Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Johnston Johansen Mutasingwa (2 total)

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. JOHNSTON J. MUTASINGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyetujalia afya njema na tunaendelea na michango yetu sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niwashukuru sana Wananchi wa Jimbo la Bukoba Mjini kwa kunichagua kuwa Mbunge wa Jimbo la Bukoba Mjini na kwa heshima kubwa sana niwashukuru kwa kumchagua Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee ninapenda kuchangia katika hotuba ya Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nimesoma kitabu kuanzia ukurasa wa kwanza mpaka ukurasa wa 40. Nimeitafakari sana Hotuba ya Mheshimiwa Rais, ni hotuba ambayo inatoa maono na mwanga kwa Mheshimiwa Rais anataka nini na anataka nchi iendeje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika haya na katika Jimbo letu la Bukoba Mjini, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametenda mambo makubwa sana na ninaweza nikasema ni muujiza ambaye hajawahi kutokea katika jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ametuletea shilingi bilioni 9.016 katika barabara za TARURA ni jambo ambalo halijawahi kutokea katika jimbo letu la Bukoba Mjini na sasa anakwenda kuongeza pesa katika barabara za TARURA. Sasa anapokwenda kuongeza pesa katika barabara za TARURA niwaombe, TARURA sasa zile kilometa 133.87 ambazo wilaya yangu ya TARURA pale Bukoba Mjini imeziomba ili iweze kuzihudumia, niombe sasa waende kuziangalia ili mwananchi anayeishi Bukoba ziweze kumsaidia na kupandisha uchumi wake na hii ndiyo sera ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Barabara inayotoka Kahororo kwenda Makongo hadi Ntoro. Hii Barabara inakwenda kwenye eneo ambalo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema anakwenda kukuza sekta binafsi. Kule kuna watu ambao wanachimba kokoto wanapiga mawe na inaenda ziwani. Niombe sasa tuweze kuiangalia ili iweze kutengenezwa, ina urefu wa kilometa 4.73.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametuleta miradi mikubwa na ya kimkakati katika jimbo letu ambayo ina thamani ya shilingi bilioni 40.04 katika Miradi ya TACTIC. Tunakwenda na tunajenga soko kubwa la Bukoba Mjini pale. Tunajenga Stendi yetu ya Kyakairabwa na tunajenga barabara kilometa 10, lakini tunakwenda kuweka taa 412. Hili ni jambo la kihistoria ambalo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amelifanya katika Jimbo letu la Bukoba Mjini ninasema mama ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la miundombinu sasa anatujengea barabara ya njia nne ambayo inaingia katika mji wetu wa Bukoba Mjini. Ametutumia shilingi bilioni 12 kwa awamu ya kwanza ambapo anajenga kilometa 1.6 likiwemo na Daraja la Kanoni. Niseme ahsante sana Wizara ya Ujenzi kwa kazi kubwa wanayoifanya katika miradi hii, maana thamani ya pesa anayotoa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa wananchi na kwa ajili ya kukuza uchumi wa Taifa letu sasa inaonekana wazi. Niombe miradi yote inayotekelezeka katika Wizara zetu, wanahabari watangaze mema ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mama ametenda mambo makubwa sana tumsemee, tuyaseme watu wajue Mama yuko site, Mama halali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mama ametuletea shilingi bilioni 2.513 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali yetu ya Wilaya, Kata ya Nshambya. Kwa sasa tunaomba pesa kumalizia majengo yaliyobaki, maana hii shilingi bilioni 2.513 zimejenga vyumba 11. Sasa tumeomba pesa nyingine kwa ajili ya kujenga jengo lingine la hospitali kumalizia ambalo ni la ghorofa. Apewe nini Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mambo mema anayoyafanya katika Jimbo letu la Bukoba Mjini? Tunasema ahsante