Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Christina Solomon Mndeme (1 total)

MHE. CHRISTINA S. MNDEME aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupanua wigo wa huduma za Watoto Njiti katika Vituo vya Afya vya Mkoa wa Tabora?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya kibali alichonipatia kusimama mbele hapa. Kwa moyo wa dhati kabisa nimshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuniteua ili niweze kumsaidia katika nafasi hii ya Unaibu Waziri. Pia, niwashukuru wananchi wa Muhambwe kwa kuendelea kuniamini ili niweze kuwatumikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho siyo kwa umuhimu, ninaishukuru familia yangu ambayo imeendelea kunipa ushirikiano mkubwa kwa kipindi chote cha safari yangu ya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Christina Mndeme, Mbunge Viti Maalum, kutokea Tabora.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 5.4 kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya kutolea huduma za watoto njiti kwa Mkoa wa Tabora ambapo Hospitali ya Kitete imetengewa shilingi bilioni 4.5, Nzega TC shilingi milioni 460, Urambo DC shilingi milioni 460, na ujenzi huu unatarajiwa kuanza mapema Februari, 2026.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali imepanua wigo wa huduma za watoto njiti katika Mkoa wa Tabora kwa kutenga vyumba maalum katika vituo vya kutolea huduma za afya, ambavyo vimewekewa vifaa kwa ajili ya kutoa huduma za watoto njiti kutoka vituo sifuri mwaka 2018 hadi kufikia vituo 33 mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha.