eneo hilo. Kwa mfano, hivi sasa Jeshi la Polisi linayo maeneo ambayo yamepewa hadhi ya mikoa, lakini kiutawala yapo hadhi ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano halisi ni kwa Mkoa wa Dar es Salaam ambao umepewa kanda maalum, na ndani yake zile wilaya zimepewa hadhi ya mikoa. Hiyo inatokana na hali ya kiutawala, na pia mahitaji ya kiulinzi katika eneo la Mkoa husika wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa vigezo hivyo, watakapowasilisha maombi yao kupitia Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, kwa maana ya Kamati ya Usalama ya Wilaya, itaweza kuchakata na kutathmini hali ya vigezo vyote vitatu kama vitakuwa vimefikiwa na kushauri ipasavyo kwenye ngazi inayofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili kwamba, ni nani ambaye ana jukumu hilo, nilieleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, ninauomba uongozi wa Jimbo la Nungwi kwamba uwasilishe pendekezo hilo kwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, kwa maana ya Kamati ya Usalama ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.