sana Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika elimu ametuletea shilingi bilioni 2.8 shule za msingi na akaleta shilingi bilioni tisa sekondari. Tumejenga sekondari za kutosha, tumejenga shule za msingi za kutosha na sasa tunapoomba kuongezewa maabara na madarasa ni kutokana na uboreshaji wa huduma za elimu ambako wanafunzi wameongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema anakwenda kutujengea Uwanja wa Ndege wa Kyabajwa. Uwanja wa ndege katika Mkoa wetu wa Kagera ni uwanja muhimu na tunauhitaji sana na kwa kuanzia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatutengea shilingi bilioni 1.6. Niiombe Wizara ya Uchukuzi na Hazina watusaidie kupata hizi pesa za upembuzi yakinifu na kulipa compensation kwa wananchi wa eneo lile ili ujenzi huu uweze kuanza mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niyashukuru sana maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kazi yetu sisi ni moja kuyatafakari, kuyaishi na kutenda vile dhamira yake inataka. Niwaombe wasaidizi wake, Mama ana mambo mengi sana kwa ajili ya Watanzania, kwa mfano katika Jimbo langu la Bukoba Mjini ametutengea shilingi bilioni moja kwa ajili ya kujenga kitega uchumi na jengo la machinga ili katika katika Jimbo letu la Bukoba Mjini ili machinga waache kuuza vitu wakitembea barabarani, wawe na sehemu yao na hapa ametenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa soko hilo. Hapa anaangalia watu wote wa hali ya chini, ya kati na ya juu. Kazi yetu ni moja kumsemea na kuunga mkono juhudi zake anazozifanya katika Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajenga Stendi ya Bukoba Mjini ya zamani sasa inakwenda kumalizika. Ametenga pale hela za kutosha zaidi ya shilingi bilioni 3.8 na sasa tunaomba atutengee pesa iliyobaki ya kumalizia jengo la kitega uchumi katika eneo lile ili wananchi wote wanaoishi maeneo yale waweze kupata maeneo yao ya kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika njia nne tunayojenga pale Bukoba Mjini, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametenga shilingi bilioni 12, lakini ameongeza shilingi milioni 340 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, kwa ajili ya Barabara kutoka pale Rwamishenye round about kwenda Kyakairabwa na kutoka Rwamishenye round about kwenda Magoti ambayo jumla ni kilometa 7.5. Niiombe Wizara ya Ujenzi upembuzi yakinifu ukamilike ili tuweze kupata pesa hizi za kuanza ujenzi wa barabara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, nipende kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri na njema anayoifanya kwa Taifa letu, lakini niwapongeze sana Mawaziri wanafanya kazi nzuri chini ya Waziri Mkuu na Mungu awabariki sana, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ENG. JOHNSTON J. MUTASINGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia katika hotuba ya Waziri Mkuu. Awali ya yote, ninapenda kumshukuru Mungu aliyetujaalia afya njema na tunaendelea na uchangiaji katika Bunge hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ninawashukuru wananchi wa Jimbo la Bukoba Mjini kwa kunichagua kuwa Mbunge wao. Ninawaahidi kwamba nitawatumikia kwa kishindo kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, ninapenda kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na njema anayoifanya na Mawaziri wote kwa ujumla. Mnafanya kazi nzuri sana na Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, ninapenda kuchangia pale kwenye ziara anazofanya Waziri Mkuu. Kweli zimetukuka na zinaonyesha jinsi ya uwajibikaji unaopaswa kuongezeka katika watumishi wa Umma. Haya yote anayoyafanya ilitakiwa yawe yameshafanywa na watumishi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba, kila mtumishi awe mzalendo kwa nchi yetu. Tukiwa wazalendo haya yote anayoyaona Waziri Mkuu kwa sasa hayatakuwepo, kwa sababu