MHE. ALI VUAI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninapokea ushauri, pia nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, Serikali ina mpango gani wa kuwapeleka askari wa doria katika eneo hilo ambalo liko mbali na kituo cha Polisi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, yuko tayari kutembelea Kijiji hicho kwenda kuona matatizo halisi ya umuhimu wa ujenzi wa kituo cha Polisi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Khamis kwa kufuatilia kwa karibu hali ya ulinzi na usalama katika Ukanda wa Mkwajuni hasa katika eneo la Matemwe, eneo ambalo ni ukanda wa utalii na lina ongezeko kubwa la idadi ya watu kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ninaomba kujibu hoja zake mbili. La kwanza, tuna mpango gani wa doria, kwa ukanda wote wa kuanzia Matemwe, Pwani Mchangani, Kiwengwa hadi Nungwi. Kwa sasa Jeshi letu la Polisi linaendelea na doria kwa sababu eneo lote hilo ni la kimkakati kwa ajili ya uwekezaji wa utalii, na kila siku Jeshi la Polisi kupitia Kituo Kikuu kilichopo Mkokotoni wanaendelea kufanya doria na Kituo Kidogo kilichopo Kiwengwa katika ukanda wote wa Pwani ambao amezungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa pili wa ombi lake la kutembelea hilo na kuona umuhimu wa kujenga kituo katika eneo hilo, napenda kukubaliana naye kimsingi kwamba eneo la ukanda wa Matemwe ni eneo la utalii, na kwa sababu ni eneo la utalii, kasi kubwa ya uwekezaji pamoja na ujio wa watalii na wageni mbalimbali kutembelea maeneo hayo, kunaakisi hoja aliyoileta ya kuweza kujengwa kituo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ninaomba nimjibu tu Mheshimiwa kwamba niko tayari kutembelea eneo hilo. Pili, tunaona umuhimu wa kujenga kituo cha Polisi katika eneo hilo.