Supplementary Questions from Hon. Joshua Samwel Nassari (3 total)
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona, nina swali moja tu kwa upande wa Serikali. Wilaya kongwe ya Arumeru Makao Makuu yake ni Halmashauri ya Mji Mdogo wa Usa River. Fortunately, kwa miaka yote Halmashauri ya Mji Mdogo ule haina hata kilometa moja ya lami katika Mji wa Usa River. Tulitenga kilometa tano, na wananchi wakafanyiwa sensitization na Wizara kwa ile teknolojia mbadala ambayo imefanyika kwenye maeneo mengine, lakini unfortunately ile ya kwetu ya Meru haikujengwa kilometa tano pale Mji wa Usa River.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali. Ni lini jambo hili litakwenda kutekelezwa ili na yale maandamano ambayo mwaka 2025 kabla sijawa Mbunge yaliyowatoa wananchi wa Usa River kwenda kwa Mkuu wa Mkoa kwa sababu yasifanyike tena? Wananchi walishafanyiwa sensitization na kuachia maeneo yao na hakuna component ya fidia. Ni lini barabara hizi zitatekelezwa (five kilometers) kwenye Mamlaka ya Mji Mdogo wa Usa River? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikiri kwamba nimefika kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mbunge, tuliambatana naye kwenda kufanya ukaguzi kwenye barabara ambayo tunaijenga kwa kiwango cha lami. Hivyo hivyo, kama ambavyo tumefanya jitihada kwenye barabara ile tuliyoikagua, tutaendelea kufanya jitihada kama Serikali kuhakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo ili wananchi wa Arumeru na Makao Makuu ya Jimbo hilo Usa River waweze kupata huduma nzuri za barabara. (Makofi)
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru. Nitumie nafasi hii kuipongeza kwanza Wizara ya Maji kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya kwenye majimbo yetu huko, lakini nina swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Uwilo pale Arumeru pamoja na Mradi mkubwa wa Maji wa Embaseni - Kikatiti pale Arumeru, ni lini Serikali itapeleka fedha ili wakandarasi waweze kurudi site na miradi hii iweze kuendelea kwa sababu tayari ilikwishaanza lakini imesimama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassari, Mbunge wa Arumeru, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Nassari kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya, lakini kubwa zaidi ushirikiano wake na Wizara ya Maji katika kubainisha changamoto zinazotokea katika jimbo lake. Tunamhakikishia kwamba, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan itapeleka fedha ili kuhakikisha miradi hii inakamilika na iweze kutoa matokeo na wananchi waweze kuona maji kwenye bomba hatimaye sasa nchi yetu isiwe na tatizo la water stress. Kwa hiyo, tunamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, hilo tunalichukua kwa makini sana. Ahsante sana.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kuniona. Swali la msingi limeulizia habari ya soko na bei ya maziwa kwa wafugaji. Sasa Katika kukabiliana na tatizo hilo la soko na bei, wakulima na wafugaji wa Meru wameanzisha umoja wao unaitwa UWAWAME (Umoja wa Wakulima na Wafugaji Meru). Wanachohitaji kwa Serikali ili waweze kusaidika ni kuongeza thamani kwenye mazao ya maziwa na vitu vingine. Kuna baadhi ya vitu ambavyo wanahitaji msaada kutoka kwa Serikali kwa maana ya Wizara inayohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali iko tayari basi kukutana na hawa UWAWAME ili waweze kuwasaidia waweze kukabiliana na hii changamoto ya bei na soko kwenye maziwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ninamshukuru pia Mbunge kwa sababu mara kwa mara amekuwa akiniuliza juu ya namna gani tunaweza tukawafanya UWAWAME waweze kuendelea kuzalisha kwa tija zaidi hasa wafugaji katika umoja juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge katika muda na saa ambao tutapanga kwa pamoja na Wizara tupo tayari kukutana na UWAWAME ili twende tukaone namna gani ya kuwaongezea tija katika uzalishaji wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.