MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -
Je, lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Daraja la Mtomoni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa daraja la Mitomoni unatekelezwa kupitia fedha za dharura zilizotolewa na Benki ya Dunia kupitia dirisha la Contingent Emergency Response Component (CERC) kwa gharama ya shilingi bilioni 9.29. Mkataba wa mradi huu ulisainiwa tarehe 1 Novemba, 2024. Hadi sasa utekelezaji wa mradi huu umefikia 21% na unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2025.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -
Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mshangano – Legele hadi Mletele?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. ZAINAB A. KATIMBA) alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa ujenzi wa barabara ya Mshangano - Legele hadi Mletele, na tayari imefanya usanifu wa ujenzi kwa kiwango cha lami ambapo kiasi cha shilingi bilioni 2.513 kinahitajika ili kujenga kilometa tano, na kwa sasa inaendelea kutafuta fedha za kutekeleza mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali imekuwa ikiendelea kuifanyia matengenezo barabara hii, ambapo katika mwaka 2022/2023 yalifanyika matengenezo ya kuifungua barabara, kung’oa miti, ujenzi wa mitaro, ujenzi wa makalavati na uwekwaji wa changarawe kwa gharama ya shilingi milioni 42.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2023/2024 na 2024/2025 Serikali ilifanya matengenezo ya kawaida katika barabara hiyo ikiwa ni pamoja na kuendelea kuimarisha tuta la barabara kwa kuichonga na kuchimba mitaro ya kutolea maji ya mvua kwa gharama ya shilingi milioni 84.5.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2025/2026 Serikali imeweka katika mipango yake matengenezo ya kawaida kwa shilingi milioni 47.5. Serikali itaendelea kuihudumia miundombinu ya barabara na madaraja ya Mji wa Songea kwa kuijenga, kuikarabati na kuifanyia matengenezo kulingana na upatikanaji wa fedha.