Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Ninaanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, kwa kuniteua na kuruhusu mimi kugombea nafasi hii kuwawakilisha wanawake wa Mkoa wa Tabora. Kwa namna ya pekee ninawashukuru sana Wanawake wa Mkoa wa Tabora kwa kunipigia kura ya ndiyo na leo hii ninawawakilisha hapa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee ninatoa pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kutoka Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa Keffi kilichopo Nchini Nigeria. Shahada hiyo ya uzamivu ya heshima kwa kutambua mchango wake, kama kinara wa nishati safi ya kupikia, afya ya mama na mtoto, taswira nzuri katika masuala ya uongozi kwa wanawake Afrika na kusimamia masuala ya biashara, hususan kwa vijana wa Kiafrika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hongera sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, dunia inatambua kazi zako na uongozi wako mzuri, bora na thabiti. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kipenzi na chaguo la Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachukua nafasi hii vilevile kumpongeza Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Spika wa Bunge letu, Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wenyeviti wa Bunge. Mwenyekiti wa Wanawake wote wa Tanzania, Mary Pius Chatanda, Makamu Mwenyekiti Zainab Shomari na vilevile Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa wote nchini, pamoja na Mkuu wangu wa Mkoa, Mheshimiwa Paulo Chacha wa Tabora. Tunawapongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakuu wa Wilaya, Maafisa Tarafa, Watendaji wa Kata, Watendaji wa Vijiji, Watendaji wa Mitaa, Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na wananchi wote kwa ujumla kwa kazi kubwa wanazozifanya. Hongera sana, kwani wao wanamuunga mkono Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vitendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi tunasema Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kazi zake anatekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa vitendo. Ninachukua fursa hii tena kwa dhati ya moyo wangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daktari huyu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake mahiri na bora wa kuwatumikia wananchi wa Tanzania na dunia inashuhudia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema Rais huyu ana mapenzi ya dhati kwa Watanzania, ana moyo wa dhati kwa Watanzania, anafanya kazi kwa uhodari wa dhati, ili Watanzania hawa waweze kufurahia matunda ya nchi yao. Sisi sote ni mashahidi wa kazi kubwa anayofanya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwaletea wananchi maendeleo. Tunashuhudia Tanzania ya leo, siyo Tanzania ya jana, imepiga hatua sana ya maendeleo, kila sekta imeguswa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashuhudia kila mkoa umeguswa kimaendeleo, kila wilaya imeguswa, kila tarafa imeguswa, kila kata imeguswa, kila kijiji kimeguswa, kila mtaa umeguswa na tabasamu la mama linaonekana. Tabasamu la mama tunaliona kwenye madarasa, tabasamu la mama tunaliona kwenye vifaa vya afya, tabasamu la mama tunaliona kwenye hospitali, tabasamu la mama tunaliona kwenye barabara, tabasamu la mama tunaliona kwenye ma-culvert, tabasamu la mama tunaliona kwenye madaraja, tabasamu la mama tunaliona kwenye ruzuku ya pembejeo na tabasamu la mama tunaliona kwenye chanjo za mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tabasamu la mama pia tunaliona katika ujenzi wa VETA katika kila Wilaya. Tabasamu la mama tunaliona kwenye ajira, tabasamu la mama tunaliona kwenye ujenzi wa masoko, tabasamu la mama tunaliona kwenye mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Tabasamu la mama tunaliona kwenye umeme, tabasamu la mama tunaliona kwenye SGR, tabasamu la mama tunaliona kwenye uchumi wa bluu, tabasamu la mama tunaliona kwenye utalii, tabasamu la mama tunaliona kila sekta; nani kama Mheshimiwa Samia? Hakuna wa mfano wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ujumla tuna kila sababu ya kumwombea Mheshimiwa Rais wetu huyu, ili Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema, Mwenyezi Mungu aendelee kumpa ulinzi, Mwenyezi Mungu aendelee kumpa nguvu, ili aweze kuwatumikia Watanzania hawa. Insha Allah Mwenyezi Mungu anasikia dua na sala zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anazozifanya za kuwafikia Watanzania. Ninamshukuru sana na kumpongeza kwa hotuba yake nzuri iliyoakisi hali halisi ya maendeleo ya Taifa letu. Hotuba yake nzuri ambayo inaakisi hali halisi ya bajeti na mpango wa maendeleo wa bajeti kwa Watanzania. Tunaliona tabasamu la mama katika hotuba yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawapongeza pia, viongozi wote wakiwemo Waheshimiwa Mawaziri chini ya Wizara yake, kwa kazi kubwa wanayoifanya. Mheshimiwa Rais ameleta tabasamu kila sekta kupitia falsafa yake ya “Kazi na Utu, Tunasonga mbele”. Ni kwa sababu, Mheshimiwa Rais wetu anathamini kazi, Mheshimiwa Rais wetu anathamini utu na Taifa linasonga mbele. Mheshimiwa Waziri Mkuu, yeye akiwa msimamizi wa shughuli zote za Serikali, sisi tunamwombea dua. Mwenyezi Mungu akusimamie kwani tunaona kazi zako na tunazithamini sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wewe umekuwa ukiwafikia wananchi, leo hii tunashuhudia maendeleo makubwa nchini kwetu. Sisi Wanatabora tunashuhudia Reli ya SGR kutoka Tabora – Isaka, Tabora – Kigoma inajengwa, maji kutoka Ziwa Victoria tumepata, ili kumtua mwanamke ndoo kichwani na hususan mwanamke wa Tabora. Ushauri wangu kwa Serikali ni, sisi Wanatabora tunaomba kujengewa hospitali ya kanda…
MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa Mndeme.
