Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Othman Maulid Suleiman (1 total)

MHE. OTHMAN MAULID SULEIMAN aliuliza:-

Je, ipi mikakati ya Serikali ya kuongeza viwanda nchini ili kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara ninaomba nijibu swali namba 82 kutoka kwa Mheshimiwa Othman Maulid Suleiman, Mbunge wa Mahonda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya CCM pamoja na Dira ya Maendeleo ya 2020 - 2050 inatoa kipaumbele kwenye uwekezaji na uzalishaji wa ndani, ongezeko la thamani la bidhaa zetu za ndani na mkakati wa Serikali unalenga katika kukuza uchumi wa viwanda, kuanzisha viwanda vipya na kufufua viwanda ambavyo vimesimamisha uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika muktadha huo, hadi kufikia mwezi Desemba, 2025, Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi, imefanikiwa kuanzisha kongani 36 katika mikoa 16 nchini. Kati ya hizo, kongani sita zipo katika hatua ya ujenzi na baadhi ya viwanda ndani ya kongani hizo, tayari vimeanza uzalishaji. Mathalani, Kongani ya Kwala iliyopo Mkoa wa Pwani na Kongani ya Kilimanjaro iliyopo Kigamboni ambapo kila moja ina viwanda vinne ambavyo vinaendelea na uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali imeanza kutekeleza Mpango Maalum wa Miaka sita (2025/2026 – 2030) wa kuendeleza viwanda vya ndani ambapo kupitia mpango huo, kongani zipatazo 52 (kongani mbili kwa kila mkoa) zitajengwa. Ujenzi wa kongani hizi zenye viwanda ndani yake utasaidia kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.