Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwanza kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu jioni ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo pengine ni siku ndefu kwangu au kwa sababu nitazungumza dakika karibu kumi, nichukue nafasi hii pia kumshukuru sana Mungu aliyenipa uzima na kunipa nguvu za kuweza kunifikisha siku ya leo ili niweze kuchangia. Pia ninawashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Mbozi walioamua kunichagua na kunifikisha hapa Bungeni ili niweze kuwasemea, kuwawakilisha niseme tu nitawakilisha uwezo ninao, nguvu ninayo na nia ninayo, nitafanya kazi usiku na mchana kwa ajili ya wananchi wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wengi tumemshukuru na ni kweli Rais wetu inawezekana hasemi sana, lakini kazi zake zinaonekana. Kazi zinaonekana anazozifanya Mheshimiwa Rais, Majimboni mwetu ni mashahidi wote Wabunge wanaona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Waziri Mkuu ameanza ziara na kwangu ameshafika amefanya kazi kubwa na ile ndiyo ambayo tunataka hata kule chini kwa watendaji, kule chini wote wacheze mpira mmoja. Sina shaka na hilo Mawaziri wapo hapo watamsaidia Waziri Mkuu, watamsaidia Rais, sisi tutawakimbilia wao usiku tutakwenda kwao, mchana tutakwenda kwao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia Chipando anasema amefika mpaka nyumbani kwa Mheshimiwa Waziri, rafiki yangu Profesa Shemdoe, kama mambo hayaendi, mimi nitakwenda. Ninawashukuru Wabunge pia wamefika hapa kwa kweli wamefanya kazi kubwa, hongera sana Wabunge kwa kuchaguliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie, wakati ninagombea nafasi hii, wakati ninaomba ridhaa kwa wananchi niliwaahidi jambo moja na wao walinituma kwa jambo kubwa moja ambalo limekuwa ni mfupa kwa Jimbo langu la Mbozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni suala la barabara. Barabara zetu za Mkoa wa Songwe za Jimbo langu hasa Jimbo langu nikianza na Barabara ya Mlowo – Kamsamba. Hii barabara imekuwa na shida miaka nenda rudi, ninaweza nikasema toka uhuru hii barabara, tunaomba ijengwe kwa kiwango cha lami, kilometa 130 toka uhuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan amevunja rekodi na alipokuja nilimwambia Mama umevunja rekodi endelea kushikilia hapo hapo. Tumesaini barabara ile kwa kiwango cha lami kilometa tano kutoka Jimbo langu na kilometa tano kutoka kwenye Jimbo la mwenzangu Condester Sichalwe, Jimbo la Momba ili mkandarasi aanze Momba na mwingine aanze Mlowo wakutane katikati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajiuliza kilometa tano, kilometa 10 barabara yenye kilometa 130 tutamaliza lini? Ni zaidi ya miaka 13 tukienda kwa mtindo huo, miaka 13 tunajenga tu. Sasa niiombe Serikali kwa kuwa barabara hii mimi kama Mbunge nilishawaambia wananchi wangu wanielewe kabisa, nitapambana na mambo mengine, lakini Barabara ya Mlowo – Kamsamba ndicho kitakachokuwa kipaumbele chetu kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka hii mitano tunaomba barabara hii ianze kujengwa ili iweze kuisha na wananchi waondokane na adha wanayoipata kilometa 130, tuipe mkakati siyo kilometa tano hizi, ninashukuru sana kwa hizi kilometa tano, lakini naomba sasa watupe kilometa za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu ni kilometa 65, Jimbo la mwenzangu ni kilometa 65 jumla 130, barabara hii Waziri wangu na rafiki yangu kutoka kule Mheshimiwa Deus Sangu, yeye anajua barabara hii tunakutana naye kule, Wabunge hapa hakuna Mbunge hajala mchele wa kule Kamsamba, unatoka kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge hapa wanajua kabisa tuna dhahabu ya kahawa inatoka barabara hiyo, tuna mahindi yanatoka barabara hiyo, tunayo maharage na kila kitu, hilo ndiyo ombi langu tu nimesimama kuomba barabara hii, kaka yangu Naibu Waziri Kasekenya na Waziri Ulega wanaona ninavyowafuatafuata ofisini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge waliotangulia kwenye Jimbo lile kila mmoja alipiga kelele barabara ile, sasa sijui wanataka nifanyaje? Nitahakikisha ninagombana nao, anisaidie barabara ile kaka yangu Kasekenya. Rais alishaagiza ijengwe yote kwenye kampeni, Waziri Mkuu amekuja pale ameagiza mkandarasi alipwe fedha za kianzio bilioni 3.8 mpaka sasa hayajalipwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tupo kwenye Bunge la Bajeti, ninaomba kabla hatujarudi mkandarasi ashuke pale site aanze kufanya kazi wananchi wanatusubiri, watatusubiri mpaka lini? Tutakuwa tunawaambia itajengwa itajengwa, sasa safari hii nimekuja Mbunge kijana. Nimeahidi kuchapa kazi, sijaahidi siasa ninataka tukafanye kazi barabara hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo pia barabara nyingine hasa hii ipo TARURA na nimeiombea Barabara ya Mlowo – Mpito – Isansa ina kilometa 13.6 iko chini ya TARURA. Kwa kweli, kwa upande wa TARURA tuombe sana waongezewe fedha za kutosha ikiwezekana kipindi hiki cha mvua Mawaziri wangefanya ziara kwenye Majimbo ndipo watatambua shida tulizonazo na barabara hizi za TARURA, tuna shida mno. Niiombe barabara hii tuipandishe hadhi kutoka TARURA iende TANROADS. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi hiki mvua zinanyesha kule kuna hospitali, kuna kituo cha afya kimejengwa na Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan lakini barabara haipitiki. Wananchi wataendaje kutibiwa kule? Akina mama wajawazito wataendaje kule? Niombe sana kipindi hiki tuhakikishe tunaipa TARURA fedha za dharura. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawauliza jamani vipi? Wanasema hakuna fedha za dharura tunafanyaje, hivi hapa ninawaza Ijumaa nirudi kwenda angalau nitafute hata chochote mfukoni mwangu nikaweze kurekebisha rekebisha mashimo kule, hivi kweli? Niombe tuziangalie hizi barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zingine za TARURA ni Barabara ya Itepula – Shasya – Halungu iangaliwe barabara hii. Sisi ni wakulima tunataka tusafirishe mazao yetu kutoka vijijini kuja mjini barabara hamna, tunaomba sana tuangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wa Msanyira wananisikia hapa barabara yenu nimekuja juzi haipitiki, niko hapa kuhakikisha ninaiomba Serikali iweze kupitika. Watu wa Intentula, watu wa Isani, watu wa Isela barabara ile na yenyewe itakuja kupitika nitamfuata rafiki yangu, kaka yangu Profesa Shemdoe analifahamu, yeye ndiye mlezi wangu, ninaomba anisaidie sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kelele pekee sasa hivi kule ni barabara. Watu wa Mwanjelwa wamenipigia simu wanataka Barabara yao ya Mwanjelwa kwenda kule Shitungulu. Nitampeleka Waziri apafahamu, lakini nazo barabara nyingi na muda wangu umeniishia, ila kilio changu kwa miaka hii mitano ni Barabara ya Mlowo – Kamsamba ninahitaji ijengwe sasa.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja. (Makofi)