Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Yohana Stephen Msita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Itigi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. YOHANA S. MSITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na mimi kunipatia fursa hii ya kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia afya na uzima. Ninaomba kipekee sana niendelee kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona Mheshimiwa Rais ana moyo wa uzalendo, amejitoa kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania. Nimpongeze pia Makamu wa Rais kwa kazi ambazo anaendelea kuzifanya, vilevile, Waziri wetu Mkuu kwa kazi kubwa ambazo wanaendelea kuzifanya nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana ninaomba nimpongeze Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera pamoja na Naibu wake Zainab Katimba. Bila kumsahau Katibu Mkuu. Niseme tu mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria. Hakika watu hawa wanafanya kazi nzuri sana. Watu wa Wizara ya Katiba na Sheria wanapambana kweli kweli. Hongereni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba uniruhusu sasa nianze kwanza kwa kutambua kauli mbiu ya Wizara hii ambayo inasema: “Haki, usawa na utawala wa sheria kwa watu wote.” Huu ndiyo msingi. Yako maandiko yanasema: “Kama misingi ikaharibika mwenye haki atafanya nini?” Tunapozungumzia Tanzania maana yake tunazungumzia Wizara hii ambayo ni Wizara mama ambao ndiyo msingi wa nchi. Wizara ya Katiba na Sheria ndiyo inabeba mambo yote, ndiyo inayoifanya Tanzania inaonekana katika sura hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uniruhusu nianze kuzungumzia msaada wa kisheria. Ninapozungumza msaada wa kisheria hapa ninazungumzia Mama Samia Legal Aid Campaign ambayo kwa kweli imefanya kazi kubwa sana. Niendelee kuwapongeza kwa kuendelea kufanya jambo hili zuri kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninapitia takwimu za huu msaada wa kisheria wa Mama Samia Legal Aid Campaign. Takribani wananchi 3,000,000 hadi kufikia Juni 2025 wamefikiwa na msaada huu wa kisheria, hilo ni jambo kubwa sana. Kazi kubwa imefanyika katika kutatua migogoro ya ardhi, kutatua migogoro ya mirathi na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo si la kupuuzwa. Watu 3,000,000 ni wengi sana, lakini niendelee kutoa ushauri wangu kwa Wizara kwamba jambo hili liwe endelevu. Limewasaidia Watanzania wenzetu ambao wamekutana na changamoto mbalimbali wakati mwingine wao kushindwa kuelewana. Chombo hiki kikifika kinafanya utatuzi mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, misaada mingi ya kisheria imeendelea kuwepo ambayo kwa kweli takribani Watanzania milioni 7.4 wameendelea kusaidiwa katika kutatua changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu mambo machache ambayo katika kutembelea miradi ambayo inasimamiwa na Wizara hii tumeona kuna mambo fulani ambayo yanahitaji kufanyiwa marekebisho kidogo au kuongeza kasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema pale awali Wizara hii ndiyo msingi na Kamati katika kutembelea, tumetembelea miradi ikiwemo ya Jengo la Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Singida. Jengo hili ni jengo zuri, lakini ujenzi umekuwa wa kusuasua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe Serikali kama kweli tunataka kuelekea kwenye Dira ya 2050 kama ambavyo inasema katika ukurasa wa 30 kwamba Taifa la kidemokrasia linalozingatia utawala wa sheria, haki za binadamu na upatikanaji wa haki jamii lazima tuhakikishe tunaboresha miundombinu kwa kupeleka fedha ili miundombinu hii iweze kukamilika na wananchi wetu waweze kupatiwa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitembelea pia Kituo cha Jumuishi cha Taasisi za Kisheria Mwanza. Hapa tumekuta fedha nyingi zimetumika, lakini jengo halijakamilika, bado linasuasua sana. Sasa kusuasua huku maana yake tunawachelewesha Watanzania kupatiwa haki zao na kupata huduma kwa ukaribu. Niiombe sana Serikali iendelee kukimbiza na kupeleka fedha pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tuligundua pale kuna changamoto kwa wajenzi wa Suma JKT. Hawa nao tumeona wanasuasua wameshapokea fedha karibu shilingi bilioni 2.9% lakini kwa kweli maendeleo ya kazi yalikuwa bado karibu 74%. Sasa hii ninaona ni jambo ambalo litatuchelewesha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambapo kwa kweli hapa ninadhani tunahitaji kuongeza kasi sana na Serikali ije na mkakati maalum wa kuhakikisha kwamba tunafikia yale matarajio. Nimeona kwamba mashauri yalipokelewa karibu 10,398, lakini mpaka kufikia Februari, 2026 ni mashauri 604 tu ndiyo yaliyokamilika, ambayo ni sawasawa na 5.8%. Mashauri mengine bado yapo kwenye mchakato. Ninadhani Serikali ije na mpango mahususi wa kuhakikisha inaongeza kasi katika eneo hili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante kwa mchango wako. Muda wako umekwisha.

MHE. YOHANA S. MSITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.