MHE. PROF. PIUS Z. YANDA aliuliza: -
Je, lini Serikali itajenga Chuo cha TEHAMA Wilayani Buhigwe ili kutekeleza ahadi ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prof. Pius Zebhe Yanda, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imewezesha upatikanaji wa eneo la ujenzi wa chuo lenye ukubwa wa ekari 155 katika Kijiji cha Songambele, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe. Pamoja na hiyo Serikali tayari imekamilisha upembuzi yakinifu wa mradi wa ujenzi wa chuo hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya tathmini ya gharama ya ujenzi wa chuo ambapo inakadiriwa kuwa kiasi cha shilingi bilioni 113 kitahitajika kukamilisha ujenzi husika. Kwa sasa Serikali inaendelea na utaratibu wa kutafuta vyanzo mbalimbali vya fedha ili kuanza ujenzi wa chuo husika.