Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Omary Marcus Msigwa (1 total)

MHE. OMARY M. MSIGWA aliuliza: -

Je, lini Serikali italeta fedha katika Jimbo la Madaba ili kutatua changamoto ya maji katika Vijiji vya Gumbiro, Ngadinda na Lilondo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Omary Marcus Msigwa, Mbunge wa Jimbo la Madaba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji vya Gumbiro, Ngadinda na Lilondo vilivyopo Halmashauri ya Madaba Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma. Miradi hiyo kwa pamoja inagharimu jumla ya shilingi bilioni 2.451 ambapo inahusisha ujenzi wa vyanzo vya maji vitatu; ujenzi wa matanki matatu yenye jumla ya ujazo wa lita 325,000, ulazaji wa mabomba umbali wa kilometa 62.9, sanjari na ujenzi wa vituo 28 vya kuchotea maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hiyo ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo inatarajiwa kukamilika ndani ya mwaka wa fedha 2025/2026 na kunufaisha zaidi wananchi 12,570 waishio katika Vijiji vya Gumbiro, Ngadinda na Lilondo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, hadi kufikia Mwezi Machi, 2026, Serikali imelipa jumla ya shilingi bilioni 1.536 katika utekelezaji wa miradi hiyo na itaendelea kupeleka fedha kadiri zinavyopatikana ili iweze kukamilika na kuanza kutoa huduma iliyokusudiwa kwa wananchi.