MHE. TAMIMA HAJI ABASS aliuliza: -
Je, upi mpango wa Serikali wa kuimarisha Mawasiliano ya Simu kwenye Vijiji vyenye changamoto ya huduma hiyo Mkoa wa Kaskazini Unguja?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Tamima Haji Abass, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilitekeleza mradi wa kimkakati wa kufikisha mawasiliano katika Shehia 38 zilizokuwa na changamoto ya mawasiliano ambapo jumla ya minara 42 ilijengwa kwa kushirikiana na mtoa huduma Honora/YAS.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya minara hiyo Mkoa wa Kaskazini Unguja ulinufaika kwa kujengewa Minara 12 ambapo mradi huu ulikamilika kikamilifu na kwa sasa wananchi wananufaika na huduma za mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada zilizofanyika kama nilivyotangulia kuzitaja, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kushirikiana na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imebaini kuwepo kwa changamoto za Mawasiliano katika Shehia ya Mafufuni, iliyoko Wilaya ya Kaskazini “B” pamoja na Shehia ya Tazari iliyoko Wilaya ya Kaskazini “A” ambapo kwa upande wa Shehia ya Mafufuni tayari imejumuishwa katika Mradi wa Awamu ya Kumi ambao mikataba yake ilisainiwa tarehe 5 Disemba, 2025. Pia Kampuni ya YAS inatarajiwa kujenga mnara katika Shehia hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Shehia ya Tazari pamoja na maeneo mengine ya pembezoni ya Mkoa wa Kaskazini Unguja yatajumuishwa katika awamu zinazofuata.