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: …ili tuweze kusogeza huduma za afya karibu, lakini vilevile tunaomba TARURA waongezewe fedha ili wawe na fedha za kutosha na kuondoa changamoto ya barabara. Barabara zikiwa nzuri, mnufaika mkubwa ni mwanamke na mtoto. Tunaomba semina iendelee kupanuliwa wigo kwa wanawake kupitia mikopo na uwezeshaji wananchi kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Serikali pia kupitia TAMISEMI, iendelee kuboresha mfumo mzuri wa kuhamasisha halmashauri kujiunga na biashara ya carbon, ili Serikali ipate fedha nyingi kupitia biashara hii iweze kuzalisha credit nyingi. Biashara ya carbon siyo kupitia tu misitu, biashara ya carbon, halmashauri inaweza kupata fedha kupitia nishati safi ya kupikia, nishati mbadala, majengo endelevu, green buildings, usimamizi wa takangumu (waste management), kama ilivyo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, kilimo himilivu (climate smart agriculture), usafiri endelevu, uhifadhi wa ardhi oevu (waste land conservation) ili sasa hamashauri zetu…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: …ziweze kupata fedha, kwa ajili ya kuzalisha credit nyingi na kupata fedha nyingi…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Mndeme.
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi uliyonipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia ninaomba nianze kwanza kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uzima na kubwa kuruhusu mimi kuwa Mbunge na kuruhusu mimi kuwemo Bungeni leo hii. Ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Mwenyekiti wangu wa CCM na Halmashauri Kuu kupitisha jina langu, na mimi leo kuwa Mbunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushindi mkubwa alioupata; na ushindi huu alistahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee pia ninawashukuru wanawake wa Mkoa wa Tabora ambao walinipa kura ambazo ziliniwezesha leo kuwa mwakilishi wao hapa Bungeni. Ahsanteni sana wanawake wote wa Mkoa wa Tabora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kinara mwongoza njia kwa kazi anazozifanya. Amegusa sekta zote, kila kijiji amegusa, kila mtaa amegusa, kila wilaya amegusa, kila mkoa amegusa na leo Tanzania ya leo, siyo Tanzania ya jana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze pia kwa kuwapongeza walioshiriki wote kuandaa mpango huu. Hongereni sana. Wote mlioshiriki mpango huu ni mzuri ambao unaonesha dira ya wapi tunakwenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajielekeza kwenye ushauri, nianze na agenda ya nishati safi ya kupikia. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yeye ndiye kinara namba moja nchini wa nishati safi ya kupikia, ndiye kinara namba moja wa Afrika na ndiye kinara namba moja wa ulimwengu wa nishati safi ya kupikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona agenda hii imeleta mafanikio makubwa sana. Sasa hivi idadi ya watumiaji wa nishati safi ya kupikia wameongezeka kutoka asilimia sita nukta tisa mpaka 23.2%. Kazi kubwa imefanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana na ndugu zangu walioandaa mpango huu, wamegusia suala hili. Katika hili ninamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa ruzuku ya 50% kwa mitungi 452,445 ya gesi ya kilo sita na kutoa ruzuku ya 85% kwa majiko banifu 200,000 kwa wananchi waishio vijijini na wanufaika wakubwa ni wanawake. Ninampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndugu zangu, nishati safi ni uchumi, nishati safi ni afya, na nishati safi ni mazingira. Ninaomba sasa katika hili tuendelee kupanua wigo wa utoaji wa elimu ya matumizi ya nishati safi kwa wananchi kama ilivyoelekezwa katika mkakati wa nishati safi ya kupikia aliyoizindua Mheshimiwa Rais mwezi Mei, mwaka 2024.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, katika hili niwashauri tuongeze wigo wa upatikanaji wa majiko ya gesi na majiko banifu yenye ruzuku. Vilevile, nizipongeze taasisi 1,136 ambazo zimeitikia wito wa matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo zikiwemo Jeshi la Magereza, Jeshi la Polisi, Jeshi la Kujenga Taifa, baadhi ya vyuo vya elimu, hospitali zetu, shule na vyuo vingine vya kati, tunazipongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu katika mpango huu ningeshauri, zipo taasisi ambazo bado hazijaunga mkono juhudi hizi za Mheshimiwa Rais. Agenda hii Mheshimiwa Rais ameileta kwa Watanzania kwa nia njema na nzuri akiwa yeye ni mwanamazingira namba moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuweke sheria, kanuni na miongozo mbalimbali na tuisimamie. Taasisi