tutakuwa tunaiwaza Tanzania, na siyo mimi kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mtu akifanya kazi kwenye diameter yake akatimiza majukumu yake kwa 100%, changamoto za Watanzania zote zitaisha, maana hizi nafasi tunapewa na Mungu tuzitumie kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya katika Taifa letu ya kuwatumikia Watanzania. Mama nia yake na dhamira inaonekana wazi, kwamba sasa anapenda wananchi wapate maisha bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kuchangia pale kwenye hotuba ya Waziri Mkuu aliposema kipaumbele namba nne cha kulipa wadau na wakandarasi. Hapa ninapenda kusema jambo moja. Tunapoelekea, bajeti ya mwaka wa fedha huu, tukienda kwenye bajeti ile tukiwa na madeni, hasa kwenye miundombinu na mvua hizi zinazonyesha, tunakwenda kuwa na changamoto kubwa sana ya utekelezaji wa miradi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaiomba Serikali kwa sasa iangalie kipaumbele hasa kwenye miundombinu maana mvua zimenyesha. Bajeti mliyoletewa kwa sasa ni tofauti kabisa na kipindi cha sasa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba Serikali ijitahidi kabla ya bajeti kutekelezwa tuangalie kwenye miundombinu, tusiwe na madeni ya wakandarasi au wazabuni. Hii itasaidia pesa yote iliyotengwa kwenda kujenga barabara, na tutakuwa tumeondoa changamoto ya barabara katika maeneo yetu nchini, maana mvua zimenyesha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hata katika Jimbo letu la Bukoba Mjini, sisi terrain yetu ni mteremko, kuna makorongo na tunapata mvua kwa muda mrefu. Kwa hiyo, uharibifu wa barabara umeongezeka sana sana sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, ninashauri TARURA kuwa na kipaumbele katika manispaa zetu na majiji yetu. Sasa, tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefungua barabara sana. Kwa kweli mbarikiwe sana TARURA na Rais abarikiwe sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo langu la Bukoba Mjini, kuna baadhi ya barabara ambazo sasa inabidi zipewe kipaumbele pamoja na kwamba zimepata matengenezo na TARURA. Kuna barabara ya Nyamukazi - Pepsi. Hii barabara inaelekea kiwanda cha Samaki, lakini baada ya mvua kunyesha mchanga wote wa ziwani umeziba, ile barabara sasa haipitiki. Kwa hiyo, ninaiomba TARURA waipe kipaumbele sana hii barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara inaitwa Kahororo – Makongo – Ntoro, na hii barabara inaelekea ziwani. Kule kuna wavuvi, lakini kuna watu wanachimba mchanga na kokoto. Hii tukiimarisha, tutakuwa tumeondoa changamoto ya ajira kwa vijana ambao wanafanya zile kazi katika ile barabara, ili waweze kwenda kuchimba mchanga na kokoto pamoja na kufanya uvuvi. Kwanza itapunguza hata gharama ya usafirishaji na wale watu watapata kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Barabara ya Kashai – Kahororo, na yenyewe inafanana vilevile. Kuna Barabara ya Chemba – Rugambwa, na hii barabara kuna wawekezaji kule wameweka shule na hoteli. Sasa, tukiijenga na wale wa sekta binafsi wataajiri vijana ambao wako mjini. Sasa, Serikali iboreshe ile miundombinu ili watu wanaoenda kujenga maeneo yale waweze kujenga na vijana waweze kupata ajira, sawasawa na barabara ya Amani ambayo inaenda Kata ya Karabaga inaunganisha Jimbo la Bukoba Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu, ninaomba Serikali ijitahidi kuangalia hayo maeneo. Pamoja na kazi nzuri inayofanyika, lakini lazima tuangalie katika hilo eneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa sana. Hapa mnaposema kuna upungufu wa vyoo, kuna upungufu wa madawati, siyo upungufu. Uhitaji umeongezeka. Maana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka mazingira bora kwa Watanzania na wanafunzi kwenda shuleni. Kwa hiyo, kinachotakiwa hapa ni kuongeza na kuimarisha maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa matundu ya vyoo, mimi ninaishauri Serikali, tukisema tuwape halmashauri au manispaa kufanya hii kazi itachukua muda mrefu. Lazima mje na mkakati maalum wa kwenda kumaliza hiyo changamoto kwa wakati mmoja. Niwashauri na TAMISEMI, sasa hivi kiukweli tuna maeneo madogo ya shule. Tunapoendelea kuongeza madarasa kama tunabana yale maeneo. Tujaribu kufikiria na kuja na wazo sasa la kuanza kujenga madarasa kwa mtindo wa ghorofa ili tutumie na eneo la juu kuliko kuendelea kutumia maeneo ya chini ambayo yanazidi kuwa madogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia sana kubakiza maeneo ya shule, lakini na kuja na kitu kingine tofauti kabisa. Kwa hiyo, tunaweza tukajenga basement chini tukaja juu tukaongeza madarasa kwenda juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana, hotuba ya Waziri Mkuu alisema anakwenda kuboresha na kukarabati shule za zamani. Hili ni wazo zuri sana. Sisi katika Jimbo letu la Bukoba Mjini kuna kipindi tulipata tetemeko na tuna shule za zamani. Unaweza ukaona zile shule hazikuathirika, lakini kiinjinia unaweza kukuta zimeathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nina Shule ya Bunena, hii shule ilianzishwa mwaka 1912, Shule ya Kibeta ilianzishwa mwaka 1954, Shule ya Ihungo mwaka 1947, na Mafumbo mwaka 1973, Bilele mwaka 1970. Sasa, Serikali izipe kipaumbele hizi shule kwenda kuzikarabati na kuziwekea mazingira bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina shule moja ya Nyamukazi, hii shule iko ziwani. Pia tuna Kisiwa cha Musira, na wanafunzi wengi wanatoka Musira na boti asubuhi na mchana kurudi kuja katika shule hii. Ninaiomba Serikali ione sasa katika Shule ya Musira tunaweza kujenga bweni ili wale watoto wanaoishi kwenye kisiwa kile waweze kuja kuishi shuleni na waweze kupata ile elimu ambayo ni bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishukuru sana Serikali kwa kazi kubwa inayoifanya katika sekta zote, elimu, miundombinu, na afya. Pale Bukoba Mjini tunazungukwa na ziwa. Tuna visiwa, tuna maeneo ya kuvua, kuna Nyamukazi, kuna Musira yenyewe, kuna Kifunga. Sasa, ninaiomba Serikali katika Ziwa Victoria, ili tuweze kulinda samaki wetu lazima tufanye mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, lazima tufuate sheria. Kwa sababu sisi tunaoishi ziwani tunategemea sana samaki na dagaa, wengine ndio waliotukuza sisi mpaka hapa. Uvuvi haramu imekuwa changamoto kubwa sana ya kusababisha mpaka Ziwa lifungwe. Sasa, ninaomba wasimamizi kwenye Ziwa Victoria waangalie hili suala.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, kuainisha maeneo ya mazalia ya samaki na kuyawekea alama ili wavuvi wasiende kuvua maeneo yale. Hii itasaidia sana. Wakati unavua huku, huku kuna sehemu inaendelea kuzalisha samaki. Hii itasaidia sana kutofunga Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tuweze kuweka mipaka kati ya Tanzania na Uganda, kwa sababu tuna wavuvi wengi wanaovuka mpaka kwenda sehemu nyingine wanapata changamoto. Sasa, tutumie gharama kidogo tuweze ku-identify, katika Ziwa Victoria mpaka wetu sisi unaishia wapi? Maana hii imekuwa ni changamoto kubwa sana kwa wavuvi na kwa watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa vijana ninamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwanza ameanzisha Wizara ya Vijana lakini ametoa fedha kwa ajili ya vijana. Je, tuna uhakika gani kwamba hizi fedha zinakwenda kwa vijana walengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ametoa fedha nyingi sana kwenda kwenye Wizara, na kwenye idara tofauti tofauti. Tuna uhakika gani kwamba hizi fedha zitawafikia vijana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninaunga mkono hoja na Mungu ambariki sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Mungu akubariki sana wewe, Amen! (Makofi)