Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mahesh Shah Bolisha (1 total)

MHE. MAHESH SHAH AKLUSHA BOLISHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Wizara ina mpango wowote wa kujenga kituo kidogo katika Wadi ya Kiuyu karibu na eneo la Mabutu kwa kuwa eneo hili limewekwa kwa ajili ya uwekezaji, na ni prime location kwa ajili ya wawekezaji kutoka nje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafikiri tuna kituo kikubwa kinajengwa cha Polisi ndani ya Jimbo la Micheweni, lakini patakuwa ni mbali kidogo kutoka Mabutu mpaka hapo kituo kinapojengwa. Je, tuna mpango wowote wa kujenga kituo kidogo katika eneo la Mabutu karibu na eneo la uwekezaji kwa ajili ya security? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mahesh, Mbunge wa Micheweni kwa swali lake ambalo ameomba kujengewa kituo kidogo katika eneo la Kiuyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulieleza kwenye mpango wa jumla wa ujenzi wa vituo vya Polisi kwamba, azma ya Serikali ni kufikisha huduma za kiusalama katika kila kata kuwe na kituo cha Polisi, lakini utekelezaji wa azma hiyo utategemea sana hali halisi ya upatikanaji wa fedha, na vile vile mpango wa hali ya usalama katika maeneo husika. Ndiyo maana tukaja na ule mpango mkuu wa kwamba tutaanza na maeneo ambayo yamebainika kiusalama yana uhitaji wa haraka zaidi halafu baadaye twende kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwahidi tu Mheshimiwa Mahesh kwamba hoja yake tunaichukua, na ikiwa Kituo cha Kiuyu kipo kwenye mpango wa dharura, basi kitaweza kujengwa katika utaratibu wa mpango huu.