ambazo zinalisha watu zaidi ya 100 ambazo bado hazijaanza kutumia nishati safi ya kupikia zitumie. Isiwe sasa ni hiari, bali iwe ni lazima kwa mujibu wa sheria na taratibu ili mazingira yetu tuyatunze. Vilevile, sasa hivi kuna kaya takribani 2,000 zinatumia gesi asilia (natural gas) kwa ajili ya kupikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali hii inapatikana nchini kwa manufaa ya Watanzania. Ninashauri katika mpango wetu tuongeze wigo wa matumizi ya gesi asilia kwa matumizi ya kupikia majumbani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninashauri tunahitaji uwekezaji katika nishati safi ya kupikia. Tunahitaji nishati safi, na teknolojia ya nishati safi. Tunamlenga mwanamke kwa sababu nishati safi ni Uchumi. Mama atatumia muda mfupi kupika na muda mrefu kufanya shughuli za uzalishaji mali. Tunamtaja mwanamke kwa sababu mwanamke ndiyo anatumia muda mwingi jikoni, yeye na mtoto wa kike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri kama ilivyoelekezwa kwenye mkakati wa nishati safi ya kupikia, tupunguze tozo na kodi kwenye nishati safi na teknolojia ya nishati safi ya kupikia na mashine za kutengenezea majiko haya ili sasa yapatikane kwa bei nafuu na wafanyabiashara wengi wawekeze katika nishati safi ya kupikia, na vilevile tuwe na teknolojia ya Pay As You Use. Unalipa kulingana na matumizi yako ya gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, kutokana na kazi nzuri anayoifanya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha kwamba Taifa hili linahama kutumia nishati isiyo salama na kutumia nishati iliyo salama, tuweke mazingira mazuri ili sasa wawekezaji waje kuwekeza zaidi na zaidi katika nishati safi ya kupikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ninaomba kushauri ni suala la watoto njiti. Takribani watoto 300,000 huzaliwa njiti ndani ya nchi yetu. Tupanue sana huduma ya watoto hawa ili wasipotee kwa sababu wakipotea ni nguvu kazi inapotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la Special Economic Zone. Haya maeneo ni muhimu sana kwa ukuaji wa Uchumi. Tupanue wigo ili sasa hizi Special Economic Zone zifanye kazi. Zikifanya kazi, wanawake wa Kitanzania watafanya biashara katika maeneo yao wanapopatia kipato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la kongani (clusters) tuzipe umuhimu na kuzipanua, kongani za kilimo, za mifugo, za viwanda. Hizi kongani zikifanya vizuri uzalishaji ukaongezeka, mwanamke huyu wa Kitanzania atafanya biashara katika maeneo hayo na atatupatia fedha ya kujikimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni viwanda kufufuliwa. Tufufue viwanda vilivyokufa. Kwa mfano, Kiwanda cha Nyuzi Tabora kimekufa, kiwanda cha Maziwa Mkoani Tabora kimekufa. Tufufue viwanda hivi ili wanawake hawa na vijana wetu wapate ajira na uchumi ukue, wazalishe ili pato la nchi liweze kuongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhakikisha kwamba wale waliopewa viwanda wameshindwa kuviendeleza wanyang’anywe wapewe wenye uwezo ili sasa vifanye kazi, uchumi ukue na watu wapate ajira wakiwemo akinamama; watafanya biashara ndogo ndogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuongeza kasi ya ujenzi wa viwanda. Tujenge viwanda ili sasa maeneo ya kufanya biashara yawepo na ajira ikue ili uchumi wa wananchi wetu uweze kukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mikopo kwa wanawake. Ninaomba tuongeze wigo wa utoaji wa elimu ya mikopo hii inayotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Mikopo ile inapotolewa tuhakikishe mazingira ya kufanyia biashara yanakuwa mazuri, na pia tutoe elimu, biashara za kuzalisha, wazalishe biashara zenye tija; TBS wafanye kazi, watembelee wanawake wawape elimu ya uzalishaji mali ili akinamama hawa waweze kukua katika bidhaa wanazozalisha. Pia wanapokwenda kwenye benki, wapate mikopo ya masharti nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ninaona muda wangu unakwenda, ni suala la mazingira…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Malizia, Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. CHRISTINA S. MNDEME: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kuwa na Taifa lenye kustahimili mabadiliko ya tabia ya nchi na himilivu, tutunze mazingira yatulinde na sisi tuyatunze sekta ya kilimo ikue ili sasa mwanamke afanye kazi maana mama ndiyo mkulima mkubwa nchini, kwa sababu sisi tupo wengi zaidi, takribani ya 51%. Tulime, tuzalishe, tutunze familia zetu na uchumi ukue kuanzia ndani ya familia na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa muda ulionipa, ninaunga mkono hoja. (Makofi)