Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Happiness Daniel Ngwando (2 total)

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kuuliza swali la nyongeza. Serikali ina mpango gani wa kuweka network kwenye hospitali zetu ambazo zinatumia system, ili kupunguza mgonjwa kukaa muda mrefu kumsubiria daktari apate network. Kwa mfano, Hospitali ya Wilaya ya Nyasa na Nangombo, Tunduru, ili daktari apate network inabidi atoke nje kutafuta mnara. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka network haraka ili wananchi wetu wasipate usumbufu wa kusubiri majibu muda mrefu hususan wanawake wa Mkoa wa Ruvuma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza kwamba tuna mkakati wa miaka mitano wa kupeleka mawasiliano ya simu na data katika maeneo yote nchini. Katika haya maeneo ya hospitali na maeneo mengine muhimu, tutayatekeleza katika awamu ya 11 ambapo Serikali ina mpango wa kupeleka mawasiliano ya internet na data katika maeneo ya mkakati yakiwemo haya ya miundombinu ya Serikali ikiwemo Reli ya TAZARA, SGR, MGR ikiwemo mbuga ya hifadhi za wanyama na maeneo mengine ya kimkakati kama hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo hilo pia kama Serikali tunalifanyia kazi na lipo kwenye mkakati mahususi wa Wizara. Kwa hiyo, tutalifanyia kazi na maeneo yote hayo yatapata mawasiliano ya internet.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na tumshukuru sana Mheshimiwa Happiness kwa maswali yake na kuweka msisitizo kuhakikisha kwamba Wilaya ya Nyasa na Tunduru zinapata mawasiliano ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Happiness, katika mradi wetu wa utekelezaji wa ujenzi wa minara 201, Wilaya ya Nyasa tutaweka minara miwili katika Kata ya Liuli pamoja na Mpepo. Vilevile kwa Wilaya ya Tunduru tutajenga mnara katika Kata ya Mchesi pamoja na Mlingoti Magharibi. Hivyo basi, niendelee kumhakikishia kwamba sasa hivi tunakamisha ujenzi wa minara 908 katika kata 730, na tutahakikisha kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyoeleza katika makakati wetu, tuwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, ifikapo 2030 hakuna eneo ambalo litakuwa halina mawasiliano. Nashukuru kwa nafasi. (Makofi)
MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa, mfumo huu umewaathiri sana wanawake wa Mkoa wa Ruvuma, ile kwenda na kurudi kwa ajili ya kufuatilia kupata mkopo huu, kiasi kwamba, wametumia gharama zao, na biashara zao zimefilisika kwa vile ni biashara ndogo ndogo kama mbogamboga au mama lishe. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wamama hawa kupata fedha kwa haraka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa mikopo hii ili kuanza kupunguza muda wa kusubiri, lakini pia, kuondoa gharama zisizokuwa na lazima na usumbufu kwa wajasiriamali wanaohitaji mikopo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunaendelea kuboresha. Moja ya mambo ambayo Serikali imetoa maelekezo, nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI kuwasisitiza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kwamba, vikundi vya wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu mara baada ya kuwasilisha maombi yao, wapewe taarifa kwa njia ya simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itawafanya wasilazimike kusafiri kwenda na kurudi mara kwa mara, ili kuepuka gharama za nauli na gharama kubwa katika kuomba mikopo. Mikopo inapokuwa tayari wapewe taarifa kwa utaratibu wa uwazi kwa njia ya simu na mbao za matangazo, ili wananchi waweze kupata mikopo hiyo kwa wakati, na pia, bila kutumia gharama kubwa.