Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Happiness Daniel Ngwando

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nami nimshukuru Mungu kwa afya aliyonijalia jioni ya leo. Nimshukuru sana pia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutupambania wanawake katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitakuwa na mambo machache tu kuhusu sheria, nimesimama hapa kwa ajili ya wanawake wa Mkoa wa Ruvuma kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022, ni wanawake 953,000 ambao wako huko na wanatamani kuona nini juu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya leo nitakuwa kwenye mambo mawili au matatu. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, kwa kazi nzuri anayoifanya hasa ile ya kusema na Waziri moja kwa moja, tunashukuru sana wakati akiwa anatatua kero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana pia Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria na kumpongeza kwa kazi anayofanya hasa ile kazi ya Mama Samia Legal Aids ambayo inatufikia hata kwenye mkoa wetu na watu wetu wanawake wanaendelea kupata haki zao, wanaendelea kusikilizwa kero mbalimbali katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina sehemu mbili au tatu. Niko kwenye suala la sheria ya mwanamke au binti upande wa ndoa. Sehemu ya kwanza ni ile ambayo inamtaka mtoto wa kike mwenye miaka 14, ndiyo yeye anatakiwa kuolewa kwa mujibu wa mzazi, lakini mtoto wa kiume wa miaka 18 yeye ndiye atakuwa akifikisha miaka 18.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyoona sasa hivi elimu msingi inaanzia awali mpaka kidato cha nne, mtoto huyu mwenye miaka 14 sheria hii ikiendelea kubaki ikikaa silence haieleweki vizuri, mtoto huyu hatapata haki ya kusoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mtoto mwenye miaka 14 bado katika uhalisia kwetu ni mtoto mdogo sana. Hapa nawaona wanangu wa darasa la saba sasa hivi wanapata mimba huko nyumbani leba akiingia mama unaanza kuchanganyikiwa nje. Si sahihi na tunaomba sana sheria hii isiwe na kigugumizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto hawa wenye miaka 14 tunaomba waingizwe kwenye miaka 18 kama watoto wa kiume kwa kuwa hata Katiba yetu inakataza ubaguzi kati ya mtoto wa kike na mtoto wa kiume. Sheria hii isiwe na kigugumizi tunaomba sana kama mwakilishi wa wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Sheria za Ndoa yanasemwa mengi na wenye sheria zetu huko na wataalam walioziandika sheria hizi. Kiuhalisia sheria hizi zimepitwa na wakati ukilinganisha na mfumo wa mwanamke sasa hivi ulivyo. Mwanamke sasa hivi ndiyo mchumi kwenye nyumba zetu na familia zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru wametuelimisha sana na somo limeeleweka, wanawake sasa hivi nyumbani wanamiliki pesa, wanamiliki kila kitu ambacho mwanaume anaweza kumiliki. Sheria bado inamtaka mwanamke, huyu hata hasa pale kwenye mirathi unakuta anaambiwa mwanaume akifariki yeye anapata moja ya tatu anagawiwa kidogo, lakini haitoshi mama huyu huyu akitokea anafariki, katika baadhi ya sehemu, anatolewa kwenye nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapata meseji nyingi kama wawakilishi na hapa simwongelei mwanamke msomi, mwanamke mwenye lace wig. Mwanamke ninayemwongelea ni mwanamke wa kijijini, Mkoa wa Ruvuma kule ambaye haijui sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba uelewa kwenye hili; sheria inasemaje mwanamke huyu anapofiwa, kwa nini nyumba yake anayoishi na mume wake wa ujana iwe ndani ya mirathi? Kwa nini nimekaa na mume wangu ujana wote leo unaniambia ninatakiwa nitoke kwa sababu amefariki ile nyumba igawiwe?


Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi baba alienda sehemu kwa starehe zake akifika huko kule kuna watoto, sheria inasema mtoto si haramu baba ndiyo haramu, itabidi arudi huku kwa bibi mkubwa akachukue mali ambazo alichuma mama huyu na mume wake. Mume aliyemvumilia miaka 40 mpaka 50, anarudi saa nane usiku, kichwa cha nyumba kinarudi kimeyumba, mama amevumilia, ameishi vizuri, ametunza watoto, analima, anaenda kulima mikorosho yake, amechangia nyumbani vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo anaambiwa yeye moja ya tatu tu, lakini watoto wote wenye jina la baba watapata mali hiyo. Hata hivyo, mali ya kule inaelezwa ni zawadi hadi ithibitike. Kwa nini mali ya baba huyu haijathibitika kule lakini watoto wamethibitishwa? Ni kitu gani kimethibitisha kuwa wale ni watoto wake ili hali hawakuthibitisha kama zile mali pia ni za mume wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kama ni hivyo sheria iseme mali ya huku na kule zirudi sehemu moja tugawane pamoja. Siyo shida; ila tugawane zote na tusiwe na kigugumizi kusema eti imekuwaje kwa sababu ile ina majina yake hakuna aliyeona hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtueleweshe hatuelewi tunagombana, tunapigana wanawake tunakuwa psychiatric tunatembea tunaongea peke yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta mama unamsalimia mama shikamoo anakwambia ona nimeachika talaka hii hapa, ameshapoteza akili. Mwanamke ni upendo kwenye jamii, leo Sheria ya Ndoa hii hii wanasema tumebadilisha na maneno yao, sheria ipo wazi, wanasema sheria iko wazi, wazi wapi? Mbona watu wetu hawaijui? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba uelewa iende huko kwenye vijiji. Wanasema sasa hivi kila mtu akiwa mwanaume na mwanamke wanachangiana wanaleta kitu pamoja; wewe unaonyesha ulichofanya na ulichochuma na mwenzako anaonyesha alichochuma, lakini unatakiwa uwe na ushahidi hata miamala.


Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mahusiano kuna wakati wa kuangalia na kutunza miamala? Muda huo mpo lele; miamala hii unaitunzaje? Tumefikia sehemu tunavyojenga nyumba nyumbani, kwanza mila za kiafrika mwanamke huwa ham-demote mwanaume, unacheza kikoba, unajinunulia mwenyewe marumaru unaweka kwenye nyumba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante.

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, unapoweka unamwambia fundi weka vizuri mume wangu amenituma. Kwa hiyo, tunaomba sheria hii imepinda...

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda.

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja na wind up moja tu…

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nyumba ya mrithi isiwekwe kwenye mirathi. (Makofi)